Habari za Punde

CC yabariki mchakato wa katiba Kinana apewa kazi kukutana na UKAWA

Na Fatina Mathias, Dodoma
Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi(CC) iliyokutana mjini Dodoma, chini ya Mwenyekiti wake Rais Jakaya Kikwete, imeridhishwa na mwenendo wa Bunge Maalum la Katiba na mijadala na hivyo kulibariki kuendelea na kazi yake.
Mbali na hilo pia imeagiza wanachama wake Mawaziri na Wabunge wasiohudhuria vikao vya bunge maalumu wahudhurie mara moja.

Kamati hiyo pia, imetangaza kuanzia sasa ziara za Rais zitakuwa na mawaziri wachache ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika vikao vya bunge hilo vinavyoendelea, ili kufanikisha upatikanaji wa katiba yenye maridhiano.

Akisoma maazimio ya CC kwa waandishi wa habari,Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema wanachokihitaji ni kuhakikisha wanamaliza jambo hilo lililopo mbele yao na kuendelea na mambo mengine, sio rahisi wajumbe kuhudhuria wote katika vikao hivyo.

Alisema Kamati Kuu imeeleza kuridhishwa na maendeleo ya majadiliano na upigaji kura katika Bunge hilo.

 “CC inawahimiza wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, kuhudhuria vikao vya kamati na vile vya Bunge na kushiriki katika mijadala kwa kutanguliza masilahi mapana ya taifa na hatimaye kuipatia nchi katiba inayotarajiwa na Watanzania wote,” alisema.

Alisema CCM inaridhishwa na namna wajumbe wa bunge maalumu wanavyoshiriki mijadala na kujenga hoja, pia wanavyoshughulikia mitazamo tofauti katika majadiliano yao na upigaji kura.


Hata hivyo, alisema Kamati Kuu imemuagiza  Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, kuendelea kukutana na vyama vya siasa vilivyokuwa katika mazungumzo ya maridhiano yaliyovunjika chini usimamizi wa Msajili wa vyama vya siasa nchini.

“Hata hivyo Kamati Kuu imesikitishwa na kuvunjika kwa mazungumzo kati ya CCM, CUF, CHADEMA  na NCCR-Mageuzi,”alisema Nnauye.

Kuhusu juhudi zinazofanywa na Kituo cha Demokrasia nchini(TCD), Kamati Kuu ilipongeza ushiriki wa Katibu Mkuu Kinana na vyama wanachama wa TCD, katika juhudi zinazolenga kuimarisha amani, utulivu, mshikamano na kuaminiana.

Alisema Kamati Kuu inaendelea kuwasii Watanzania wote kuendelea kushikamana na kuvumiliana, pale wanapopishana kimtazamo juu ya hoja mbali mbali za katiba.


“Tuvumiliane kwani amani, utulivu na utanzania wetu ni muhimu kuliko tofauti zetu za kimtazamo,” alisema.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.