Habari za Punde

Kutoka Baraza la wawakilishi: Wananchi watakiwa kujiepusha na vitendo vya uhalifu


Na Abdulla Ali Maelezo-Zanzibar                                              28/01/2015

Wananchi wametakiwa kujiepusha na vitendo vya kihalifu ili kuepusha uvunjifu wa amani nchini.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais Mhe. Mohamed Aboud Mohamed katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja wakati akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Mtambwe Mhe. Salim Abdalla Hamad.

Amesema endapo mtu atatuhumiwa kutenda vitendo hivyo vya kihalifu sheria zitatumika bila ya kumuonea au kumkandamiza mtu yeyote ili kuhakikisha amani na utulivu inabakia na kudumishwa nchini.

Amefafanua kuwa ni utaratibu wa kisheria katika nchi za Jumuiya ya Madola kwamba nchi ina mamlaka ya kumfikisha muhalifu mahakamani na kumshitaki iwapo tukio husika la kihalifu limetokea katika nchi hiyo, hivyo endapo tukio la uhalifu limetokea Tanzania Bara na endapo limetokea Zanzibar, mahakama za Zanzibar pia zinaweza kuwashitaki watuhumiwa hao.

Ametanabahisha kuwa Katiba ya Zanzibar ya 1984, kifungu cha 101 kinaweka masharti ya kikatiba ya utaratibu wa utekelezaji wa hati za mahakama ndani ya Zanzibar na Tanzania Bara kwa ujumla na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 124 imeweka masharti kama yaliyomo kwenye kifungu cha 101 cha Katiba ya Zanzibar.


Waziri Aboud amesema kwa mujibu wa masharti ya vifungu vya katiba vilivyotajwa ni utaratibu halali wa kisheria wa mtuhumiwa kukamatwa upande mmoja wa Muungano na kupelekwa upande mwengine wa Muungano endapo uhalifu umetokea na kutendwa katika eneo husika.

Aidha Waziri Aboud amefafanua kuwa misingi ya katiba zote mbili kuna utaratibu pia wa kisheria ambapo Mzanzibari au Mtanzania yeyote ambae atatuhumiwa kutenda kosa lolote la uhalifu nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anaweza kukamatwa na kupelekwa nchi ambayo atatuhumiwa kutenda kosa na kushitakiwa.

Amesema Sheria hizo ni Sheria ya kubadilishana wahalifu Sura ya 368 (Extradition Act Cap. 368) na Sheria ya kusaidiana katika mambo ya jinai Sura ya 254 (The Mutual Assistance in Criminal Matters Act Cap. 254) sheria hizo zote zinaweka masharti na utaratibu wa kubadilishana wahalifu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.