Habari za Punde

Kutoka Baraza la wawakilishi: Wananchi watakiwa kutokata misitu na kuchimba michanga ovyo


Na Abdulla Ali Maelezo-Zanzibar                                              28/01/2015

 

Naibu Waziri wa Kilimo na Maliasili Zanzibar Mhe. Mtumwa Kheir Mbarak amewataka wananchi kutokata misitu ya asili na kuchimba mchanga ovyo kwani ndizo sababu zinazopelekea mabadiliko ya Tabianchi.

Hayo ameyaeleza katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja wakati akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Wawi Mhe. Saleh Nassor Juma.

Mhe. Mtumwa amesema ukataji wa misitu ya asili pamoja na uchimbaji mchanga ovyo husababisha kukosekana kwa mvua za misimu na kuathiri maisha ya wakulima na wananchi kwa ujumla.

Amesema ikiwa wananchi wataendelea kukata misitu ya asili hususan mikoko ambayo huzuia upepo wa Bahari na kupandisha kina cha maji, kutapelekea Visiwa vya Zanzibar kukatika vipandevipande na maji kujaa hadi katika makaazi ya watu kama ilivyo hivi sasa kwa baadhi ya vijiji hapa zanzibar.  

“Na athari za ziada zitafuata baadae ikiwa wataendelea kukata hasa mikoko ambayo inazuia upepo wa Bahari na kupandisha kina cha maji, matokeo yake visiwa vitakatika vipande vipande na maji yatapanda mpaka viamboni (katika makaazi ya watu) na mfano hai hayo sasa yanatokea katika vijiji vya Jozani, Mziwanda, Koowe na kwengine kwingi”, alieleza Naibu Waziri Mtumwa.


Aidha ametanabahisha kuwa Serikali imechukua juhudi mbalimbali katika kuhakikisha kwamba athari za mabadiliko hayo zinapungua, miongoni mwa juhudi hizo ni kuanzishwa vikundi mbalimbali vya jamii husika kwa matakwa yao wenyewe kutunza misitu ya asili iliopo katika maeneo yao wanayoishi Unguja na Pemba, Udhibiti wa msumeno wa moto kutotumika mpaka kwa ruhusa na kibali maalumu.

Sambamba na hayo Mhe. Mtumwa amesema kuwa Serikali imeanzisha miradi mbalimbali ili kuondokana na tatizo hilo ikiwemo mradi wa TASAF unaojishughulisha na mpango wa kujenga miundombinu ya umwagiliaji maji ambao umesaidia umwagiliaji kwa kilimo cha Mpunga, Mboga na Matunda, pia wakulima kusomeshwa njia bora za ukulima na kuwapa fedha za kuanzishia mashamba kupitia mradi wa PADEP, ASSP na ASDPL.

Akiongezea Mhe. Mtumwa amesema serikali imeanzisha sheria maalumu za kuzuia ukataji wa miti ovyo ikiwemo sheria ya COFMA ambayo imetungwa ili kudhibiti wanaoharibu misitu kiholela.

Mhe. Mtumwa amewataka viongozi na wananchi kwa ujumla kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupiga vita ukataji wa misitu ya asili na uchimbaji mchanga ovyo ili kuondokana na janga la Tabianchi na ukosefu wa mvua za misimu na kutilia mkazo kilimo cha kisasa pamoja na upandaji wa miti.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.