STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba 3.10.2015
MGOMBEA nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM na Makamu
Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameibomoa ngome ya CUF huko Kiungoni
Pemba na kuvuna wanachama zaidi ya 40 huku akiwaleleza wananchi kuwa siasa za
chuki, fujo na hasama zimeshapitwa na wakati hapa nchini na yeyote
atakaezirejesha sheria itachukua mkondo wake.
Hayo aliyasema leo katika Mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM uliofanyika kiungoni
katika Jimbo la Mgogoni, Mkoa wa Kaskazini
Pemba ambao umehudhuriwa na maelfu ya wanaCCM na wananchi ambapo mgeni rasmi
alikuwa mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohamed Shein.
Dk. Shein alisema kuwa Tanzania ikiwemo
Zanzibar kuna amani na utulivu mkubwa na kuwathibitishia wananchi kuwa amani
hiyo imesimamiwa na kuandaliwa na Mwenyewezi Mungu pamoja na vyombo vya dola na
Serikali iliopo hivyo si rahisi kuazisha vurugu na fujo.
Alisema kuwa siasa za vyama vingi
isiwatenganishe Wazanzibari kwani kila mtu ana chama chake na kuwataka wananchi
wasihujumiane wala kufanyiana fujo kwa sababu za itikadi za kisiasa kwani
sheria inasema kila mwananchi ana fursa ya kupenda chama anachokitaka.
Dk. Shein alisema hayo baada ya gari ya
wafusi wa CCM kupigwa mawe wakati wakirudi mkutanoni Gando na kusisitiza kuwa siasa
ya vyama vingi sio fujo ambapo aliwaeleza vijana wanaotaka kuvunja amani ya
Zanzibar na kuleta vurugu wakati wa uchaguzi wajue hilo haliwezekani na mwenye
nia ya kutafanya ajue kuwa vyombo vya dola na dola viko macho.
Alisema kuwa uchaguzi wa amani ndio
unaotakiwa "tunataka Zanzibar iwe na utulivu wakati wote na kusihini watu
wote waishi kwa amani na utulivu, Zanzibar na watu wake hawataki
fujo",alisema Dk. Shein.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa panapozuka
zahama hata ibada hazifanyiki wala jambo lolote la maendeleo na kueleza kuwa mtu
yeyote atakaejaribu kufanya fujo hapa Zanzibar atashughulikiwa na kuwataka
wananchi kuishi vizuri na kufanya siasa bila ya kugombana pamoja na kufanya
kampeni za kistaarabu.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza
vijana waliojiunga na CCM na kusema kuwa anaamini kuwa wataungana na vijana
wenzano wa CCM kwa lengo la kuiletea maendeleo nchi yao.
Alisema kuwa elimu imeimarika sana,
ujenzi wa majengo mapya ya msingi na Sekondari kama Kiuyu Minugwini, kuanzishwa
kwa Tawi la Chuo Kikuu Pemba katika chuo cha Penjamin Wilium Mkapa na kusema
kuwa huduma za chuo hicho katika miaka mitano ijayo zitaimarishwa.
Kwa upande wa sekta ya afya alisema kuwa Kojani,
huduma za meno zitapelekwa kwani huduma
za afya katika Jimbo la Kojani zimeimarika ikiwa ni pamoja na kujenga nyumba za
daktari na kuendelea kuahidi kuwa katika miaka miwili ya uongozi wake huduma za
fya zitakuwa bure.
Aidha, alisema kuwa katika mwaka wake wa
kwanza elimu ya Sekondari nayo itakuwa bure na kueleza kuwa huduma za maji
zimeimarika Kangagani na Kiuyu na Shehia zote za Kojani zitapata maji safi na
salama katika miaka mitano ya uongozi wake.
Alisema kuwa mji wa Chake, Mkoani na Wete
huduma za maji zimeimarika na kiwango cha maji Mkoa wa kaskazini Pemba
zimeimarika zaidi hivi sasa na lengo ni ifikapo mwaka 2018 huduma hiyo
zitafikiwa asilimia 100.
Alieleza kuwa sekta ya miundombinu ya
barabara katika Mkoa huo wa Kaskazini imeimarika kwa kiasi kikubwa na kila
pahala katika barabara kuu zimetiwa lani na ni barabara za kisasa na hivi
karibuni barabara kutoka Wete hadi Chake itajengwa upya mapema hapo mwakani.
Akigusia sekta ya umeme alisema kuwa
sekta hiyo imeimarika kwa kiasi kikubwa na kuahidi kupelekwa umeme katika
maeneo yote yaliobaki ndani ya miaka mitano ijayo.
Dk. Shein alisema kuwa mafanikio yote
yaliopatikana tokea Mapinduzi yametokana na ASP na CCM, huku akieleza kuwa
serikali imekuwa ikiwatekelezea wananchi maendeleo na kuwatumikia bila ya
ubaguzi.
Aliwataka wananchi kumchagua kwani
ataendelea kuwapelekea maendeleo zaidi.
Pamoja na hayo Dk. Shein alisema kuwa
wakati akiomba ridhaa katika uchaguzi uliopita alisema kuwa pindipo wananchi
wakimchagua Serikali ya Umoja wa Kitaifa ataiendesha vizuri kwa kufuata
taratibu zote ikiwa ni pamoja na sheria na Katiba ya Zanzibar.
Alisema kuwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa
ameiendesha kwa bidii kubwa na kushangwazwa na kauli zinazotolewa na viongozi
wa CUF kuwa chama hicho hakikutendewa haki wakidai kuwa wanataka na wao wawe na
Wakuu wa Mikoa na Masheha wakati Katiba haielekezi hivyo.
Katika kuiongoza Serikali hiyo alisema
kuwa kila kitu kimefanywa pamoja, na hakuna jambo la kiserikali aliloamua peke
yake kwani katika maamuzi huwashirikisha viongozi wote wa ngazi za juu akiwemo Makamu wa Kwanza wa Rais, Makamu wa Pili
pamoja na Wajumbe wote wa Baraza la Mapinduzi.
Dk. Shein alieleza kuwa hata suala la kutafuta
ufumbuzi wa Uwamsho baada ya kufanya vurugu walikubaliana na kushaurinana na viongozi
wote wa Serikali wakiwemo viongozi wa CUF lakini anashangaa kuwa hilo hawalisemi.
"sina ninaemchukia wala kumuonea kwani
hata mimi mwenyewe nafuata sheria... wanajua watashindwa na wanatafuta sababu
lakini nawaambia kuwa uchaguzi utafanyika na CCM intashinda.. na mimi nikiwa
Rais nitawatumikia wote"
Pamoja na hayo aliahidi kuiimarisha sekta
ya kilimo na uvuzi na kuwataka wavuvi wakae mkao wa kula kwa kuanza kuvua
kisasa.
"Tutagawa vihori, boti za kisasa,
kiwanda kikubwa cha kuvua samaki Unguja kitajengwa na nitamshwawishi muekezaji kuja
kujenga kiwanda na Pemba sambamba na kuwapa mitaji wavuvi",alisema Dk.
Shein.
Alisema kuwa Serikali itaagiza matrekta
mia moja na tayari mchagkato wa kuja kushughulikia sekta ya uvuvi na washirika
wengi wa maendeleo wameahidi kuja kuekeza Zanzibar.
Alieleza kua tokea mwaka 2001 hadi 2010
ameanza kulishughulikia suala la mafuta tokea akiwa Makamu wa Rais hadi hii leo
na hakuna hata mmoja atakae sema kafanya yeye.
Alisema kuwa tayari ameshakwenda nchi
mbali mbali kwa lengo la kulifanyia kazi suala hilo 2012 mwezi wa Agosti Ras-
El Haiman, Uholanzi Kampuni ya Shell na kuja zaidi ya nchi nane nazo zimekuja
kuomba mashirikiano hayo.
"Tutayachimba wenyewe kwa sheria
zetu... si vizuri kujitokeza mtu mmoja kwa lengo la kutaka asifiwe kwani
iliofanya ni Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar",alisema Dk. Shein.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment