Habari za Punde

MFUMUKO WA BEI UMEPUNGUA- OFISI YA TAIFA YA TAKWIMU.

Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Ephraimu Kwesigabo akitoa taarifa ya kupungua kwa mfumuko wa bei nchini kwa mwezi Novemba, 2014 leo jijini Dar es salaam.



Na. Aron Msigwa – MAELEZO.Dar es salaam.
Ofisi ya Taifa ya Takwimu imesema kuwa Mfumuko wa Bei wa Taifa kwa mwezi Novemba, 2014 umepungua hadi kufikia asilimia 5.8 kutoka 5.9 iliyokuwepo mwezi Oktoba ,2014 kutokana na kupungua kwa kasi ya bei ya bidhaa na huduma katika maeneo mbalimbali nchini.

Akitoa taarifa ya mfumuko wa bei kwa  waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa  Sensa na Takwimu za Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Ephraim Kwesigabo amesema kuwa kupungu kwa mfumuko wa Bei nchini kumesababishwa na kupungua kwa bei za bidhaa za vyakula na zile zisizo za vyakula. 

Amezitaja bidhaa za vyakula zilizochangia kupungua kwa mfumuko wa bei nchini kuwa ni pamoja na Unga wa mahindi , unga wa ngano, tambi na vyakula vya lishe kwa watoto.

Bidhaa nyingine ni mavazi ya wanaume zikiwemo suti, suruali, sare za shule na viatu vya wanaume huku bidhaa za gesi, mafuta ya taa, mkaa, mazulia, vyandarua pamoja na simu na saa za mkononi zikichangia kwa asilimia 17.2.

Kuhusu Fahirisi za bei kwa maana ya kiwango cha badiliko la kasi ya bei  za makundi ya bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na Kaya binafsi kwa kuzingatia kipimo cha mwezi amesema kuwa zimeongezeka hadi kufikia 150.54 mwezi Novemba kutoka 149.70 za mwezi Oktoba, 2014.

Amefafanua kuwa kuongezeka kwa Fahirisi hizo kumechangiwa na ongezeko la bei ya bidhaa za vyakula hususan mchele, vitafunwa vinavyotokana na unga wa ngano,samaki, matunda,mbogamboka,viazi mviringo, mihogo na viazi vitamu.

Akizungumzia uwezo wa shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma za mlaji kwa mwezi Novemba , 2014 amesema kuwa umefikia shilingi 66 na senti 43. 

“Uwezo wa shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma kwa mlaji umepungua ,hii inamaanisha  mtu anahitaji kuongeza ziada  ya shilingi 33 ili aweze kununua bidhaa na huduma zilezile anazozihitaji”

Kwa upande wa mfumuko wa Bei wa mwezi Novemba 2014 katika nchi za Afrika Mashariki amesema  kuwa una mwelekeo unaofanana , Kenya ukipungua  kwa asilimia 6.04 kutoka asilimia 6.43 za mwezi Oktoba, Uganda  mfumuko wa bei ukiongezeka hadi asilimia 2.1 kutoka asilimia 1.8 za mwezi Oktoba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.