Habari za Punde

Dk.. Shein:Tutaendelea Kuhakikisha Malengo ya Elimu katika Mipango Yote ya Maendeleo Yanatekelezeka

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                                                       23 Septemba, 2014
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewahakikishia wananchi wa Zanzibar kuwa Serikali imejidhatiti kuhakikisha kuwa malengo yote katika mipango ya maendeleo ya nchi yanayohusu uimarishaji wa elimu yanafikiwa na kutoa matokeo yanayotarajiwa.
Akihutubia maelfu ya wananchi katika kilele cha Maadhimisho ya Miaka 50 ya Elimu bila Malipo yaliyofanyika kwenye uwanja wa Amaan mjini Unguja leo, Dk. Shein amesema Serikali inatambua kuwa mafanikio ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya nchi yanategemea kuimarika kwa kiwango cha elimu hivyo ndio maana suala la uimarishaji wa elimu limepewa kipaumbele katika mipango mbalimbali ya maendeleo.
Aliitaja mipango hiyo kuwa ni pamoja na Dira ya Maendeleo 2020, Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA II),Mpango wa Maendeleo ya Elimu, Malengo ya Milenia ya Elimu na Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2010.
Katika kufanya hivyo, aliwaambia wananchi kuwa Serikali itaendelea kuongeza nafasi za masomo katika viwango vyote kuanzia skuli za maandalizi hadi chuo kikuu ili kutoa fursa kwa kila mtoto kupata elimu katika ngazi zote.    
Sambamba na kuongeza fursa za masomo, kwa upande mwingine alisema Serikali inafanya jitihada kubwa kuhakikisha ubora wa elimu inayotolewa katika ngazi zote unazidi kuongezeka kwa kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mazingira ya utoaji elimu nchini.
Alizitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na kuzipatia skuli vifaa na nyezo za kisasa za kufundishia ikiwemo vitabu, vifaa vya maabara, kompyuta na walimu bora ili kuwawezesha wanafunzi kufaulu masomo yao vyema.
Dk. Shein alitoa mfano wa hatua mzuri iliyofikiwa katika kuwapatia wanafunzi vitabu katika skuli za sekondari ambapo alieleza kuwa kushirikiana na Benki ya Dunia na Serikali ya Marekani hivi sasa kila mwanafunzi katika ngazi hiyo ana vitabu vya masomo anavyovidhibiti mwenyewe na kwenda navyo nyumbani.
Katika hotuba yake hiyo, Dk. shein alitoa wito kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuendeleza juhudi za ufundishaji wa taaluma ya tekinolojia ya habari na mawasiliano katika skuli za Unguja na Pemba ili Zanzibar iweze kwenda sambamba na maendeleo na mabadiliko ya karne 21 ambayo yanazingatia matumizi ya tekinolojia hiyo.
Hata hivyo ameitaka wizara hiyo kuwa mstari wa mbele katika kudhibiti matumizi kwa kutunga kanuni zinazokataza matumizi mabaya ya mitandao na simu za mikononi kwa wanafunzi maskulini.
Kuhusu maslahi ya walimu, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliwahakikishia walimu kuwa Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi kwa kuwapatia mafunzo zaidi pamoja na kuwaongezea mishahara kadri uchumi unavyokua na hali inavyoruhusu.
Dk. Shein alizungumzia pia suala la ukosefu wa ajira kwa wahitimu wengi wanaomaliza vyuo mbali mbali huku akitambua changamoto inayowakabili wengi wa wahitimu hao ya kukosa maarifa ya kutosha kujiajiri hivyo kutegemea ajira.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Awali Bibi Zahra Ali Hamad alieleza mafanikio mbalimbali yaliyopatikana katika sekta ya elimu na kuongeza kuwa ongezeko kubwa la bajeti ya elimu mwaka hadi mwaka ni hatua inayodhihirisha umakini wa Serikali katika kuimarisha elimu nchini.
Tarehe kama leo 1964, miezi tisa baada ya Mapinduzi ya Zanzibar, Rais wa kwanza wa Zanzibar marehemu Sheikh Abeid Amani Karume alitangaza elimu bila malipo kwa kila mwananchi na kuondosha kabisa ubaguzi katika mfumo wa elimu Zanzibar.
Mapema Rais wa Zanzibar na Mwenyekiri wa Baraza laMapinduzi alipokea maandamano ya wanafunzi kutoka skuli mbalimbali za Unguja na Pemba na baadae kufuatiwa na burudani za vikundi vya sanaa na michezo.    

Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.