Habari za Punde

Maazimio ya mkutano wa Amani Zanzibar

MAAZIMIO YA MKUTANO WA AMANI ZANZIBAR ULIOFANYIKA KUANZIA TAREHE 19 HADI 20 SEPTEMBA 2015 KATIKA HOTELI YA ZANZIBAR BEACH RESORT –ZANZIBAR
Bismillahir Rahmaanir Rahym
1.  Ofisi ya Mufti kwa kushirikiana na Friends of Zanzibar, ziandae utaratibu kuhakikisha mafunzo ya Mkutano huu yanafika katika wilaya zote za Unguja na Pemba.

2.  Ofisi ya Mufti ichukue jukumu la kuyawasilisha Maazimio ya Mkutano huu kwa Viongozi Wakuu wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa pamoja na Taasisi nyengine zote muhimu katika kutunza amani nchini.

3.  Tume ya Uchaguzi Zanzibar, iwajibike katika kusimamia na kuendesha Uchaguzi ulio huru, haki, uadilifu na uwazi ili kuepusha visababishi vya uvunjaji wa amani nchini.

4.  Tume ya Uchaguzi Zanzibar pamoja na taasisi nyengine husika, wavifanyie kazi kwa haraka VIASHIRIA VYA UVUNJAJI WA AMANI vilivyosababisha uvunjaji wa amani na machafuko katika chaguzi zilizopita.

5.  Serikali na Mamlaka zinazohusika na utunzaji wa amani, wawe waadilifu na kutumia busara katika kukabiliana na matukio ya uvunjaji wa amani ili kuepusha mizozo isiyo ya lazima nchini.

6.  Viongozi wa Siasa, Viongozi wa Dini, Walimu wa Madrasa, Walimu wa Skuli, Wahadhiri wa Vyuo Vikuu na Wakufunzi wajiepushe kutumia kauli zinazoweza kuwachochea wafuasi na wanafunzi wao kuingia katika kuvunja amani ya nchi.

7.  Viongozi wa Dini wawaelimishe Wazanzibari kushikamana na Misingi ya Dini yao inayohimiza AMANI pamoja na kufanya juhudi za kurudisha hadhi ya kihistoria ya Zanzibar kama chimbuko la ELIMU, MAENDELEO na USTAARABU.

8.  Viongozi wa Dini wawe waadilifu hasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu kwa kuepuka ushabiki wa kivyama ili kulinda hadhi na heshima yao.

9.  Washiriki wa Mkutano huu, Waandishi wa Habari na Wadau wote wa Uchaguzi, waichukue na kuitangaza Kauli Mbiu ya Mkutano huu inayosema “UCHAGUZI UTAPITA, ZANZIBAR ITABAKIA, PIGA KURA KWA MAENDELEO NA AMANI ENDELEVU”.


10.             Waandishi wa habari wazitumie kalamu zao vizuri kushajiisha jamii kudumisha AMANI kuelekea Uchaguzi Mkuu na wasikubali kutumiwa kuchochea chuki, uadui na migawanyiko itakayopelekea machafuko ya nchi.

11.             Friends of Zanzibar kwa kushirikiana na Ofisi ya Mufti iwe tayari kuwajengea uwezo Wanawake kupitia Taasisi zao ili kushiriki kikamilifu katika kushajiisha ujumbe wa AMANI, UTULIVU na MSHIKAMANO miongoni mwa Wazanzibari.

12.             Friends of Zanzibar, Ofisi ya Mufti na taasisi nyengine za dini, wawajengee uwezo Walimu wa Madrasa ili kutekeleza jukumu la malezi ya watoto na vijana kwa azma ya kuwa na raia wema wa sasa na baadaye.

13.             Friends of Zanzibar, Ofisi ya Mufti na taasisi nyengine, wawe tayari kujenga uwezo wa vijana kimaadili na kiuchumi ili kuwafanya watumike katika kuleta maendeleo ya nchi.


14.             Friends of Zanzibar na Ofisi ya Mufti kwa kushirikiana na Taasisi nyengine za Kiislamu, waandae mpango kazi wa utekelezaji wa Maazimio haya.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.