Na Eleuteri
Mangi, Maelezo
Bodi ya
Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Biashara Mashariki na Kusini mwa Afrika (PTA)
itakutana jijini Dar es Salaam.
Hayo yalibainishwa
jana mjini Dodoma
na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wasira,
alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya mkutano huo utakaofanyika
mwishoni wiki hii.
“Huu ni
mkutano wa kawaida wa mwaka wa Bodi ya Magavana wa nchi wanachama pamoja na
Mawaziri wa Fedha, Tanzania ni mwanachama ndio maana mkutano wa 30 unafanyika
hapa,” alisema.
Alisema katika
mkutano huo mada mbalimbali zitajadiliwa ikiwemo masuala ya fedha na uchumi,
maendeleo ya benki ya PTA na mafanikio yake kwa nchi washirika.
Alisema sio
kweli kwamba Tanzania
haikopesheki bali deni lililopo linahimilika.
Aidha alisema PTA
ni benki ya kiafrika na inafanyakazi nzuri ambapo inaonesha inakua kwa zaidi ya
asilimia 30 kwa mwaka kwa miaka kadhaa hadi sasa na imekuwa na mizania ya dola
za Kimarekani mil. 2.8 ikiwa miongoni mwa benki za maendeleo zinazofanya vizuri
katika bara hilo .
Alisema
mkutano huo utatanguliwa na semina ya wafanyabiashara itakayofanyika Agosti 21
siku moja kabla ya mkutano mkuu ambapo serikali itawakilishwa na Naibu Waziri
wa Fedha, Mwigulu Nchemba.
Kwa upande
wake Rais na Mtendaji Mkuu wa benki hiyo, Admassu Tadesse, alisema Tanzania imekuwa mstari wa mbele na ni
mwanachama hai ambapo imekuwa mfano mzuri kwa nchi wanachama kwa kutoa michango
mbali mbali kwa wakati.
Benki ya PTA
ilianzishwa mwaka 1985 ambapo hadi sasa ina jumla ya wanachama 22 ikiwemo nchi
18 ambazo ni Burundi, Comoros, Djibouti Congo, Kenya
na Malawi .
Nchi nyinine
ni Misri, Eritrea, Ethiopia, Mauritania, Rwanda, Seychelles, Somalia, Sudan,
Uganda, Zambia, Zimbabwe na
mwenyeji Tanzania .
Aidha, PTA
inashirikiana na nchi nyingine nje ya bara la Afrika ambazo ni Belarus na China .
Washirika
wengine ni Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Kampuni ya Bima ya Mauritia
iitwayo Eagle na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Mauritius .
Mkutano wa
mwaka huu unafanyikia Tanzania ikiwa ni utaratibu wa benkiya PTA kufanya
mikutano ya mwaka kwa mzunguko ambapo washiriki watakuwa Mawaziri wa Fedha,
Magavana wa nchi wanachama, sekta binafsi, Mabalozi wanaowakilisha nchi
mbalimbali nchini na Wawakilishi wa Mashirika ya kimataifa.
No comments:
Post a Comment