Habari za Punde

Balozi Seif Azungumza na Watendaji wa SMZ Dar es Salaam, na Kumtembelea Kanali Fara Hospitali.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na watendaji wa Ofisi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar waliopo Mtaa wa Magogoni Mjini Dar es salaam ambapo Ofisi hiyo kwa sasa iko chini ya uratibu wa Ofisi yake.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akimjuilia hali Mbunge Mstaafu wa lililokuwa Jimbo la Rahaleo Wilaya ya Mjini Kanal Mstaa Saleh Ali Fara aliyelazwa Hospitali ya Jeshi Lugalo Jijini Dar es saam akipatiwa huduma za matibabu akizumbuliwa na maradhi ya Mgongo.

Balozi Seif akibadilishana mawazo na Madaktari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania { JWTZ } Lugalo Hospitali Mjini Dar es salaa baada ya kumjulia hali Mbunge mstaafu wa Mlandege Kanal Mstaafu Saleh Ali Fara.

Picha na- OMPR – ZNZ.


Na. Othman Khamis OMPR. 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na mipango ya kuijengea utaratibu madhubuti Ofisi yake iliyopo Mjini Dar es salaam ili iweze kuratibu shughuli zake kwa ufanisi mkubwa zaidi.


Balozi Seif alisema hayo wakati akizungumza na watendaji wa Ofisi ya SMZ iliyopo Mtaa wa Magogoni Jijini Dar es salaam baada ya kupokea changamoto zinazowakabili sambamba na kuangalia muelekeo mzuri utakachangia majukumu ya Ofisi hiyo kutekelezwa katika njia ya kitaalamu.

Alisema Mipango hiyo itawawezesha watendaji wa Ofisi hiyo kuwapa fursa ya kubuni njia sahihi zitakazoiwezesha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutanua mafungamano yake zaidi na Taasizi za Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na zile za Kimataifa.

Balozi Seif alieleza kwamba malengo ya kuanzishwa kwa Ofisi ya SMZ Dar es salaam ilikuwa ni kuratibu masuala ya uchumi na fedha kati yake na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika dhana nzima ya kudumisha Muungano wa Tanzania.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwashauri watendaji hao kuzingatia  mfumo wa utaratibu watakaopewa  na Serikali baada ya kukamilika kwake na kutumia utaalamu sambamba na bidii zao ili lile lengo lililokusudiwa la kuundwa kwa Ofisi hiyo likamilike vizuri.

“Tunachokitarajia kutoka kwenu ni kuona taaluma zenu zinaleta mafanikio katika Nyanja zote za maendeleo iwe, Kilimo, uchumi,Utamduni  na hata ustawi wa wananchi ”. Alisema Balozi Seif.

Akigusia hali ya Visiwani Zanzibar Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwaomba watendaji hao wa SMZ Dar es salaam kuendelea majukumu yao ya ujenzi wa Taifa bila ya hofu yoyote.

Alisema hali ya utulivu, amani na mshikano ndani ya Visiwa vya Unguja na Pemba hivi sasa  inaendelea kama kawaida na kuwaomba waondoe shaka kutokana na baadhi ya taarifa zinazosambazwa na baadhi ya vyombo vya Habari na mitandao ya Kijamii vikidai kwamba hali ya kisiasa Zanzibar
wakati huu imekuwa tete.

“ Unashangaa kusikia au kuona kwenye baadhi ya  vyombo vya habari vikiandika na kutangaza kwamba hali ya Zanzibar ni tete wakati wananchi wanaendelea na harakati zao za kimaisha bila ya bughdha. Sasa hii hali tete inatoka wapi? ”. Aliuliza Balozi Seif.

Alisema harakati za kimaisha hasa wananchi kuendelea na shughuli zao za kawaida zinakwenda na ushahidi wa hao ni mmiminiko wa watalii na wageni wanaoingia Zanzibar kila kukicha.

Balozi Seif  aliwahakikishia wananchi kwamba hali ya amani itaendelea kuimarishwa na Taasisi za ulinzi kabla na wakati wa marejeo ya uchaguzi Mkuu wa Zanzibar unaotarajiwa kufanyika Tarehe 20 mwezi huu.

1 comment:

  1. dah! sasa imekuwa mpaka mikutano ya SMZ ikafanyike bara?

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.