Na Abdulla Ali na Mwanaisha
Moh’d Maelezo-Zanzibar
Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ Mhe. Haji Omar Kheri amesema Serikali
itaendelea kutoa elimu madereva wa
daladala ili waweze kufuata sheria za barabarani na kuepusha ajali zisizo za
lazima.
Hayo ameyaeeleza katika
ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja wakati
akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Wawi Mhe. Saleh Nassor Juma.
Amesema Serikali imeamua
kutoa elimu hiyo kutokana na baadhi ya madereva wa daladala kuwa wakaidi wa
kufuata na kutii sheria, jambo linalopelekea kuwepo kwa misongamano ya gari
isiyo ya lazima katika vituo vya daladala, ambapo hurejesha nyuma harakati za
abiria wakati wa safari zao.
Aidha Waziri huyo
ameliomba Jeshi la Polisi kusimamia sheria za
barabarani kikamilifu ili kuepusha ajali za mara kwa mara na zisizo za
lazima.
Wakati huo huo nae
Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii, na Michezo Mhe. Bihindi Hamad Khamis
amesema Serikali ina mpango wa kujenga viwanja vya kisasa vya mpira wa miguu na
mikono kwa kila Mkoa wa Zanzibar.
Amesema kwa sasa Serikali
imeshaanza mchakato wa kujenga viwanja vya
mikoa ya Kaskazini Pemba na Kaskazini Unguja ambapo kwa upande wa Kaskazini
Unguja kitajengwa katika kijiji cha Nungwi na kwa upande wa Kaskazini Pemba kitajengwa
katika kijiji cha Kinyasini.
Amefahamisha kuwa lengo
la kujenga viwanja hivyo ni kukuza Sekta ya Michezo na hadi sasa Baraza la Michezo
Zanzibar limeshasajili rasmi vyama 33 vya michezo kwa ajili ya kuunga mkono
hatua hizo za kukuza sekta za michezo nchini.
Vile vile amempongeza Mwakilishi
wa Jimbo la Uzini Mhe. Mohamedraza kwa kuwa mstari wa mbele katika kukuza Sekta
ya Michezo Nchini kwa kujenga viwanja 2 vya mpira wa miguu vyenye Taa katka Jimbo lake na kuwataka viongozi
wengine wa Serikali na Sekta Binafsi
kuiga mfano huo.
No comments:
Post a Comment