Habari za Punde

Serekali Itaendelea Kutoa Elimu kwa Madereva wa Daladala.

Na Abdulla Ali na Mwanaisha Moh’d Maelezo-Zanzibar        
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ Mhe. Haji Omar Kheri amesema Serikali itaendelea kutoa elimu madereva  wa daladala ili waweze kufuata sheria za barabarani na kuepusha ajali zisizo za lazima.

Hayo ameyaeeleza katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja wakati akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Wawi Mhe. Saleh Nassor Juma.

Amesema Serikali imeamua kutoa elimu hiyo kutokana na baadhi ya madereva wa daladala kuwa wakaidi wa kufuata na kutii sheria, jambo linalopelekea kuwepo kwa misongamano ya gari isiyo ya lazima katika vituo vya daladala, ambapo hurejesha nyuma harakati za abiria wakati wa safari zao.

Aidha Waziri huyo ameliomba Jeshi la Polisi kusimamia sheria za  barabarani kikamilifu ili kuepusha ajali za mara kwa mara na zisizo za lazima.


Wakati huo huo nae Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii, na Michezo Mhe. Bihindi Hamad Khamis amesema Serikali ina mpango wa kujenga viwanja vya kisasa vya mpira wa miguu na mikono kwa kila Mkoa wa Zanzibar.

Amesema kwa sasa Serikali imeshaanza mchakato wa kujenga viwanja vya   mikoa ya Kaskazini Pemba na Kaskazini Unguja ambapo kwa upande wa Kaskazini Unguja kitajengwa katika kijiji cha Nungwi na kwa upande wa Kaskazini Pemba kitajengwa katika kijiji cha  Kinyasini.

Amefahamisha kuwa lengo la kujenga viwanja hivyo ni kukuza Sekta ya Michezo na hadi sasa Baraza la Michezo Zanzibar limeshasajili rasmi vyama 33 vya michezo kwa ajili ya kuunga mkono hatua hizo za kukuza sekta za michezo nchini.

Vile vile amempongeza Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mhe. Mohamedraza kwa kuwa mstari wa mbele katika kukuza Sekta ya Michezo Nchini kwa kujenga viwanja 2 vya mpira wa miguu vyenye Taa  katka Jimbo lake na kuwataka viongozi wengine  wa Serikali na Sekta Binafsi kuiga mfano huo.            


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.