Habari za Punde

Gharama za uendeshaji zachangia bei ya ukulima wa matrekta kupanda

Na Maryam Talib, Pemba
ONGEZEKO la gharama za uendeshaji ikiwa ni pamoja na bei ya mafuta, imetajwa ndio sababu ya kuondolewa ruzuku ya ukulima wa matrekta kwa wakulima wa mpunga kisiwani hapa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Ofisa Mkuu Kilimo Pemba, Amour Juma Mohammed, alisema awali serikali ilikuwa ikiwalimia wakulima kwa bei ya shilingi 16,000 kwa ekari moja, huku ikifidia baadhi ya gharama.

Lakini kutokana na ongezeko la gharama za uendeshaji wa matrekta zinazojumuisha vipuri na mafuta, ilisababisha wasimamizi wa kilimo cha matrekta kurejesha gharama katika uhalisia wake.

Alisema iwapo wangeendelea kubakisha bei hiyo, wasingemudu kuwafikia wakulima wote waliokuwa wakihitaji huduma hiyo kwa vile gharama zilikuwa kubwa kuliko uwezo wa kuendesha.

Alisema hali hiyo ndio iliyosababisha bei ya kulima kupanda kutoka shilingi 16,000 hadi shilingi 32,000 na kwamba maamuzi hayo yalifikiwa kwa makaubaliano na maofisa wa kilimo 
wanaoshughulika na ukulima wa matrekta.


“Kwa miaka mitatu kuanzia 2011 serikali ilitoa ruzuku ya punguzo la ukulima, kwa bahati msimu wa mwaka 2014 ruzuku ile ya mfuta ilikuwa imemalizika na sisi kama viongozi tukaona tuongeze bei kidogo ili wakulima waweze kulimiwa,”alisema.

Baadhi ya mabwana shamba na maofisa wa kilimo wilaya za Pemba, walisema ruzuku ya mafuta imekuwa kikwazo wakati msimu wa kilimo unaofika.

Hamad Ali Hassan alisema wakulima wamekuwa hawajui matatizo hayo, bali wanachokifahamu wao ni kulimiwa na kwamba inaweka mkazo zaidi kwenye kilimo.

Mratibu wa pembejeo wilaya ya Wete, Hamad Ali Hassan, alisema mafuta wanayopewa ni tofauti na Unguja, kwani Pemba maeneo mengi ni mabonde wakati Unguja maeneo mengi ni tambarare.

Nassor Hamad Khamis, ambaye ni bwana shamba wilaya ya Wete, alisema licha ya mafuta, usumbufu mwengine ni upatikanaji wa matrekta, kwani yaliyopo hayatoshi kutokana na idadi ya wakulima wanaohitaji huduma hiyo.

Alisema wakati mwengine matrekta huharibika hali inayorudisha nyuma na kuvunja matumaini ya wakulima msimu unapofika.
Alisema serikali inapaswa kutengeneza matrekta hayo ili kuondoa usumbufu kwani hali ya ulimaji kwa kutumia jembe la mkono umekuwa tatizo.

Naye Nassor Mwalim Kai bwanashamba, alisema serikali inapaswa kuweka kipaumbele katika kutoa mafuta kwa wakati.
Hamad Omar Mohamed, mkuu wa kitengo cha Ufundi na Uhifadhi wa zana za kilimo Pemba, alisema kitengo chake kinakabiliwa na uchakavu wa matrekta na kusababisha kufanya kazi kwa kiwango cha chini.

Alithibitisha kwamba mtrekta mapya yalikuja katikati ya msimu wa mwaka huu na kusema yanafanya kazi lakini nguvu zake ni ndogo tofauti na makongwe yaliyopo.

Alisema uwezo wa trekta kwa siku linaweza kulima ekari nane mpaka 12 lakini kutokana na uwezo mdogo pamoja na ugumu wa ardhi hulima ekari 5 hadi sita.

Ali Mohamed Omar Mkuu wa Idara ya Uhakika wa Chakula na Lishe Pemba, alisema idara hiyo ipo na imeanzishwa kwa sheria namba 5 ya mwaka 2011 na tayari imeshateua baadhi ya wafanyakazi na kutolewa miongozo.

Amour Juma Mohammed, Ofisa Mkuu Kilimo Pemba, alisema msimu uliopita serikali haikuongeza mafuta katika bajeti yao, huku wilaya za Micheweni, Wete na Chake Cheke kwa msimu uliopita zimepata mavuno madogo.


Mratibu wa Pembejeo za Kilimo wilaya ya Chake Chake, Mohammed Khamis Haji, aliiomba serikali kununua majembe mapya ya kulimia kuliko kununua vipuri vya kutengeneza. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.