Habari za Punde

Wanawake TZ igeni mfano kutoka Kengeja Pemba


Na Salmin Juma - Pemba

Kufuatia hali ngumu za kimaisha na uhaba wa nafasi za kazi serikalini wanawake wa Kengeja wilaya ya Mkoani Mkoa wa kusini Pemba wameamua kujiari wenyewe kupitia sekta ya kilimo na mifugo na hatimae matunda ya ajira hizo wameanza kuyaona.

Hayo yamedhihirika leo baada ya baadhi ya akina mama hao  wanaojishuhulisha na harakati hizo walipozungumza na mwandishi wa habari hizi kijijini kwao juu ya hali halisi ya uwendeshaji shuhuli hizo.

Wamesema kua, kutokana na hali ilivyo sasa wameamua kwa makusudi  kujiingiza katika kilimo na wengine mifugo ili kujikwamua kiuchumi na kupiga hatua mbele kimaendeleo kuanzia wao binafsi na familia zao kwa ujumla.

Mmoja miongoni mwa wakulima kijijini hapo Bi Rabia Hassan Mzee ambae pia ni mwanakikundi cha “WACHEWASEMA” kinachojishulisha na harakati za kilimo amesema kua ingawa katika harakati hizo alikuwemo tokea zamani lakini amezidi kunufaika mara baada ya kujiunga na kikundi hicho ambapo sasa anajivunia kutokana na faida anayoipata.

Amesema kuna utofauti mkubwa alipokua akilima peke yake na alipo jiunga katika kikundi hicho cha ushirika, amesema kufanya kazi kwa pamoja hata manufaa yake yanakua ni mazuri na makubwa kuliko yapeke yako.

Bi Rabia amesema, kutokana na harakati zao hizo sasa ameanza kujipatia fedha ingawa sio kubwa lakini anaendesha maisha yake na kukidhi matumizi mengine madogomadogo.

Mwanakikundi mwengine Bi Amina Juma Omar kutoka kikundi hichohicho  ameipongeza serikali ya SMZ kupitia wizara ya kilimo kwa hatua zao za kuwashajihisha mabwana na mabibi shamba kuwatembelea ili kujua hali halisi ilivyo katika harakati zao hizo.

Amesema ujio wao ni wamunafaa kwani wamepata elimu ya ukulima bora na ufugaji.

Kwa upande wake Bi Riziki Ali Saleh  kutoka katika kikundi cha “MWANZOMGUMU” amesema kua, harakati zake za kilimo sasa zinamuwezesha kujenga nyumba yake binafsi  na kumudu gharama nyengine katika familia jambo ambalo linampa faraja na ari ya kudizisha bidii katika kazi yake.

Pia amewashukuru mabwana shamba wanaofika kijijini kwao ambapo amesema kua,huwapa mbinu mbalimbali za uzalishaji katika kilimo na ufugaji na umuhimu wao wanauona.

Nae Bi Hawa Ali kutoka katika kikundi cha “WACHEWASEMA” amesema ingawa kazi wanayoifanya ni kubwa lakini faida wanaoipata inaridhisha ingawa si kwa kiwango kikubwa, lakini wanaweza kujikimu kimaisha kwa kumsaidia mume katika baadhi ya majukumu na familia kuboreka.

Wakijibu swala la mwandishi wa habari aliyetaka kujua wanajamii kijijini hapo wanawatazama vipi kuhusiana na shuhuli hizo, wamesema kua kunabaadhi yao wanawadhihaki kutokana na kitendo chao cha kujiunga katika vikundi vya ushirika wakiamini kwamba hawana lolote walipatalo ispokua ni kujitesa na kujisumbua.

Wameiomba jamii hasa wanawake wenzao kuondokana na dhana hiyo potofu  na badala yake kwa pmoja waungane katika harakati za kujikomboa kiuchumi na faida itapatikana kama wao wanavyoanza kuiona hvi sasa.

Sheha wa shehia ya Kengeja Bw: Muhammeda Kassim (Africa)   amewapongeza wanawake hao huku akisema kua katika shehia yake wanawake hawako nyuma kimaendeleo hata yeye kupitia serikali wamekua mstari wa mbele kuwasaidia katika shuhuli zao.

Akina mama hao ni wakulima wa mazao tofauti yakiwamo ya Mpungu, Mihogo, Ndizi na karafuu pia ni wafugaji wa kuku na Ng’ombe kijijini hapo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.