Habari za Punde

Dk Shein awatunuku vyeti wahitimu wa Chuo kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA)


 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                  19.12.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amekitaka Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kuendelea kufanya tafiti kwa kuzingatia mahitaji yaliyopo na kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti hizo yanasambazwa kwa taasisi na sekta zinazohusika na yanatumika ipasavyo katika mipango ya maendeleo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), kiliopo Tunguu, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja katika Mahafali ya Kumi na Moja ya Chuo hicho baada ya kuwatunuku vyeti wahitimu 699 katika fani 15 wakiwemo 7 wa Shahada ya Uzamili ya Sayasi katika Kemia.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa ameridhishwa sana na dhamira na juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na SUZA hivi sasa za kuimarisha shughuli za utafiti na ubunifu kwani amekuwa akihimiza ufanyaji wa utafiti kila mahali na ndio maana akaanzisha Idara za utafiti kwa kila Wizara za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Dk. Shein alisema kuwa kwa kufanya hivyo itakuwa ni rahisi kutimiza dhamira ya chuo hicho ya kukifanya kuwa kinaongoza katika Ukanda wa Afrika Mashariki kwa utoaji wa taaluma bora, ufanyaji wa tafiti na kukuza ubunifu katika fani mbali mbali.


“Matunda ya jitihada zenu tayari yanaonekana tukijua kwamba wakati vyuo vyengine vinakosa waombaji wa kujiunga na masomo, SUZA imepata zaidi idadi inayohitajika tena wakiwa na sifa nzuri zaidi ya viwango vilivyowekwa”,a lsiema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alikitaka chuo hicho kuendeleza utamaduni wa kuzishirikisha taasisi za Serikali katika mafunzo mbali mbali yanayotolewa Chuoni kupitia miradi iliyopo kila inapotokezea fursa za aina hiyo kwani utamaduni huo utasaidia sana juhudi za Serikali za kuwajengea uwezo watumishi wa Umma.

Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa SUZA pamoja na wahitimu kwa ongezeko la wahitimu wa fani nyengine tatu mpya ambazo ni Stashahada ya Usimamizi wa Urithi wa Kale na Utalii, Stashahada ya Ukutubi na Shahada za Uzamili ya Kemia.

Alisema kuwa kupata wahitimu katika kiwango cha Shahada ya Uzamili, katika masomo ya Sayansi kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar ni tukio kubwa na la kutia moyo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa sekta ya utalii hivi sasa ndiyo sekta kiongozi kwa uchumi wa Zanzibar hivyo matumaini yake ni kuwa wahitimu wa fani ya Usimamizi wa Urithi wa Kale na Utalii watakuwa ni chachu ya mabadiliko na watasaidia kukabiliana na vyema na changamoto za usimamizi wa maeneo ya urithi wa kale.

Aidha, wahitimu wa diploma ya ukutubi watasidia kwa kiasi kikubwa kufikia azma ya Serikali ya kuanzisha maktaba katika skuli zote za Sekondari na msingi na kutoa wito kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kufanya jitihada za kuwaajiri na kuwaenzi vijana hao pale hali itakaporuhusu ili waweze kutoa mchango wao katika fani hiyo.

Dk. Shein alisema kuwa amevutiwa na taarifa za maandalizi ya kuanzisha masomo ya fani mbali mbali katyika ngazi ya Uzamili kama vile Usimamizi wa Mali Asili na Tabianchi pamoja na ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni.

Alisema kuwa ni wazi kwamba licha ya mafanikio hayo yaliopatikana hadi sasa, uongozi wa chuo unahitaji kuendelea kuongeza kasi kwa kufanya kazi kwa umakini na ubunifu wa hali ya juu, kwani Serikali na wananchi wanategemea maendeleo makubwa zaidi katika Chuo hicho.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alsiema kuwa Wizara Ya Elimu pamoja na Uongozi wa Chuo wamefikia hatua nzuri ya kulifanyia kazi agizo la Serikali la kuziunganisha na SUZA taasisi tatu za elimu ya juu ikiwemo Chuo cha Taalamu za Sayansi za Afya kiliopo Mbweni, Chuo cha Uongozi wa Fedha na Chuo vcha Utalii Maruhubi.

Katika hotuba yake hiyo pia, Dk. Shein alieleza kufurahishwa kwake na juhudi za SUZA za kuimarisha fursa za elimu kwa wanawake kwani katika mahafali hiyo sehemu kubwa ya wahitimu ni wanawake ambao ni sawa na asilimia 64.2 ambapo pia mwanafunzi wa kike kwa mara nyengine tena ndie aliyefanya vizuri katika masomo ya sayansi.

Dk. Shein pia, aliueleza uongozi wa SUZA kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi zao ili malengo ya kuanzishwa kwa Kampasi ya Benjamin William Mkapa iliyopo Mchanga Mdogo Pemba, yaweze kufikiwa  huku akiwataka wananchi wa Pemba waitumie fursa hiyo huku Serikali ikiwa na nia ya kuanzisha Chuo Kikuu kisiwani humo.

Katika nasaha zake kwa wahitimu hao, Dk. Shein aliwataka kila mmoja kuhakikisha anajiwekea malengo ambayo yatakuwa na tija kwake mwenyewe, familia, jamii na nchi kwa jumla sambamba na kupanga mikakati ya kuyafikia malengo hayo.

Pia, aliwataka wahitimu kuendelea kuwa waadilifu na wazalendo kwa nchi yao na kuwahimiza hasa kwa wale wote walioomba mikopo Serikalini na wakakopeshwa, kufanya juhudi za kurejesha mikopo hiyo kwa mujibu wa sheria na makubaliano yaliopo ili fedha hizo ziweze kuwasaidia wanafunzi wengine wanaotaka kujiendeleza.

Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuiagiza Wizara ya Fedha, Wizara ya Elimu pamoja na Tume ya Mipango kukaa pamoja na kuhakikisha katika mahafali kama hiyo hapo mwakani  inafanyika katika ukumbi maalum badala ya maeneo yanayofanyika hivi sasa.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Mhe. Ali Juma Shahuna alieleza juhudi zinazofanywa na Serikali kupitia Wizara yake katika kutoa mashirikiano na chuo hicho na kumpongeza Dk. Shein kwa uongozi wake na juhdui zake za kukisimamjia na kukionoza chuo hicho akiwa Mkuu wa Chuo hicho.

Nae Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Idrisa Ahmada Rai, alimueleza Dk. Shein mikakati iliyowekwa na chuo hicho sambamba na mafanikio yaliopatikana  ikiwa ni pamoja na kuanzisha televisheni ya chuo hico (SUZA TV) itakayotumika kutoa taaluma ya masomo ya sayansi kwa skuli za Sekondari za Zanzibar sambamba na kuitumia TEHAMA kwa kufundishia.

Pamoja na hayo, alieleza azma ya ujenzi wa daghalia kwa mashirikiano ya ZSSFna PBZ pamoja na majengo mengine ya chuo hicho. Aidha, alieleza mafanikio ya wanawake chuoni hapo na kupongeza kwa jinsi wanavyofanya vizuri katika masomo yao.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.