Habari za Punde

Dk Ali Mohamed Shein, Atowa Risala ya Kuukaribisha Mwaka Mpya wa 2016.

RISALA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA  LA MAPINDUZI, MHESHIMIWA DK. ALI MOHAMED SHEIN
YA KUUKARIBISHA  MWAKA MPYA WA 2016.

NduguWananchi,
Assalam  Aleikum,
Kwa hakika tuna wajibu wa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mtukufu, Muweza wa Kila Kitu kwa kutupa uhai tukaweza kufika hadi siku hii ya leo tunapouaga mwaka  2015 na kuukaribisha  mwaka mpya wa 2016.  Hii ni neema kubwa aliyoturuzuku Mola wetu, Subhana Wataala kwani katika kipindi kama hiki mwaka jana, tulikuwa na wenzetu ambao kwa hivi sasa wamekwishatangulia mbele ya haki. Tumuombe Mwenyezi Mungu awasamehe makosa yao na awape malazi mema.  Na sisi tulio hai atujaalie khatma njema.

Wakati mwaka 2015 unamalizika ni vyema japo kwa muhtasari tukatafakari baadhi ya masuala muhimu tuliyokabiliana nayo katika mwaka huo.  Hatua hiyo, itatuwezesha kufanya tathmini ya mafanikio na changamoto tulizokumbana nazo ili tuweze kujipanga na kuweka dhamira ya kuzifanyia kazi kwa lengo la kupiga hatua zaidi za maendeleo kwa mwaka ujao.

Ndugu Wananchi,
Katika mwaka wa 2015, nchi yetu ilikuwa na hali ya amani na utulivu jambo ambalo tunapaswa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa neema hiyo ambayo imetuwezesha kutekeleza kwa mafanikio mipango yetu ya maendeleo ikiwemo Dira ya Maendeleo ya  Mwaka 2020, MKUZA II, Malengo ya Milenia na Ilani ya Uchaguzi Mkuu  ya CCM ya mwaka 2010 – 2015 ambayo tuliweza kuitekeleza kwa asililmia 90.  Kuwepo kwa amani kumetuwezesha wananchi kuendelea na shughuli zetu za kila siku kwa utulivu.  Kutokana na amani na utulivu uliopo wageni wengi  wameendelea kuitembelea nchi yetu.  Jumla ya watalii 254,699  waliitembelea Zanzibar katika kipindi cha Januari-Novemba, 2015 na kupelekea sekta hii kuimarika kwa kiasi kikubwa.

Kufuatana na takwimu za robo mbili za mwanzo wa mwaka 2015, uchumi wetu umeendelea kuimarika.  Sura halisi itafahamika baada ya kumalizika kabisa kwa mwaka huu na tathmini kamili ya hali ya uchumi kufanywa.  Kwa upande mwengine, huduma za jamii zikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama, huduma za afya pamoja na elimu zimeimarika.

Ndugu Wananchi,  
Katika mwaka huu, tumepiga hatua kubwa katika kuimarisha miundombinu. Tumeweza kumaliza ujenzi wa barabara muhimu na kuzizindua Unguja na Pemba, ikiwemo barabara ya Wete Gando na Wete Konde. Tumeimarisha bandari zetu pamoja na viwanja vya ndege. Sote ni mashahidi wa kazi kubwa tuliyoifanya katika kukiimarisha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume pamoja na Kiwanja cha ndege cha Pemba ambacho tayari tumekitia taa za kurukia ndege. Katika mwaka 2015, tulikamilisha na kuzindua mradi wa ujenzi wa maegesho ya ndege (Apron) na njia za kupitia ndege (taxiway) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume.  Kadhalika, tumeendeleza ujenzi wa jingo la abiria litalokuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni 1.6 kwa mwaka.

Hatua tuliyofikia katika ujenzi wa viwanja hivi tayari imepelekea kuwepo kwa ongezeko kubwa la idadi ya ndege za Kimataifa zinazokuja Zanzibar, jambo ambalo limepelekea kuimarika kwa sekta ya utalii na shughuli za biashara.

Ndugu Wananchi,  
Miongoni mwa masuala muhimu ya maendeleo ambayo nchi yetu imeyapata katika mwaka uliomalizika ni kufanikiwa kwa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, la kuwapatia meli mpya wananchi wa Zanzibar.  Serikali iliweka dhamira ya dhati ya kupambana na tatizo la uhaba wa vyombo vya kuaminika vinavyofanya safari zake kati ya Unguja, Pemba na Dar es Salaam.  Tulifanikiwa kuitengenezesha meli mpya, yenye mitambo ya kisasa katika Kampuni ya “Daewoo International” ya Jamhuri ya Korea ambayo ina utaalamu na uzoefu mkubwa wa kutengeneza meli.

Tayari meli hiyo tuliyoipa jina la MV Mapinduzi II, iliwasili nchini tarehe 2 Disemba, 2015.  Nasaha zangu kwenu nyote wananchi ni kuwa, tuithamini na kuienzi meli yetu hiyo.  Tukumbuke msemo wa Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, kuwa “kithamini kilicho chako mpaka usahau cha mwenzako” .

Katika mwaka 2015, tumefanya juhudi kubwa katika kuhakikisha kuwa dhamira yetu ya kujenga bandari ya Mpiga Duri tunaanza kuitekeleza.  Juhudi kubwa zimefanywa katika kutafuta fedha za mradi huu.  Hivi sasa Serikali inakamilisha mazungumzo ya kupata fedha kwa njia ya mkopo kutoka “Exim Bank” China.  Kwa kuanzia ujenzi wa bandari hii, utachukua eneo la mita 300 kutoka Kusini kwenda Kaskazini na utajumuisha ufukiaji wa bahari, eneo lenye urefu upatao mita 490.  Ujenzi wa bandari hii utategemea kuanza wakati wowote katika mwaka 2016.  Ujenzi huo utakapomalizika utapunguza msongamano uliopo katika bandari ya Malindi na utaimarisha kwa kiasi kikubwa ukuaji wa biashara hapa Zanzibar.  Kadhalika, gati hiyo itatoa ajira kwa wananchi na kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wetu.

Vile vile,  katika mwaka huu unaomalizika tumepata mafanikio katika juhudi zetu za kusambaza huduma za umeme  vijijini. Vijiji mbali mbali kama vile Kijini na Mbuyu Tende katika Mkoa wa Kaskazini Unguja vimepatiwa huduma hizo. Aidha, kwa kuwatumia wataalamu wazalendo tumeweza kuufikisha umeme huko Kisiwa Panza na Kisiwa cha Makoongwe kwa upande wa Pemba.

Kadhalika, katika mwaka 2015, tumetekeleza kwa mafanikio miradi ya maji safi na salama katika maeneo mbali mbali, Unguja na Pemba.  Tumeshuhudia ongezeko la uchimbaji wa visima katika maeneo kadhaa. Vile vile, tunatarajia kulipatia ufumbuzi, tatizo la maji safi na salama katika Manispaa ya mji wa Zanzibar kufuatia kutiwa saini Mkataba wa Mradi wa Maji Mjini tarehe 29 Disemba, 2015.

Mradi huo utagharimu jumla ya Dola za Marekani 21,000  zikiwa ni mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itachangia asilimia 10.  Kampuni zinazohusika ni NSPT LTD na SPENCON SERVICES LTD zilizosajiliwa nchini Tanzania.  Maeneo yatakayofaidika ni Mji Mkongwe na maeneo yanayopakana na mji huo.

Tumeanza kuifanyia kazi changamoto ya ukosefu wa huduma za umeme katika sehemu tulizochimba visima, jambo ambalo kwa kiasi kikubwa  huathiri juhudi zetu za kuwafikishia wananchi huduma hizi muhimu. Matumaini yangu ni kuwa ifikapo mwishoni mwa  mwaka 2016 changamoto hii itakuwa imeshapatiwa ufumbuzi na kukidhi matarajio ya wananchi.

Ndugu Wananchi,
Kwa upande wa huduma za afya, katika mwaka 2015 tumeziimarisha huduma hizo kwa  kuongeza kasi ya kusomesha wataalamu, upatikanaji dawa na huduma mbali mbali pamoja  na kuziimarisha hospitali zetu kwa kutekeleza miradi mbali mbali ya ujenzi.   Katika mwaka wa 2015, tulianza kuijenga upya hosptali ya Abdalla Mzee Pemba kwa msaada wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.  Ujenzi huo utakamilika mwaka 2016.  Hivi sasa tunaendelea na uimarishaji wa Hosptali ya Mnazi Mmoja kwa kujenga majengo mapya na kuongeza kasi ya utoaji wa huduma mpya  ili tufikie azma yetu ya kuifanya hosptiali hii kuwa ya rufaa.  Katika kipindi hiki tumeziondoa gharama za kuchangia  huduma za uchunguzi wa maradhi kwa kutumia “X-Ray”, “CT-Scan” na “Ultra Sound” na sasa zinatolewa bila ya malipo kwa wananchi wote.  Katika mwaka ujao wa 2016 juhudi zitafanywa za kuondoa kuchangia huduma za uchunguzi wa maabara, ili nazo ziwe bila ya malipo.

Katika mwaka 2015 tumepata mafanikio makubwa kwa upande wa elimu. Tumemaliza na kuanza upya miradi ya ujenzi wa skuli mbali mbali na kuongeza fani za mafunzo katika vyuo vikuu na  taasisi za elimu ya juu. Vile vile, tumeanza kutekeleza lengo letu la  kuondoa utaratibu kwa wazazi kuchangia gharama za elimu maskulini kama nilivyotangaza tarehe 12 Januari, 2015.  Lengo letu ni kuifanya elimu ya msingi kuwa bure huku tukiandaa utaratibu ili elimu ya sekondari nayo iwe bure kama ilivyodhamiriwa na Muasisi wa Mapinduzi yetu ya 1964.

Katika mwaka 2015, tulifikia uamuzi ya kuwapatia pensheni ya kila mwezi wazee wetu wote waliofikia umri wa miaka 70 bila ya kujali kama waliwahi kuajiriwa Serikalini au hawakuajiriwa.  Hatua hiyo itaanza kutekelezwa kuanzia mwezi April mwaka 2016.  Ni wajibu wetu kuwatunza wazee wetu ambao wamefanya kazi kubwa ya kuijenga nchi yetu katika ujana wao.
Ndugu Wananchi,
Katika mwaka 2015 tulipanga na kuanza kutekeleza kwa kasi, mipango ya ujenzi wa miji na majengo ya kisasa katika sehemu mbali mbali ili kuweza kujenga taswira  mpya ya Zanzibar katika kipindi kifupi kijacho.
Serikali kupitia ZIPA ilipanga kutekeleza miradi mitano ambayo baadhi yake tayari imeshapata wawekezaji na kuanza kutekelezwa katika eneo la Fumba.  Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa miji ya kisasa ya makaazi, uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo, ujenzi wa kituo cha kimataifa cha mikutano na maonyesho ya biashara.  Serikali, kwa kushirikiana na Kampuni za “Union Property Developer” na “Coastal Dredging” inaendelea na ujenzi wa barabara katika maeneo yaliyopangwa kuendelezwa kwa kujengwa mji mpya wa kisasa huko Fumba.  Kwa sasa barabara kuu zenye urefu wa kilomita 13 zimo katika hatua mbali mbali za ujenzi.   Jumla ya nyumba 1,300 zinatarajiwa kujengwa kwa ajili ya kuuzwa kwa wazalendo katika kipindi cha mwaka mmoja ambapo kwa kuanzia, nyumba 150 zitaanza kujengwa mwezi wa Februari, 2016.

Kwa upande wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mradi wa ujenzi wa mji wa kisasa wa kibiashara pamoja na hoteli kubwa ya nyota tano, utakaojengwa huko Ma        temwe umeanza kutekelezwa na unatarajia kuwekeza jumla ya Dola za Marekani milioni 800.  Kampuni ya “Pennyroyal ya Gibralter” ndiyo inayotekeleza mradi huo.

Kwa upande mwengine katika mwezi wa Novemba 2015, Serikali ilitiliana saini Mkataba na Kampuni ya “Quality Group Limited” ambayo itaanzisha mradi mkubwa wa kuendeleza Hoteli ya Bwawani na maeneo yanayoizunguuka.  Mradi huo utawekeza mtaji wa Dola za Marekani kiasi cha Milioni 200 na utahusisha kulifanyia ukarabati mkubwa jengo la Hoteli ya Bwawani na kuliwezesha kutoa huduma za hoteli ya nyota tano. Jengo hili  la hoteli litaimarishwa ili kuhifadhi kielelezo cha mafanikio cha Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya 1964.

Kadhalika, Serikali imeidhinisha mradi wa upanuzi wa Hoteli ya Mtoni Marine, unaohusisha utengenezaji wa ufukwe kwa ajili ya mapumziko ya wageni na wenyeji.  Upanuzi huo, vile vile, unahusisha uanzishwaji wa mji mdogo wa kisiwa kwa ajili ya watu wenye uwezo wa kifedha na hivyo kupelekea Serikali kukusanya mapato yatayotokana na umiliki wa majengo katika mji huo. Mwaka 2015, ulibeba shughuli nyingi za uanzishwaji wa ujenzi wa miji mipya.

Sambamba na juhudi hizo zinazochukuliwa na ZIPA za kushajihisha wawekezaji katika ujenzi wa miji ya kisasa, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) nao unaendelea na juhudi za kubadillisha taswira ya Zanzibar kwa kuwekeza katika ujenzi wa majengo ya kisasa katika eneo la Mbweni. Mradi huu umejumuisha  ujenzi wa jumla  ya majengo 18 ya ghorofa 7 kila moja, yatakayokuwa na nyumba 252.  Ujenzi wa majengo hayo umeshaanza.  Wakati tunamaliza mwaka huu 2015, tunapaswa kujipongeza kwa kufanikisha ujenzi wa Viwanja vya Watoto, Kiwanja cha Kariakoo kwa Unguja na Tibirinzi kwa upande wa Pemba. Kukamilika kwa ujenzi wa Mnara wa Kumbukumbu ya Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika eneo la Michenzani, kumeiletea haiba mpya mji wetu wa Zanzibar na umekuwa ni kielelezo kizuri cha kumbukumbu ya Mapinduzi yetu ya 1964.

Ndugu Wananchi,
Ili mafanikio haya tuliyoyapata yawe endelevu, napenda nikumbushe  kuhusu umuhimu wa kuitunza miundombinu yetu yote ya maendeleo ambapo fedha nyingi zinatumika katika kuitengeneza kwa ajili ya maendeleo yetu.  Inasikitisha kuona kwamba katika mwaka uliomalizika, baadhi ya watu waliendeleza vitendo vya kuharibu miundombinu katika maeneo mbali mbali kwa kuweka mbele maslahi yao binafsi na kusahau wajibu wa kutanguliza maslahi yetu sote.

Katika baadhi ya maeneo ya nchi yetu, watu hao walikata nyaya za umeme na kusababisha hasara kwa shirika la umeme (ZECO) na usumbufu kwa wananchi kwa kukosa huduma hiyo.  Aidha, katika maeneo  mengine vitendo vyao vimesababisha kukosekana kwa huduma za maji safi na salama.  Natao wito kwa wananchi wote ili tuwe walinzi wa miundombinu yetu na tusichelee kuwafichua wale wote wanayoiharibu.

Ndugu Wananchi, 
Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa neema ya mvua ambayo imetuwezesha kupata  mazao ya chakula na biashara hasa zao la karafuu katika mwaka uliomalizika.  Kwa mara nyengine tena napenda niwashukuru wakulima wetu kwa jitihada zao katika kilimo,  hali ambayo imesaidia sana kuwapo kwa uhakika wa mazao ya chakula zikiwemo ndizi, muhogo, viazi, matunda na aina za mboga. Kadhalika, natoa shukurani kwa wakulima wa mpunga wa kutegemea mvua kwa jitihada zao, ingawa kwa bahati mbaya hali ya mavuno kwa mwaka uliomalizika haikuwa nzuri sana.

Tayari maandalizi ya kilimo cha mpunga wa kutegemea mvua kwa mwaka huu yamekwishaanza katika mabonde mbali  mbali ya Unguja na Pemba kwa hatua ya kuchimbua mashamba.  Serikali inaendelea kutoa ruzuku kwa huduma za matrekta na pembejeo za kilimo kwa wakulima ambapo kwa  msimu wa mwaka 2015/2016, tani 750 za mbolea na lita 15,000 za dawa ya kuulia magugu zimekwishanunuliwa.

Natoa wito kwa wakulima wetu kuzitumia fursa zilizowekwa na Serikali ili kuongeza tija katika kilimo chetu. Kadhalika, nawasihi wafuate maelekezo ya maafisa ugani ya kuzingatia misingi ya kilimo bora kwa kutayarisha mashamba kwa wakati, kutumia mbegu bora, mbolea na dawa za kuulia wadudu ili tupate mazao mengi yatakayotuwezesha tupunguze uagiziaji wa mchele hatua kwa hatua kutoka nje ya nchi.

Ndugu wananchi,
Kuhusu zao la karafuu, napenda nitoe pongezi kwa wakulima wa karafuu kwa jitihada zao na kushirikiana na Serikali katika kuliendeleza zao  hilo.  Wakulima wetu wameitikia vyema wito wa Serikali wa kuuza karafuu zao katika vituo vya ZSTC ambapo katika msimu wa ununuzi wa karafuu 2015/2016, hadi kufikia mwezi Novemba, 2015 jumla ya tani 962.7 za karafuu zenye thamani ya TShs. Bilioni 13.471 zimenunuliwa katika vituo vya ununuzi wa karafuu vya ZSTC  Unguja na Pemba. Kwa mara nyengine nalipongeza Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC) kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kuliendeleza zao la karafuu pamoja na vikosi vyetu vya ulinzi na wananchi wote kwa kupambana na magendo ya karafuu. Kwa lengo la kuzidi kuliimarisha zao la karafuu na kuendeleza zaidi zao hili. Mnamo mwezi wa August, 2015 tulizindua Mfuko wa  Maendeleo ya Karafuu Zanzibar kwa lengo la kuliendeleza zaidi zao hili.   Kupitia mfuko huu, tuna matumaini ya kuongeza ufanisi katika kulishughulikia zao la karafuu ili kuongeza tija.

Ndugu Wananchi, 
Mwaka 2015 ulikuwa ni mwaka wa Uchaguzi Mkuu ambapo tarehe 25 Oktoba, wananchi wa Zanzibar walishiriki katika kuwachagua Viongozi kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Uchaguzi Mkuu ulitanguliwa na kampeni za vyama vilivyoshiriki uchaguzi huo na wananchi walishiriki kwa wingi katika kampeni zake. 

Uchaguzi wa Viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliosimamiwa na Tume ya Uchaguzi ya Taifa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umemalizika na Chama cha Mapinduzi kimepata ushindi mkubwa.  Nampongeza Mheshimiwa Dk. John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Makamu wa Rais.  Kwa upande wa Zanzibar Tume ya Uchaguzi uliufuta uchaguzi huu hapo tarehe 28 Oktoba, 2015, baada ya kubainika kutokea kwa kasoro kadhaa kama zilivyoelezwa na Tume hiyo.  Aidha, uamuzi huo wa Tume ulitangazwa katika Gazeti Rasmi la Serikali la tarehe 6 Novemba, 2015 kwamba Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imeyafuta matokeo yote ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa tarehe 25 Oktoba, 2015 na kwamba uamuzi wa Tume wa tarehe nyengine ya kurudiwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar utatangazwa baadae.

Aidha, katika suala zima la hali ya kisiasa ya Zanzibar, iliyojitokeza baada ya kufutwa kwa Uchaguzi Mkuu, viongozi wenu tulishauriana tukutane ili tufanye mazungumzo ya kutafuta suluhu kwa njia ya amani, ili nchi yetu iendelee kuwa na amani, umoja na mshikamano. Hatimaye tulikubaliana tuanze mazungumzo hayo. Mazungumzo haya yanatuhusisha viongozi sita.  Viongozi hao ni mimi nikiwa Mwenyekiti, Makamu wa Kwanza wa Rais, Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad na Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wakiwa wajumbe.  Wajumbe wengine ni Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu wa Zanzibar wa Awamu ya Tano Dk. Salmin Amour Juma na Rais Mstaafu wa Zanzibar wa Awamu ya Sita Dk. Amani Abeid Karume.  Mazungumzo hayo yamefikia hatua kubwa na bado yanaendelea. Taarifa kamili ya mazungumzo hayo itatolewa mara tu yatakapokamilika.

Ndugu Wananchi,  
Kama inavyofahamika kuwa kila  mwaka inapofika mwezi wa Januari, huwa tuna maadhimisho ya sherehe za Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari, 12 mwaka 1964.  Katika mwezi wa Januari wa mwaka 2015, tuliadhimisha sherehe za miaka 51 ya Mapinduzi kwa matukio mbali mbali yaliyojumuisha uzinduzi na uwekaji wa mawe ya msingi wa miradi ya maendeleo kwa Unguja na Pemba.  Wengi wetu, tulishiriki katika maadhimisho ya siku ya kilele, tarehe 12 Januari, 2015 kwenye Uwanja wa Amaan na sherehe hizo zilifana sana.

Tarehe 12 Januari, 2016, panapo majaaliwa tutaadhimisha miaka 52 ya Mapinduzi, ambapo kama kawaida, sherehe hizo zitatanguliwa na matukio mbali mbali ya shughuli za uzinduzi wa miradi ya maendeleo na uwekaji wa mawe ya msingi.  Wito wangu kwa wananchi wote ni kujitokeza kwa wingi katika matukio mbali mbali yaliyopangwa katika maadhimisho hayo. Tukumbuke kuwa Mapinduzi yetu ni kielelezo muhimu cha ukombozi wa nchi yetu na uzalendo.  Aidha, kushiriki kwetu kwenye sherehe ya maadhimisho haya ni hatua ya kuyaendeleza malengo ya Mapinduzi kwa shabaha ile ile waliokuwa nayo waasisi wetu.

Ndugu Wananchi,  
Wakati tunapoukaribisha mwaka mpya na tukiwa katika maandalizi ya sherehe za miaka 52 ya Mapinduzi, napenda nisisitize umuhimu wa kuendeleza usafi wa mazingira katika maeneo tunayoishi. Mazingira yaliyo machafu ni chanzo kikubwa cha maradhi mbali mbali ya miripuko ikiwa ni pamoja na maradhi ya kipindupindu. Taarifa kutoka Wizara ya Afya zinaeleza kuendelea kuwepo kwa maradhi ya kipindupindu katika baadhi ya maeneo nchini na hali bado si ya kuridhisha sana.  Hata hivyo, Serikali inachukua hatua za kukabiliana na maradhi hayo kwa kuendeleza kambi za matibabu na kutoa elimu ya afya juu ya namna ya kujikinga nayo.

Natoa wito kwa wananchi nyote mzingatie kanuni za afya ikiwa ni pamoja na kuimarisha usafi, kutotupa taka ovyo, kuepuka kuweka bidhaa chini hasa katika kipindi cha  mvua na kuhifadhi vyakula hasa vinavyouzwa barabarani.  Aidha, Baraza la Manispaa, Mabaraza ya miji kwa Pemba na Halmashauri zote za wilaya zichukue hatua ya kusimamia uzoaji wa taka na kuzipeleka katika maeneo yaliyotengwa pamoja na kuishughulikia misingi ya  maji machafu kama hatua ya dharura ya kukabiliana na  maradhi ya mripuko.  Sote tushiriki katika kuisafisha Miji yetu na maeneo tunayoishi hapo tarehe 3 Januari, 2016, kama ilivyopangwa katika ratiba ya Maadhimisho ya Sherehe za Mapinduzi kwa mwaka huu.

Ndugu Wananchi,  
Namaliza risala yangu, kwa kukukumbusheni kwamba kesho tarehe 1 Januari ni siku yetu ya kujitokeza sote kufanya mazoezi.  Tujitokezeni kwa wingi.  Nakutakieni kheri ya mwaka mpya viongozi wote, wananchi, nchi marafiki, washirika wetu wa maendeleo pamoja na mashirika ya Kimataifa kupitia mabalozi na wawakilishi waliopo nchini. Namuomba Mwenyezi Mungu atujaalie kheri, baraka na neema nyingi katika mwaka mpya wa 2016.  Atuzidishie amani, umoja na masikilizano. Atujaalie uwezo zaidi wa kuitekeleza mipango yetu kwa ufanisi ili kuimarisha uchumi na ustawi wa maendeleo ya nchi yetu.


Ahsanteni kwa kunisikiliza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.