Na Salum Vuai,
MAELEZO
WAZIRI wa Ofisi ya Makamu
wa Rais anayeshughulikia mambo ya muungano Januari Makamba, ameyachangia
mabaraza ya vijana Unguja Ukuu shilingi milioni tatu na kuyataka yaelewe kuwa
mustakbali wa taifa la Tanzania umo mikononi mwao.
Makamba, alikuwa
akizungumza na vijana wa shehia tatu za kijiji cha Unguja Ukuu wakati wa
uzinduzi wa mabaraza ya vijana wa shehia hizo uliofanyika juzi katika uwanja wa
mpira wa Tindini katika jimbo la Tunguu Wilaya ya Kati.
Mabaraza
yaliyozinduliwa ni yale ya shehia za Kaepwani, Tindini na Kaebona.
Hata hivyo, Waziri
huyo aliyepangwa kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo, aliwahutubia vijana hao
kwa kuunganishwa na teknolojia ya mtandao akiwa mjini Dodoma ambako ametingwa
na vikao vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Makamba aliwataka
vijana hao kutojiingiza katika siasa chafu zinazoweza kuwafarakanisha na
kurudisha nyuma jitihada zao na za serikali katika kuleta maendeleo nchini.
Badala yake,
aliwaeleza kuwa siasa nzuri ni zile zilizojikita katika kuwaunganisha watu,
kuimarisha upendo, na kujenga taifa kwa lengo la kuwakomboa na umasikini.
Waziri huyo pia
aliwashauri vijana kutoendekeza mihemko kwa kujiingiza kwenye vitendo viovu
ikiwemo biashara au matumizi ya dawa za kulevya, uvutaji bangi, uasherati na
uporaji, ambavyo alisema havina hatima njema kwao na kwa taifa.
Alieleza kuvutiwa
kwake na ubunifu wa vijana hao katika kujishughulisha na miradi mbalimbali ya
kuwaendeleza kimaisha na kuahidi kuendelea kuwaunga mkono ili kuhakikisha
wanafikia malengo yao.
Mapema, Mwakilishi
wa jimbo la Tunguu Simai Mohammed Said, na kwa niaba ya mbunge Khalifa Salum
Suleiman, aliwapongeza vijana hao kwa kuitikia wito wa serikali kuunda mabaraza
yao ambayo ndiyo njia inayoweza kuwainua.
Aliwahakikishia
kuwa viongozi wa jimbo wako pamoja nao kwa kuwasafishia njia ya kutimiza
mipango yote ya maendeleo wanayoipanga, huku akiwataka wasiyumbishwe na watu wasiokuwa na nia njema, ambao
wamelenga kuwarejesha nyuma.
Aidha aliyachangia
mabaraza hayo kwa pamoja shilingi laki tano.
Katika risala yao,
vijana wa mabaraza hayo walisema wamejidhatiti kuupiga vita umasikini kwa
kuanzisha miradi mbalimbali ikiwemo ufugaji nyuki, kuku, mbuzi na ng’ombe,
pamoja na kilimo ingawa wanakabiliwa na changamoto kadhaa za uhaba wa vitendea
kazi walizoomba wasaidiwe kuzipatia ufumbuzi.
Hafla ya uzinduzi
huo iliyopambwa kwa burudani za sarakasi, muziki, tenzi, ngongoti na maigizo,
ilihudhuriwa pia na Mkuu wa Wilaya ya Kati Mashavu Sukwa Said, madiwani wa wadi
za jimbo la Tunguu, masheha na wananchi mbalimbali.
No comments:
Post a Comment