Habari za Punde

Watoto wawaangukia wazee wao kurudu bunge la katiba

Na Fatina Mathias, Dodoma
KAMATI kuu ya Baraza la Watoto Tanzania, imewataka baba na mama zao wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kurudi bungeni ili kukamilisha kazi waliyoianza kwani ni pigo kubwa kwa watoto.

Tamko hilo lilitolewa jana na Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya baraza hilo,Ummy Jamaly, wakati akitoa tamko la baraza hilo mbele ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba.

Alisema watoto hawaridhishwi na mwenendo mzima wa bunge la katiba  hasa  kwa baadhi ya wabunge kususia mchakato huo na kuhatarisha ukamilishaji wa katiba ambayo ni muhimu kwa mustakabali wa watoto nchini.

“Kwa sababu yoyote ile kutokamilika kwa katiba ni pigo kubwa kwa watoto si tu kwa kuwa ni kundi kubwa la watu nchini bali pia ni muda mrefu haki za watoto hazikupata nafasi ya kutosha katika michakato mbalimbali ya jamii,” alisema.

“Tunatoa wito kwa baba na mama zetu wa kundi la UKAWA kurudi bungeni mara moja ili kukamilsha kazi hii muhimu kwa ajili ya taifa letu,” alisema.

Alisema katika kuhakikisha  haki za watoto zinaingizwa katika rasimu ya katiba mpya, wamefanya mikutano mingi ya ushawishi na viongozi mbali mbali wakiwemo wabunge wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pia baraza hilo ilimeomba haki za watoto zibaki katika katiba mpya kama ilivyotajwa kwenye rasimu ya pili ya katiba ibara ya 43.


Walitoa wito kwa wabunge wa bunge la katiba kuyapa kipaumbele mapendekezo ya watoto ambayo yalikuwa muhimu yawemo katika katiba mpya.

Aliyataja mapendekezo hayo ni malengo ya taifa, tafsiri ya mtoto, haki ya kupata elimu, haki ya kupewa jina, uraia, mtoto kutopewa adhabu kali ikiwemo viboko na mabaraza ya watoto kutambulika kikatiba.

Pia haki ya mtoto kupata huduma ya afya, wajibu wa mtoto, haki za wanawake,uwakilishi wa watoto bungeni, tume ya taifa ya haki za watoto, kuwepo na Wizara ya watoto tu na masuala ya muungano.

Kwa upande wake, Waziri Simba alisema wajumbe wa UKAWA wanaombwa kurudi bungeni ili wakubaliane na kupiga kura kama wakiridhia.

Alisema rasimu ya Jaji Joseph Warioba iliweka vipengele vyenye maslahi kwa watoto na sasa vinajadiliwa kwenye kamati na katiba itabeba mambo yenye maslahi kwao.

“Tumekubaliana mtoto ni yule aliye na umri chini ya miaka 18 na suala la watoto kuchapwa viboko litawekwa kwenye sheria,” alisema.


Alisema sasa serikali haina uwezo wa kuweka wizara itakayoshughulikia masuala ya watoto pekee.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.