Na Mwandishi wetu
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, amewaongezea muda wa miezi sita viongozi
na wasimamizi wa ujenzi wa maabara katika skuli za sekondari nchini, ili
kuwawezesha kukamilisha kazi hiyo ipasavyo.
Aidha alitoa pongezi kwa
wananchi wa Tanzania na viongozi kwa kazi kubwa waliyoifanya katika ujenzi wa
maabara nchini.
Alisema anachangia shilingi milioni
200 katika Mfuko Maalum wa Dhamana (Endowment Fund For Excellence) wa Taasisi
ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela.
Alisema hayo jana wakati
alipozungumza na uongozi, wahitimu na wana-jumuiya ya taasisi hiyo, baada ya
ametunukiwa shahada ya uzamivu ya heshima (PhD honoris causa) ya taasisi hiyo
katika mahafali ya pili yaliyofanyika Tengeru, Arusha.
Alitunukiwa shahada hiyo na
Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Mhe.Mohamed Gharib
Bilal ambaye ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Taasisi ya Sayansi na
Teknolojia ya Nelson Mandela ni chombo cha elimu ambacho hutoa wahitimu wa shahada
za uzamili na uzamivu (PhD) tu katika sayansi na teknolojia na ni moja ya
taasisi mbili tu za aina hiyo katika bara la Afrika.
Pia alizungumzia maendeleo ya
ujenzi wa maabara ya masomo ya sayansi nchini ambalo lengo lake ni kutekeleza
agizo lake la kuhakikisha skuli zote za sekondari nchini zinajenga maabara ya
kufundishia masomo ya sayansi.
Alitoa agizo hilo miaka miwili
iliyopita, Novemba 2012 na akatoa miaka miwili kukamilisha kazi hiyo ifikapo
Novemba 30 mwaka 2014.
Alitoa agizo hilo baada ya
kubaini kuwa ukosefu wa maabara kwa ajili ya masomo ya fikizia, kemia na
biolojia ilikuwa moja ya sababu ya kuwakatisha tamaa wanafunzi nchini kupenda
masomo ya sayansi.
Alisema umuhimu wa kujenga
maabara uliongezwa kasi na ongezeko kubwa la skuli za sekondari ambazo
ziliongezeka kutoka 828 mwaka 2004 hadi kufikia 3, 551 kwa sasa.
Kati ya hizo ni 88 zilizokuwa
na vyumba vitatu kwa ajili ya masomo hayo matatu ya sayansi.
Alisema tathmini ya sasa
inaonesha kuwa zinatakiwa zijengwe maabara kwenye skuli 3,463 ambazo ni sawa na
vyumba 10,389 na kuwa tathmini hiyo inaonesha hadi Disemba 7, 2014, vilikuwa
vimejengwa vyumba 3,867 vya maabara ambavyo ni sawa na asilimia 37.2 ya
mahitaji ambavyo vimekamilika, vyumba 5,891, sawa na asilimia 56.7 ambavyo viko
katika hatua mbali mbali za kukamilishwa na vyumba 631 ama sawa na asilimia 6.1
ambavyo ujenzi wake haujaanza.
No comments:
Post a Comment