HOTUBA YA
RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA
BARAZA LA
MAPINDUZI, MHE. DK. ALI MOHAMED SHEIN,
KATIKA SHEREHE
ZA MAADHIMISHO YA MIAKA 53 YA
MAPINDUZI
YA ZANZIBAR, AMAAN STADIUM
TAREHE 12
JANUARI, 2017
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan;
Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa;
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi;
Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar,
Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi;
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
wa Awamu ya
Pili,
Mheshimiwa
Benjamin Wiliam Mkapa;
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
wa Awamu ya
Tatu,
Mheshimiwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete;
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
wa Awamu ya Nne,
Mheshimiwa Dk. Salmin Amour Juma;
Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi,
Mheshimiwa Dk. Amani Abeid Karume;
Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi,
Waheshimiwa Viongozi Wakuu Wastaafu Mliohudhuria,
Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Mheshimiwa Job Ndugai;
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid;
Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar,
Mheshimiwa Othman Chande Mohamed;
Jaji Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Omar Othman Makungu;
Jaji Mkuu wa Zanzibar,
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya
Kimataifa,
Mheshimiwa Ayoub Mohamed Mahmoud;
Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi,
Waheshimiwa Viongozi mbali mbali wa Serikali na Vyama
vya
Siasa Mliohudhuria,
Ndugu Wananchi,
Mabibi na Mabwana,
Assalaam
Alaikum,
Tuna wajibu
mkubwa wa kutanguliza shukurani zetu kwa Mola wetu; Subhanahu Wataala; Muumba
wa Mbingu na Ardhi kwa kutujaalia neema ya uhai na uzima, tukaweza kuifikia
siku hii ya tarehe 12 Januari, 2017. Tunamshukuru
Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuwa pamoja katika kilele cha Maadhimisho ya miaka 53 ya
Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya tarehe
12 Januari , 1964.
Kwa niaba ya
wananchi wa Zanzibar, natoa shukrani zangu za dhati kwako Mheshimiwa Samia
Suluhu Hassan, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa niaba ya Mheshimiwa Dk. John
Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuungana
nasi katika sherehe zetu adhimu na muhimu.
Vile vile, natoa shukrani kwa viongozi wote wa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, waliopo madarakani
na waliostaafu, Mabalozi wa nchi mbali mbali, Wawakilishi wa Mashirika ya
Kimataifa, Viongozi wa dini na vyama vya siasa na wananchi wote kwa kuhudhuria
kwenu kwenye sherehe hizi.
Mahudhurio yenu makubwa yanatuthibitishia
kuwa Mapinduzi yetu yanaheshimika na yanapewa taadhima kubwa ndani na nje ya nchi
yetu. Nasema ahsanteni sana kwa mahudhurio yenu.
Ndugu
Wananchi,
Leo ni siku muhimu sana katika historia
ya wananchi wa Zanzibar, ambapo miaka 53 iliyopita tuliikata minyororo ya
utawala wa Kisultani na ukoloni wa Kiingereza uliodumu kwa takriban miaka
132. Wananchi walikataa kwa vitendo
kudharauliwa, kunyanyaswa, kubaguliwa na kutokuheshimiwa katika nchi yao. Chama
cha Afro-Shirazi, kiliongoza vuguvugu la kuikomboa Zanzibar, dhidi ya madhila
ya wakoloni, mabwanyenye na mabepari. Wananchi walitendewa madhila,walinyanyaswa
na walinyimwa haki kwenye mambo yote
muhimu katika maisha yao.
Ndugu
Wananchi,
Tunapoadhimisha miaka 53 ya Mapinduzi,
tunawakumbuka na kuwashukuru wazee wetu Waasisi wa Chama cha Afro-Shirazi
walioongozwa na Rais wake wa Kwanza, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume. Daima
hatutowasahau kutokana na ushujaa wao na
ushindi wa jitihada zao za kupigania haki, kuleta usawa na maelewano na
kuondoa pingamizi zote walizokuwa
wakizipata wananchi wa Unguja na Pemba. Ni ukweli ulio wazi kwamba Mapinduzi ndiyo
yaliyowainua wanyonge, yameleta uhuru wa kweli na yamesimamisha utawala wao
katika misingi ya usawa na haki. Ni
kutokana na Mapinduzi, ndipo Wafanyakazi na Wakulima wa Zanzibar walipoirudisha
heshima yao na ubinadamu wao katika nchi yao.
Namuomba Mwenyezi Mungu amrehemu
Jemadari wa Mapinduzi yetu Matukufu ya tarehe 12 Januari, 1964, Marehemu Mzee
Abeid Amani Karume pamoja na waasisi wengine wa Mapinduzi hayo waliotangulia
mbele ya haki na awape afya njema na umri mrefu, wale wote ambao bado wapo hai.
Siku zote tutawakumbuka, tutawaenzi na tutawaombea dua kwa kujitoa muhanga kwa
ajili ya kutukomboa. Hivi sasa, tupo
huru na tunasherehekea miaka 53 ya Mapinduzi yetu tukiwa na mafanikio makubwa. Tunaahidi kuendelea kuyadumisha na
kuyaendeleza malengo ya Mapinduzi yetu Matukufu ya Mwaka 1964.
Ndugu
Wananchi,
Leo tunafikia kilele cha Maadhimisho ya
Sherehe za Miaka 53 ya Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 tukiwa na furaha
kubwa na kusherehekea kwa vifijo na hoi hoi, kama tunavyojionea wenyewe hapa
uwanja wa Amaan.
Katika kipindi hiki cha miaka 53 ya
Mapinduzi, tunasherehekea kuwepo kwa
hali ya amani, umoja, mshikamano na maendeleo makubwa yaliyopatikana. Kwa hivyo, tuna wajibu mkubwa wa kuuenzi na
kuuendeleza umoja na mshikamano wetu ambao ndio siri kubwa ya kuendelea kuwepo
kwa hali ya amani na utulivu yenye kuimarisha maendeleo yetu.
Ndugu
Wananchi,
Nafarijika sana kuona wananchi wa
Zanzibar wameungana na Serikali yao katika kipindi cha miaka 53 kwa
kuyatekeleza malengo ya Mapinduzi yetu na kupatikana mafanikio makubwa ya maendeleo
ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Katika
kipindi chote hicho, Serikali ilipanga mipango yake na iliitekeleza kwa
mafanikio makubwa, bila ya kuingiliwa na nchi ye yote.
Yapo mambo mbali mbali yanayotekelezwa,
ambayo yanaelezea mafanikio yaliyopatikana ikiwemo miradi 51 iliyozinduliwa na
kuwekewa mawe ya msingi katika shamra shamra za maadhimisho haya. Ni haki ya
kila mmoja wetu kujivunia mafanikio hayo na kuyaendeleza kwa manufaa yetu na
wale watakaokuja baadae.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya
Awamu ya Saba, imeingia madarakani katika kipindi cha pili, baada ya Chama cha
Mapinduzi kupata ushindi mkubwa wa asilimia 91.4, wa kura za Rais, ushindi wa majimbo
yote 54 ya Baraza la Wawakilishi na ushindi wa viti vyote vya Madiwani; kwenye
Uchaguzi wa marudio wa tarehe 20 Machi, 2016.
Uchaguzi huo ulirudiwa baada ya ule wa tarehe 25 Oktoba, 2015, kufutwa
pamoja na matokeo yake na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, kwa mujibu wa Katiba ya
Zanzibar ya 1984 na Sheria ya Uchaguzi Namba 11 ya 1984.
Ndugu
Wananchi,
Katika mwaka wa kwanza wa kipindi hiki
cha pili, 2015/2016, cha Awamu ya Saba, Serikali imeanza vizuri utekelezaji wa
Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, MKUZA III na Dira ya Maendeleo
2020 na kupata mafanikio ya kuridhisha katika kuuimarisha uchumi wetu, huduma
za jamii na nyenginezo.
Katika kipindi hiki, pato halisi la Taifa
lilikua kwa kiwango cha wastani wa asilimia 6.6. Kadhalika, pato la mtu binafsi limefikia
wastani wa TZS 1,632,000 sawa na USD 817 kwa mwaka 2015. Katika mwaka 2016, kasi ya mfumko wa bei za bidhaa na huduma ilifikia
asilimia 6.7 ambapo kasi hiyo ilikuwa asilimia 5.7 katika mwaka 2015. Mfumko wa bei bado umedhibitiwa katika
kiwango cha tarakimu moja.
Ndugu Wananchi,
Mafanikio
tunayoyaona, ya kuimarika kwa huduma mbali mbali, yametokana na juhudi za
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya ukusanyaji wa mapato. Kwa kipindi cha Januari hadi Novemba 2016,
mapato yaliyokusanywa kutokana na vyanzo vya ndani, yameongezeka kutoka
TZS bilioni 336.6 mwaka 2015 hadi TZS bilioni 441.3 mwaka 2016. Hili ni ongezeko la TZS bilioni 104.7, sawa
na asilimia 31.1. Kadhalika, katika
kipindi hiki, Serikali imepokea jumla ya TZS bilioni 54.53 kutoka kwa Washirika
wetu wa Maendeleo, kuanzia mwezi wa Januari hadi Oktoba, 2016.
Natoa pongezi
kwa Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa
kazi nzuri waliyoifanya na nawahimiza waendelee na juhudi hizi, ili mapato
yanayokusanywa kwa kila mwaka yazidi kuongezeka kwa kiwango kikubwa zaidi.
Ndugu Wananchi,
Kwa upande wa
matumizi, Serikali imetumia jumla ya TZS bilioni 436.6 kwa kipindi cha Januari
hadi Oktoba 2016. Kwa jumla, katika kipindi hicho, Mapato ya Serikali
yalipindukia matumizi kwa jumla ya TZS bilioni 4.7, sawa na ongezeko la
asilimia 1.08. Haya ni mafanikio makubwa katika usimamizi wa fedha za umma. Jitihada
za kudhibiti matumizi zilizochukuliwa na Serikali, zimefanikiwa. Serikali itaendelea
kuyadhibiti matumizi ambayo si ya lazima na kwa hivyo, fedha za Serikali
zitaendelea kutumiwa katika kuwahudumia wananchi kwa mambo muhimu ya maendeleo
yao.
Katika kipindi
hiki, Serikali iliidhinisha jumla ya miradi 51 ya uwekezaji, yenye thamani ya USD
milioni 497.92. Katika miradi hiyo, asilimia 53 ni miradi inayomilikiwa na
wawekezaji wazalendo. Miradi hii inatarajiwa kutoa ajira zipatazo 2,658 na
hivyo inakwenda sambamba na azma ya Serikali yetu ya kupunguza tatizo la ajira,
na hatimae kupunguza umaskini.
Ndugu Wananchi,
Katika kipindi hiki, Serikali imeendelea
kuimarisha sekta ya biashara
ambayo ni muhimu kwa maisha na uchumi wetu. Juhudi hizo zimeiwezesha Serikali kuongeza
thamani ya bidhaa zilizosafirishwa nje ya nchi. Jumla ya bidhaa zenye thamani ya TZS
bilioni 94.94 zilisafirishwa nje
ya nchi katika mwaka 2016, ikilinganishwa na
bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni
45. 71, zilizosafirishwa mwaka 2015 . Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 99. Vile vile, jumla ya bidhaa zenye
thamani TZS bilioni 167.09 ziliingizwa nchini katika mwaka 2016, ikilinganishwa
na bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni 156.94, zilizoingizwa nchini mwaka
2015. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 7. Serikali inaendeleza juhudi katika kuongeza
usafirishaji wa bidhaa na kuimarisha kilimo ili kupunguza nakisi ya
biashara iliyopo.
Biashara kati
ya Zanzibar na Tanzania Bara inaendelea vizuri
na ambapo bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni 63.13 zilisafirishwa
kwenda Tanzania Bara na bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni 118.66
zilisafirishwa kutoka Tanzania Bara kuja Zanzibar, katika mwaka 2016.
Katika kuhakikisha
kwamba bidhaa zinazoingizwa zinakidhi viwango vinavyotakiwa, Serikali kupitia Shirika la Viwango la Zanzibar (ZBS),
imeanzisha mfumo wa ukaguzi wa bidhaa kwa lengo
la kumlinda mtumiaji na kuongeza mapato.
Ndugu
Wananchi,
Serikali
imeendelea kusimamia biashara ya karafuu kupitia Shirika la ZSTC. Wakulima wa karafuu wameendelea kulipwa TZS
14,000 kwa kilo moja, ikiwa ni sawa na asilimia 80 ya bei ya soko ya kuuzia nje. Katika mwaka 2015/16, ZSTC
ilinunua tani 5,764.8 za karafuu, kwa TZS bilioni 80.9 Katika mwaka 2015/16, ZSTC iliuza nje ya nchi,
jumla ya tani 5667 za karafuu, zenye thamani ya USD milioni 45.63, sawa na TZS
bilioni 98.2. Kadhalika, Shirika limeuza
nje ya nchi mafuta ya viungo yenye thamani ya TZS milioni 872.37 katika mwaka
2016.
Katika kipindi
hiki, Serikali imeendelea na utaratibu wake wa kuwapa wakulima wa karafuu miche
ya mikarafuu bure, kwa lengo la kuliendeleza zao hilo. Jumla ya miche 450,540 ya mikarafuu ilitolewa
Unguja na Pemba. Kadhalika, maandalizi
ya Mkakati wa Tasnia Malibunifu (Branding),
kwa karafuu za Zanzibar na viungo vyengine yalikamilishwa na majaribio
yake yamezinduliwa tarehe 6 Januari, 2017.
Ndugu Wananchi,
Miongoni mwa malengo ya Serikali, katika kipindi hiki cha
pili cha Awamu ya Saba, ni kuimarisha viwanda, ili kupunguza uagiziaji wa
bidhaa kutoka nje ya nchi, kuongeza usafirishaji wa bidhaa hizo kwenda nje, kuimarisha utumiaji wa malighafi
zinazopatikana nchini na kuongeza ajira kwa wananchi.
Sekta ya
Viwanda ilichangia asilimia 19.8 ya Pato la Taifa katika mwaka 2015 ikilinganishwa
na asilimia 16.8 mwaka 2014. Hii ni sawa
na ongezeko la asilimia 3.0. Katika
mwaka 2016, viwanda vitatu vikubwa vya watu binafsi, kiwanda cha maziwa cha Azam,
kiwanda cha “Zanzibar Milling Corporation”, kilichopo Mtoni na kiwanda cha
Sukari kilichopo Mahonda vimeendelea kufanya kazi ya uzalishaji. Aidha, Kiwanda cha Serikali cha Makonyo ya
Karafuu na Viungo vyengine kimeendelea
na uzalishaji. Vile vile, Kiwanda cha Matrekta, Mbweni kimefanya
kazi ya kuyatengeneza matrekta yote ya Serikali, kwa ajili ya kutoa huduma kwa
wananchi katika kilimo cha mpunga.
Ndugu Wananchi,
Katika kipindi
hiki, Serikali kwa kushirikiana na wawekezaji na wafanyabiashara, imeanza kuchukua
hatua ya ujenzi wa Ukanda wa Darajani na Michenzani, “Mapinduzi Square”, ambapo yatajengwa maduka
ya biashara, maeneo ya kuegesha gari, kumbi
za mikutano, ofisi na kadhalika. Michoro
kwa upande wa Darajani imetayarishwa na Serikali inawasiliana na UNESCO kwa
ajili ya kuzingatia utaratibu wa uhifadhi wa Mji Mkongwe. Ujenzi wa Darajani na Michenzani wote
utasimamiwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ya “ZSSF”.
Ndugu Wananchi,
Katika kipindi
hiki cha 2015/16, Serikali kwa kushirikiana na Kampuni ya SS Bakhresa imeanza
ujenzi wa miundombinu ya mji mpya wa
kisasa (Fumba Bay Satelite City), uliopo Fumba katika eneo la EPZ. Kadhalika, nyumba za kisasa 150 kati ya 500,
zimejengwa kwenye Mradi wa “Uptown living” unaoendeshwa na Kampuni ya “Union
Property Developers”. Mji mpya wa kisasa
wa (Fumba Bay Satelite City) na mradi wa nyumba mpya 150 “Uptown Living” zikiwa
kwenye hatua mbali mbali za ujenzi zimewekewa mawe ya msingi tarehe 9 Januari, 2017.
Vile vile, mradi
wa ujenzi wa nyumba za kisasa katika eneo la Nyamanzi umeanza kutekelezwa katika kipindi hiki. Hadi hivi, sasa nyumba 20 kati ya nyumba 1300 zimeanzwa
kujengwa na zimefikia katika hatua mbali mbali.
Ndugu Wananchi,
Kupitia Mfuko
wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF), Serikali ilianza kutekeleza mradi wa
ujenzi wa nyumba katika eneo la Mbweni. Mradi
huo ni wa ujenzi wa majengo 18 yenye
urefu wa ghorofa 7, yatakuwa na nyumba 252 (Flats). Hadi kufikia mwishoni mwa
mwezi Novemba 2016, tayari majengo matano yamejengwa yenye jumla ya nyumba 70 za kuishi. Majengo haya yanatarajiwa
kumalizika mwezi wa Aprili, 2016.
Ndugu Wananchi,
Kadhalika,
ujenzi wa hoteli kubwa ya kisasa ya “Verde” (Mtoni Marine) ya nyota tano na
vyumba 106, umeanza katika kipindi hiki na umefanyika kwa kasi sana. Hoteli hii inajengwa na Kampuni ya SS
Bakhressa iliwekewa jiwe la msingi tarehe 3 Januari, 2017, na ujenzi unatarajiwa kukamilika hivi
karibuni.
Ndugu Wananchi,
Kuhusu utalii, katika
mwaka 2016, jumla ya watalii 332,379 waliitembelea Zanzibar katika kipindi cha
Januari hadi Novemba, 2016. Idadi hii ni
ongezeko la asilimia 13 ikilinganishwa na watalii 294,243 waliofika nchini
mwaka 2015. Utalii ulichangia Pato la
Taifa kwa asilimia 27.
Katika kipindi
hiki, Serikali ilitekeleza uamuzi wake wa kukiunganisha Chuo cha Utalii
cha Maruhubi na Chuo Kikuu cha Taifa
(SUZA). Madhumuni ya uamuzi huu ulikuwa
ni kukiandaa Chuo hicho ili kutoa elimu ya juu kwa madhumuni ya kuimarisha
taaluma ya utalii na huduma zake kwa jumla.
Katika kipindi
hiki, Serikali imeendelea kutoa ruzuku ya
asilimia 75 ya gharama za pembejeo za
kilimo zikiwemo mbegu, mbolea, dawa za
magugu na huduma za matrekta kwa wakulima wa Unguja na Pemba. Kuhusu kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji,
katika kipindi hiki, Serikali imeendelea na ujenzi wa miundombinu ya
umwagiliaji maji kutoka hekta 800 za sasa hadi kufikia hekta 1,560, Pamoja na hatua hizo, Serikali ilianza ukarabati
wa ghala mbili za kuhifadhia chakula ambapo
jumla ya TZS milioni 200 zimeanza kutumika kwa ajili ya kukamilisha matengezo
makubwa ya ghala hizo ziliopo Malindi. Pamoja na matengenezo hayo ya ghala, vitendea
kazi vya ghalani vitanunuliwa ili lengo la kuhifadhia chakula liweze kufikiwa.
Kadhalika, Serikali
imeziimarisha shughuli za utafiti wa kilimo katika Taasisi ya Utafiti wa Kilimo
ya Kizimbani. Katika kipindi hiki, Taasisi hii iligundua mbegu mpya mbili za
muhogo zenye uzazi mkubwa na zenye kustahamili maradhi pamoja na kuendeleza
utafiti kwenye mbegu tatu za mpunga mpya.
Kuhusu Chuo cha
Kilimo Kizimbani, wahitimu 130 walimaliza
masomo ya Cheti cha Kilimo na wahitimu 100 katika Stashahada ya kilimo, katika
mwaka 2016. Wahitimu hawa, watapoajiriwa wataongeza nguvu katika kazi za ugani wa
kilimo na ufugaji.
Ndugu Wananchi,
Ufugaji bora na
wa kisasa ni miongoni mwa malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu
ya Saba. Katika kipindi hiki cha 2016, Serikali iliongeza jitihada katika
kuongeza kipato cha wafugaji. Mradi mkubwa wa mifugo ulizinduliwa kwa ufadhili
wa IFAD na “HEIFER International”. Mradi huu unatarajiwa kuongeza idadi ya
ng’ombe wa kisasa na uzalishaji wa maziwa.
Jumla ya
wafugaji mbali mbali walitembelewa na kupatiwa mafunzo ya kitaalamu na ufugaji
bora wa ng’ombe, mbuzi na kuku. Serikali
inaendelea kuziimarisha huduma za uchunguzi wa maradhi ya mifugo na utibabu kwa
kuongeza wataalamu, vifaa na kuimarisha maabara ya Maruhubi. Vile vile iliendeleza ujenzi wa vituo vya
karantini na vituo vya uzalishaji na
ilianza kuandaa utaratibu wa kuanzisha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo.
Ndugu Wananchi,
Serikali
imefanya jitihada kubwa katika kuendeleza sekta ya uvuvi. Maandalizi ya kuanzisha mradi wa kituo cha
kuzalisha vifaranga vya samaki huko Beit el Ras, yamekamilika. Mradi huo utasaidia kuongeza uzalishaji wa
vifaranga vya samaki kwa lengo la kuongeza idadi ya wafugaji na kurahisisha
upatikanaji wa samaki nchini.
Katika kipindi
hiki, kiwango cha samaki waliovuliwa mwaka 2016, kilifikia tani 33,000, wenye thamani ya TZS bilioni
136.2 ikilinganishwa na tani 31,435 wenye thamani ya TZS bilioni 123.8 mwaka 2015, ikiwa ni ongezeko la asimilia 5.26.
Matayarisho ya
ujenzi wa soko jipya la kisasa la samaki katika eneo la Malindi, yamekamilika katika kipindi hiki. Miundombinu ya maji, umeme na huduma nyengine
kutoka Serikalini zimeshafikishwa katika
eneo la ujenzi na wakati wote wote ujenzi
huo utaanza kwa ufadhili wa Serikali ya Japan.
Ujenzi wa soko la Malindi unakwenda sambamba na uamuzi wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar wa kuanzisha kampuni yake wenyewe ya uvuvi. Kampuni hiyo, inatarajiwa kuanza baadae mwaka
huu.
Kwa mwaka 2016,
uzalishaji wa mwani ulifikia tani 11,210 zenye thamani ya TZS bilioni 4.7. Kwa upande wa mwani, Zanzibar ni nchi ya
tatu ya uzalishaji wa zao hilo duniani. Serikali itaendeleza juhudi za
kuwatafutia wananchi soko la uhakika la mwani na kuwahamasisha kuongeza uzalishaji
wa zao hilo.
Ndugu Wananchi,
Serikali inachukua
jitihada mbali mbali katika kuimarisha matumizi bora ya ardhi ndogo tuliyo nayo, kukabiliana na athari za mazingira na kuongeza
kasi ya kutatua migogoro ya ardhi. Kuhusu
migogoro ya ardhi, jumla ya migogoro 215 imetatuliwa kati ya mwezi wa Januari
hadi Oktoba 2016 kwenye Mahkama ya Ardhi ikilinganishwa na migogoro 178
iliyotatuliwa katika kipindi kama hicho katika mwaka 2015. Natoa wito kwa
wananchi wazingatie Sheria ya Ardhi na Mipango Miji na Vijiji ili kuepuka
kuanzisha migogoro mengine maana hiyo iliyopita inatosha.
Ndugu Wananchi,
Kwa kipindi cha
mwaka mmoja uliopita, Serikali imefanya ufuatiliaji wa maeneo 35 yaliyoharibiwa
kutokana na uharibifu wa mazingira, 23 Unguja, na 12 Pemba.
Katika kutekeleza Sheria Namba 3 ya Usimamizi wa Mazingira ya Zanzibar ya
mwaka 2015, jumla ya miradi 33 imefanyiwa tathmini za kimazingira na kupewa
vyeti baina ya mwezi wa Januari hadi Oktoba, 2016.
Serikali itaendelea
kuelimisha wananchi kuhusu athari za uharibifu wa
mazingira na suala la mabadiliko ya tabianchi na itaendelea kushirikiana na
Washirika wa Maendeleo katika kukabiliana na
athari za mazingira pamoja na mabadiliko ya tabianchi.
Ndugu Wananchi,
Uimarishaji wa
miundombinu ya barabara ni muhimu katika kuchochea kasi ya maendeleo ya
kiuchumi na kuimarisha huduma za jamii. Katika
kuimarisha ujenzi wa barabara, kwa upande wa Unguja, kazi ya ujenzi wa barabara
ya Mwanakwerekwe hadi Fuoni Polisi (km 4) imekamilika. Barabara
kutoka Maktaba Kuu hadi Gofu, Kwarara hadi
Fuoni pamoja na barabara ya Kinazini hadi Kariakoo
zimefanyiwa matengenezo ya dharura kwa kiwango cha lami. Aidha, ujenzi
wa barabara ya Jendele kupitia Cheju hadi Unguja Ukuu Kaebona, (km 11.7), matengenezo
yake yanaendelea vizuri ambapo km 3, kati ya hizo zimeshakamilika kwa
kiwango cha lami.
Kwa upande wa
Pemba, Serikali inaendelea na ujenzi wa barabara ya Ole hadi Kengeja (km 35)
katika hatua ya kuweka kifusi, na km 11, kati ya hizo zimekamilika. Ujenzi huo bado unaendelea. Aidha, kazi ya
ujenzi wa barabara kutoka Mgagadu hadi Kiwani (km 7) kwa kiwango cha lami utakamilika
mwezi huu wa Januari.
Ndugu Wananchi,
Katika mwaka
2016, idadi ya abiria waliotumia bandari zetu za Unguja na Pemba walifikia
2,412,657 kutoka abiria 1,938,857 mwaka 2015, sawa na ongezeko la abiria
473,800, ikiwa ni sawa na asilimia 19.6.
Katika kuimarisha huduma za bandari za kupakia na kuteremsha makontena
na mizigo mengine, Serikali imenunua vifaa vipya vya kutekeleza kazi hiyo. Jumla ya TZS bilioni 11.00 zimetumika katika
kununua vifaa na zana mbali mbali,
katika mwaka 2016. Vifaa hivyo
vimezinduliwa rasmi, katika shamra shamra za sherehe za Mapinduzi hapo tarehe 4
Januari, 2016.
Aidha, huduma
za usafiri wa meli za Serikali baina ya visiwa vya Unguja na Pemba zimekuwa za
uhakika zaidi, baada ya Serikali kununua
meli mpya ya MV Mapinduzi II, ambayo tayari imeshaanza kufanya kazi baina ya
Unguja, Pemba na Dar es Salaam katika kipindi cha mwaka mmoja. Matayarisho ya
ununuzi wa meli nyengine ndogo ya mizigo na abiria inayolingana na MV Maendeleo
pamoja na meli ya mafuta inayolingana na meli ya MT Ukombozi yamekamilika. Meli hizi mbili zinatarajiwa kununuliwa
katika mwaka huu wa fedha.
Ndugu Wananchi,
Kadhalika,
katika kuimarisha huduma za uwanja wa ndege, Serikali imenunua gari mpya nne za
kisasa za zimamoto. Kituo kipya cha
zimamoto kimejengwa, kitakachoweza kuzihifadhi gari zote nne kwa wakati mmoja,
pamoja na ofisi za maofisa wa zimamoto, ghala,
na kadhalika.
Katika mwaka
2016, Serikali iliendelea na mpango wake wa kuimarisha kiwanja cha ndege cha
kimataifa cha Abeid Amani Karume. Ujenzi
wa jengo la abiria jipya ulisita
kutokana na changamoto zilizojitokeza. Hata hivyo, changamoto hizo zitapatiwa
ufumbuzi hivi karibuni na ujenzi utaendelea.
Kuhusu uwanja wa ndege wa Pemba, mipango ilitayarishwa ya kufanya
upembuzi yakinifu kwa kukipanua kiwanja hicho, ili ndege kubwa za aina ya
Boeing 737 - 800 ziweze kutua pamoja na ujenzi wa jengo la abiria jengine. Fedha kwa ajili ya kazi hio tayari
zimepatikana kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika.
Ndugu Wananchi,
Kuanzia mwezi
Februari hadi Oktoba 2016, jumla ya vijiji 34 vimepatiwa umeme, Unguja na Pemba,
ambapo vijiji 17 kati ya hivyo ni vya Unguja na 17 vya Pemba. Matayarisho ya
kupeleka umeme katika Kisiwa cha Fundo, Pemba, yameanza ambapo kazi hiyo
inatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2017. Aidha, Serikali imepanga kuufikisha
umeme katika Kisiwa cha Kokota na Uvinje huko Pemba.
Katika kuhakikisha
wananchi wenye kipato cha chini wanafaidika na huduma za umeme, katika mwaka wa
fedha 2014/2015 na mwaka 2015/2016, wananchi wapatao 4,487 wameungiwa umeme kwa
njia ya mkopo. Mikopo iliyotolewa ina thamani ya
TZS bilioni 1.35. Kati ya wananchi walionufaika na mikopo hiyo, 1,290 ni wa Unguja na 3,197 ni kutoka Pemba.
Ndugu Wananchi,
Tarehe 15
Novemba, 2016 Zanzibar, ilifungua ukurasa mpya wa historia kufuatia kutiwa
saini kwa Sheria Namba 6 ya Utafutaji na
Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia ya mwaka 2016, inayoipa uwezo Zanzibar
kushughulikia utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia. Kwa mara
nyengine tena, natoa shukurani zangu za dhati kwa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Awamu ya Nne, Mhe. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa jinsi
tulivyoshirikiana, ili kuhakikisha kwamba kabla hajaondoka madarakani, suala la Zanzibar kusimamia utafutaji na
uchimbaji wa mafuta na gesi asilia, linapatiwa ufumbuzi.
Hivi sasa,
Serikali inaendelea na mazungumzo na wawakilishi wa kampuni za mafuta
zilizojitokeza ili hatua za utafutaji na baadae uchimbaji wa mafuta na gesi
asilia uweze kuanza.
Ndugu
Wananchi,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
imeendelea kutoa elimu bila ya malipo wala ubaguzi. Katika mwaka 2016, idadi ya skuli imeongezeka
kutoka 792 mwaka 2015 hadi 843, sawa na ongezeko la asilimia 7. Idadi ya wanafunzi walioandikishwa, nayo
imeongezeka kutoka wanafunzi 388,616 mwaka 2015 hadi kufikia 424,074 mwaka
2016, sawa na ongezeko la asilimia 8.36.
Kwa lengo la kuondoa msongamano wa wanafunzi katika skuli za sekondari,
Serikali imeshakamilisha michoro ya ujenzi wa skuli 9 za ghorofa zitakazojengwa
katika Wilaya ya Mjini, Magharibi A na B kwa Unguja na Wilaya zote nne za
Pemba. Fedha za ujenzi huo tayari
zimepatikana kutoka Benki ya Dunia.
Aidha, vituo
viwili vipya vya mafunzo ya amali vimeanza kujengwa huko Makunduchi, Unguja na
Daya Mtambwe, Pemba kwa mkopo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika. Vile vile,
jengo jipya la Taasisi ya Karume ya Sayansi na Teknolojia litakalokuwa
na madarasa, maabara na karakana limeanza kujengwa na jiwe la msingi liliwekwa
rasmi tarehe 8 Januari, 2017 na linatarajiwa kukamilika, mwezi wa Mei,
2017.
Ndugu
Wananchi,
Mafanikio yamepatikana katika
kuimarisha elimu ya juu. Idadi
ya wanafunzi wanaosoma elimu ya juu katika vyuo vikuu vya Zanzibar imeongezeka,
kutoka wanafunzi 6,370 mwaka 2015 hadi kufikia 7,383 mwaka 2016, ongezeko hili
ni sawa na asilimia 5.9. Katika kupanua
fursa za elimu ya juu, Serikali imekiunganisha Chuo Kikuu cha Taifa cha
Zanzibar (SUZA) na Chuo cha Utalii Maruhubi,
Chuo cha Ukaguzi wa Fedha Chwaka pamoja na Chuo cha Sayansi za Afya
Mbweni, ili vyuo hivyo vilivyounganishwa viweze fursa ya kutoa elimu ya juu na
kuongeza idadi ya wanafunzi wa elimu ya juu.
Kuhusu mikopo
ya elimu ya juu, Serikali imetoa mikopo
kwa wanafunzi 2,655 na jumla ya TZS bilioni 3.7 zimetolewa kwa ajili
ya wanafunzi hao. Kadhalika, Serikali
imekusanya jumla ya TZS milioni 480 kutoka
kwa wahitimu waliorudisha mikopo, kwenye Bodi ya mikopo ya Elimu ya Juu.
Nawahimiza wahitimu wanaodaiwa, wayalipe madeni yao hayo, ili wanafunzi wengine
nao waweze kufaidika.
Ndugu
Wananchi,
Kwa kutambua
umuhimu wa afya kwa wananchi, katika mwaka 2016 Serikali imeendelea kuchukua
hatua madhubuti ili kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote mijini
na vijijini bila ya ubaguzi.
Katika mwaka
2016, vituo vinne vipya vya afya vimejengwa
na kuifanya Zanzibar kuwa na jumla ya vituo vya afya 152 ikiwa ni ongezeko
la asilimia 13.4 ikilinganishwa na vituo 134 katika mwaka 2014/2015. Matengenezo
makubwa yamefanywa katika kuimarisha miundombinu ya hospitali za Koteji na
kuzipatia vifaa vya kisasa vya kutolea huduma na vitafikia hadhi ya hospital za
Wilaya hivi karibuni.
Ndugu Wananchi,
Katika
kuimarisha huduma za rufaa kwenye Hospitali ya Mnazi Mmoja, ujenzi wa wodi ya
wazazi ya vitanda 100 na wodi ya watoto yenye vitanda 100, pamoja na vyumba
maalum vya kutolea huduma za maradhi ya figo, zilizinduliwa rasmi tarehe 21
Novemba, 2016. Vifaa vipya vya kisasa vimewekwa
katika wodi zote mbili. Sheria ya kuiongoza Hospitali ya Mnazi Mmoja
imetungwa na tayari inafanya kazi na Bodi ya Ushauri, nayo tayari imeteuliwa na
imeanza kazi zake.
Baada ya
kujengwa upya, Hospitali ya Abdalla Mzee, iliopo Mkoani Pemba na kutiwa vifaa
vya kisasa vya matibabu na uchunguzi wa maradhi kwa ajili ya kutolea huduma,
hospital hii iliyopandishwa daraja kuwa ya Mkoa, ilizinduliwa rasmi tarehe 26
Novemba, 2016. Hospitali hii itakuwa na
uwezo wa kulaza wagonjwa 160 kwa wakati mmoja, wenye matatizo mbali mbali. Hospitali
ya Wete na Chake Chake nazo zimeimarishwa katika kipindi hiki, kwa kupatiwa
vifaa na nyenzo mbali mbali za kutolea huduma.
Ndugu Wananchi,
Jitihada zetu
zimefanikiwa sana katika kupambana na maradhi kwa kushirikiana na taasisi mbali
mbali duniani. Mafanikio yaliyopatikana
yanatia moyo dhidi ya mapambano ya UKIMWI, Malaria, Kipindupindu, Kifua Kikuu,
na maradhi mengine ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza. Kiwango cha malaria na kasi ya kuenea kwake, kimezidi
kushuka na kufikia asilimia 0.4, mwaka
2015-2016, kutoka asilimia 0.6, mwaka 2013-2014.
Upatikanaji wa
dawa katika hospitali zote na katika vituo vya afya vyote vya Serikali
umeimarika sana baada ya kuongeza bajeti ya Serikali, kutoka TZS bilioni 4.3,
mwaka 2015/2016 hadi kufikia TZS bilioni 4.9 mwaka 2016/2017 pamoja na TZS
bilioni 1.5 kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.
Fedha za kununulia dawa zilifikia TZS bilioni 6.4 sawa na ongezeko la
asilimia 48.8.
Maradhi ya
kipindupindu yaliikumba nchi yetu kuanzia Septemba, 2015 hadi Julai, 2016. Jumla ya wagonjwa 4,330 waliambukizwa na
kutibiwa maradhi hayo katika vituo 21, vilivyofunguliwa Unguja na Pemba. Kati ya wagonjwa hao, wagonjwa 48 sawa na
asilimia 1.5 walifariki dunia na maradhi hayo hivi sasa yamemalizika. Serikali inawapa pole, wafiwa, ndugu na jamaa
wa ndugu zetu hawa waliofariki.
Ndugu Wananchi,
Hadi sasa,
mahitaji ya jumla ya maji safi na salama kwa Mikoa yote ya Zanzibar kwa siku ni
lita milioni 177.4 na maji yanayopatikana ni lita milioni 140.7, sawa na asilimia 79.3 ya
mahitaji. Kwa kiwango hiki, upungufu uliopo kwa siku ni lita milioni 36.7 sawa
na asilimia 20.7. Hata hivyo, Serikali ilifanya
jitihada katika kukabiliana na hali hiyo ya upungufu wa maji katika maeneo
mbali mbali.
Katika Mkoa wa
Mjini Magharibi, Serikali kupitia Mamlaka ya Maji ya Zanzibar (ZAWA), imeanza
kutekeleza Mradi wa Kuimarisha Miundombinu ya Maji (ZUWSP) katika shehia 27 za Mji Mkongwe na Ng’ambo ya zamani. Kupitia mradi huu, visima vipya 9
vitachimbwa, visima 23 vya zamani vitatengenezwa na mabomba yenye urefu wa
kilomita 68 yatalazwa. Kadhalika, matangi makubwa matatu; yatajengwa Saateni na
Mnara wa Mbao. Mradi huu utatekelezwa
kwa fedha za mkopo wa USD milioni 21.25
kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika na mchango wa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar wa USD milioni 2.428.
Vile vile, visima
150 vilivyochimbwa kwa msaada wa
Serikali ya Ras-Al-Khaimah vinaendelezwa ili viweze kutumika. Hadi mwisho wa mwezi Disemba, 2016 visima 17 kati
ya vilivyochimbwa, maji yalianza kupatikana.
Ndugu Wananchi,
Kwa upande wa
miradi itakayotekelezwa hapo baadae kwa ajili ya kuimarisha huduma za maji,
jumla ya USD milioni 92, ikiwa ni mkopo kutoka Serikali ya India zimepatikana
kwa ajili ya kuimarisha huduma za maji katika Wilaya ya Magharibi B na baadhi
ya maeneo katika Mkoa wa Mjini Magharibi.
Vile vile, jumla ya USD milioni 100 zitatolewa na Serikali ya Japan, ikiwa
ni msaada kwa ajili ya kuimarisha huduma za maji katika eneo la Migombani, Dole
na Fumba. Kadhalika, Serikali ya Jamhuri
ya Watu wa China, itasaidia uchimbaji wa visima na usambazaji maji huko Chaani,
Donge, Kisongoni na Miwani.
Ndugu Wananchi,
Katika
kuliimarisha Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), Serikali, mnamo mwezi wa
Novemba, 2016, imenunua vifaa vipya vya
kisasa na mitambo kwa ajili ya ZBC TV na Radio.
Vifaa hivyo vinatarajiwa kufika nchini hivi karibuni. Vile vile, vifaa mbali mbali vimeagizwa pamoja
na ving’amuzi vipya na vya kisasa kwa ajili ya mitambo ya digitali ya ZBC TV. Kwa kupatikana vifaa hivyo, ZBC wataweza
kuzima, mitambo ya “Analog” kuanzia Aprili mwaka huu. Aidha, jengo la “Karume House” na jengo la
ZBC Radio yameanza kufanyiwa matengenezo makubwa ili yalingane na vifaa
vitakavyowekwa.
Kwa upande wa
Shirika la Magazeti la Zanzibar, Serikali
imeanza kununua vifaa vipya na nyenzo mbali mbali na kulikarabati jengo
litakalotumiwa na wafanyakazi wa Zanzibar Leo liliopo Kikwajuni. Katika kipindi hiki, uongozi wa gazeti wa Zanzibar Leo utaongeza
usambazaji wa gazeti hilo kutoka nakala 692 hadi 3,000.
Ndugu Wananchi,
Hivi karibuni
Serikali imetoa tamko la Kisheria
Nambari 54 la mwaka 2016 kwa lengo
la kuimarisha utendaji wa
iliyokuwa Idara ya Upigaji
Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na kuanzisha Wakala wa Serikali wa Uchapaji Zanzibar. Aidha, mitambo mipya ya kisasa ya upigaji chapa ilinunuliwa na ilifungwa
kwenye jengo jipya hapo Maruhubi. Baada
ya jitihada hizi, hivi sasa kazi zote za Wizara zote za Serikali za upigaji chapa zinatekelezwa katika Wakala
wa Serikali wa Upigaji Chapa Zanzibar na pia, utatengeneza gazeti la Zanzibar
Leo ambalo litachapishwa hapo.
Ndugu Wananchi,
Shughuli za
utamaduni na michezo zimeendelezwa vyema katika mwaka 2016. Tamasha la Filamu la Kimataifa la Zanzibar
(ZIFF), Sauti za Busara na Tamasha la Utamaduni wa Mzanzibari, yamefanyika. Wasanii wa fani mbali mbali, wameendelea
kuitumia studio mpya ya Rahaleo kwa ajili ya kurekodia kazi zao. Kuhusu sekta ya michezo, maadhimisho ya siku
ya mazoezi yanayofanyika kila mwaka tarehe 1 Januari yameendelezwa. Vile vile, Serikali imeendelea kutoa vifaa
vya michezo kwa timu mbali mbali na imeanza
kutekeleza Agizo la Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020, ambapo
kiwanja cha michezo kwa Wilaya ya Kusini Unguja, kimeanza kujengwa Kitogani,
kati ya viwanja vitano vilivyoagizwa kwenye Ilani.
Kwa lengo la
kukabiliana na tatizo la ajira kwa vijana, Serikali imechukua hatua ya
kuimarisha Mfuko wa Vijana unaoratibiwa na Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi
Kiuchumi, ili kuwawezesha vijana wajiajiri wenyewe. Hadi kufikia
Novemba, 2016, mikopo ya TZS bilioni 1.075 imetolewa kwa vijana 2,326, Unguja
na Pemba. Vile vile, vijana 1,824 waliajiriwa
kwenye sekta binafsi katika mwaka 2016 na ajira kutoka Serikalini zilikuwa 711.
Ndugu
Wananchi,
Mafanikio
yamepatikana katika kuuendeleza Mfuko wa Kuwawezesha Wananchi Kiuchumi, ambapo hadi
kufikia Disemba, 2016 jumla ya TZS bilioni 1.76 wamekopeshwa wananchi
wanaofanya shughuli mbali mbali Unguja na Pemba. Kati ya fedha hizo zilizokopeshwa, TZS bilioni
1.06 tayari zimelipwa. Katika jitihada
za kuandaa ajira, Serikali imeanzisha kituo cha kulelea wajasiriamali Mbweni
ambapo wajasiriamali 819 wamepatiwa mafunzo.
Kituo hicho kimepanuliwa ili kutoa fursa zaidi kwa wajasiriamali. Aidha,
Serikali ina mpango wa kujenga kituo kama hicho katika eneo la Tibirinzi Chake
Chake Pemba, ili wajasiriamali wa Pemba nao waweze kufaidika na huduma za
mafunzo ya ujasiriamali.
Aidha, katika kukabiliana na vitendo
vya udhalilishaji wa wanawake na watoto, Serikali imeendeleza kampeni kwa
kupiga vita vitendo hivyo, ambapo vituo vya mkono kwa mkono vimesaidia sana. Wananchi wengi wameunga mkono mapambano haya. Hata hivyo, tatizo la udhalilishaji bado
lipo. Katika mwaka huu, Serikali
itaandaa mikakati maalum katika kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa
wanawake na watoto. Natoa wito kwamba
sote tushirikiane katika kuvikomesha vitendo hivi viovu.
Ndugu
Wananchi,
Serikali imeanza kuwalipa wazee TZS
20,000 ikiwa ni pencheni ya jamii kwa mwezi kwa wazee waliofikia umri wa miaka
70, kwa Unguja na Pemba kwa lengo la kuwatunza.
Hadi Disemba 2016, jumla ya wazee 25,259 waliosajiliwa wamelipwa ambapo
TZS bilioni 4.3 zimetumika.
Katika mwaka 2016, Serikali imeendelea
kuwatunza wazee wanaoishi katika nyumba za wazee Sebuleni, Welezo na Limbani
kwa kuwapatia malazi, matibabu na fedha za matumizi ya kila mwezi.
Kadhalika, jitihada za kuwahudumia watu
wenye ulemavu zimefanywa ambapo jumla ya watu 125 walipewa vifaa vikiwemo
magongo ya kutembelea, viti vya magurudumu na fimbo nyeupe. Vile vile, jumla watu wenye ulemavu 16,611
wamesajiliwa ili kurahisisha namna ya kuwahudumia. Aidha, hadi sasa jumla ya TZS milioni 167.4
zimekusanywa kwa ajili ya kuendeleza Mfuko wa watu wenye ulemavu ambazo
zitatumika kwa ajili ya kuwaendeleza.
Ndugu Wananchi,
Serikali, katika
mwaka 2016, imeshughulikia nidhamu za wafanyakazi kwa mujibu wa Sheria Nam. 2
ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2011 na Kanuni za Kazi. Wapo watumishi walioondoshwa kwenye dhamana
za uteuzi kwa kukiuka maadili ya kazi, vile vile, wapo waliosimamishwa kazi
kutokana na ubadhirifu wa mali za umma na wanaendelea kuchunguzwa na kushughulikiwa
na taasisi zinazohusika. Katika kipindi
hiki, Serikali imesimamia udhibiti wa matumizi ya fedha za umma kwa kupunguza
safari za nchi za nje na za ndani ya nchi kwa watumishi wa umma. Mikutano, semina na kongamano imefanyika bila
ya wahusika kulipwa posho katika wakati wa saa za kazi.
Kwa jumla, uwajibikaji
wa wafanyakazi kazini umeongezeka ingawa bado wapo wafanyakazi wanaoendelea
kufanya kazi kwa mazowea. Serikali,
itaendelea kuchukua hatua za ziada ya kusimamia nidhamu kazini. Zaidi ya hayo
katika kipindi hichi mipango yote inakamilika ya kuwalipa wafanykaazi wa
Serikali kima cha chini cha mshahara kutoka TZS 150,000 kwa sasa hadi TZS
300,000, kiwango hichi kimeongezeka sasa kwa asilimia mia moja, mshahara huu
mpya utaanza kulipwa kuanzia mwezi April hivi karibuni.
Katika mwaka
2016, Serikali imeimarisha mfumo wa sheria, kupitia mradi wa mageuzi ya sekta
ya sheria, kwa kufanya mabadiliko katika utendaji kazi wa Mahkama, Ofisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Vyuo vya Mafunzo. Taasisi hizo zimejengewa uwezo zaidi. Mahkama ya Chake Chake imezinduliwa rasmi,
baada ya ukarabati mkubwa, ujenzi wa Mahkama ya watoto ya Mahonda umekamilika
na matayarisho ya ujenzi wa Mahkama Kuu mpya huko Tunguu umeanza.
Katika mwaka
2016, Baraza la Wawakilishi limetekeleza majukumu yake kwa kufanya mikutano
minne ya kawaida, ukiwemo mkutano mmoja wa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka
2016/2017. Jumla ya maswali 910
yaliulizwa na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, kati ya hayo maswali 254
yalikuwa ni ya msingi na 656 ya nyongeza.
Maswali yote hayo yalijibiwa na
mawaziri wa Wizara mbali mbali.
Kadhalika,
jumla ya miswada 12 ya sheria imejadiliwa na kutungiwa sheria. Miongoni mwa hiyo ni, ule unaohusiana na
Sheria Namba 6 ya mwaka 2016 ya Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia
na marekebisho madogo ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kuhusu uteuzi wa
Rais wa nafasi 10 za wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.
Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la
kukabiliana na vitendo vya rushwa na uhujumu wa uchumi, katika kipindi cha
mwaka 2016, Mamlaka ya Rushwa na Uhujumu wa Uchumi imeshughulikia tuhuma 46
ambazo zipo katika hatua nzuri za uchunguzi na 6 zipo Mahkamani. Kadhalika, Mamlaka imeendelea kutoa elimu kwa
wananchi juu ya madhara ya vitendo vya rushwa na uhujumu wa uchumi kwenye
shehia 123 Unguja na Pemba.
Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma iliyoanzishwa
kwa mujibu wa Sheria Nam. 4 ya mwaka 2015, ilianza kazi zake mwezi wa Aprili,
2016. Viongozi wa Umma, walipewa fomu za
Tamko la Mali na Madeni na kutakiwa wazijaze na wazirudishe fomu hizo kwenye
Tume si zaidi ya tarehe 31 Disemba, 2016. Wale viongozi ambao walishindwa
kuziwasilisha fomu zao, baada ya tarehe 31 Disemba, 2016; watakuwa wamevunja
sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Tume ya Maadili ya Umma itawachukulia hatua. Kadhalika, Tume itazihakiki
taarifa zote zilizowasilishwa na viongozi wa umma.
Katika mwaka
2016, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ziliandaa Kongamano la Tatu la Watanzania wanaoishi
nchi za nje ambalo lilifanyika Zanzibar kwa mafanikio. Kadhalika, Wazanzibari wanaoishi nje ya
nchi walichangia kujenga madarasa ya
skuli, kutoa vitabu vya masomo mbali mbali pamoja na samani katika skuli na
vyuo vyetu nchini.
Ndugu
Wananchi,
Kudumishwa kwa
Mapinduzi ya Zanzibar ambayo leo yametimiza miaka 53, lazima twende sambamba na
kudumishwa na kuendelezwa kwa Muungano wa Tanzania ambao ifikapo tarehe 26
Aprili mwaka huu wa 2017 utatimiza miaka 53 tangu kuasisiwa kwake.
Kadhalika,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuyaendeleza masuala ya Muungano. Vile vile, tutahakikisha kuwa
tunashirikiana katika mambo yasiyo ya
Muungano kwa faida ya pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mimi na
Mheshimiwa Dk. John Pombe Joseph Magufuli tunatambua uzito wa dhamana mliyotupa
Watanzania katika kuhakikisha kwamba Muungano wa Tanzania unadumu na unaimarika
kwa dhamira ile ile ya viongozi wetu wa Awamu zilizotangulia.
Ndugu
Wananchi,
Siri kubwa ya
mafanikio tunayoendelea kuyapata nchini ni kuendelea kuwepo kwa amani na
utulivu. Kwa hivyo, kuhimiza amani na
kuiendeleza ni wajibu kwa viongozi wote pamoja na wananchi. Tusichoke kuhimizana juu ya umuhimu wa amani, ili tuweze kupiga
hatua zaidi katika kukuza uchumi na ustawi wa wananchi. Nakuhakikishieni wananchi nyote, kwamba
Serikali zetu zote mbili; zitachukua
hatua ili nchi yetu inabaki kuwa nchi ya amani na utulivu.
Ndugu Wananchi,
Nakamilisha
hotuba yangu kwa kutoa shukurani zangu za dhati kwa mara nyengine tena kwa
viongozi na wageni wetu wote mliokuja kutuunga mkono katika maadhimisho ya
Miaka 53 ya Mapinduzi. Vile vile, natoa
shukurani zangu kwa Kamati ya Halmashauri ya Sherehe na Maadhimisho
inayoongozwa na Mheshimiwa Makamo wa Pili wa Rais; Balozi Seif Ali Iddi kwa uongozi wake mahiri
ambao umezifanikisha sherehe zetu hizi.
Vile vile, natoa
shukurani kwa nchi zote marafiki, washirika wetu wa maendeleo, taasisi na
mashirika ya kimataifa wanaoshirikiana nasi katika kuifanikisha mipango yetu ya
maendeleo. Kadhalika, natoa shukurani kwa
viongozi na wafanyakazi wote wa Serikali kwa jitihada zenu za kuwatumikia
wananchi wote kwa misingi ya haki, uadilifu na utumishi bora. Matumaini yangu ni kuwa tutaendelea kushirikiana
na kuongeza kasi katika kuyatekeleza majukumu yetu, ili nchi yetu izidi kupiga
hatua za maendeleo.
Kadhalika, shukurani
zangu, zende kwa makamanda na wapiganaji
wa vikosi vyetu vya ulinzi na usalama kwa
kuendelea kudumisha ulinzi wa nchi yetu na mipaka yake. Vile vile, nawapongeza kwa gwaride la
ukakamavu lililozipamba sherehe zetu za leo.
Aidha, natoa shukurani kwa wasanii waliotuburudisha, vijana wetu, pamoja
na wafanyakazi wa vyombo vya habari pamoja kwa kuzitangaza sherehe zetu kwa
wananchi ambao kwa sababu mbali mbali hawakuweza kuhudhuria. Nakutakieni nyote
safari njema ya kurudi nyumbani.
MAPINDUZI DAIMA
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU IBARIKI TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment