Habari za Punde

Hospitali za Kivunge na Makunduchi kuwa za Mkoa

 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                    26.2.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imedhamiria kuzipandisha hadhi Hospitali ya Kivunge na Makunduchi kuwa za Mkoa katika kipindi kifupi kijacho.

Dk. Shein aliyasema hayo katika chakula cha usiku kilichoandaliwa na Wizara ya Afya kwa ajili ya kuchangia fedha za kusaidia Hospitali ya Makunduchi na Hospitali ya Kivunge ikiwa ni pamoja na maadhimisho ya miaka kumi ya Mradi wa kuendeleza huduma za afya Zanzibar (HIPZ), huko katika ukumbi wa Hoteli ya Park Hyatt mjini Zanzibar.

Katika hotuba yake, Dk. Shein alisema kuwa juhudi za Mradi wa kuendeleza huduma za afya Zanzibar (HIPZ), sio tu umeweza kusaidia kuziweka hospitali za Makunduchi na Kivunge katika hali nzuri na bora katika utoaji wa huduma lakini amesema mradi huo umesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa uongozi wa Mradi huo wa HIPZ kwa kuweza kuimarisha huduma za afya, miundombinu, usimamizi na uwajibikaji katika Hospitali hizo.

Aliongeza kuwa Mradi wa HIPZ umesaidia sana kutekeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuzifanya Hospitali hizo kuwa na hadhi ya Hospitali ya Wilaya hali ambayo imeonesha njia ya kutekeleza lengo la kuzifanya Hospitali hizo kuwa za Mkoa.

Aidha, Dk. Shein alitoa wito kwa Wizara ya Afya kuimarisha utoaji mafunzo kupitia Maradi huo kwa madaktari wazalendo kupitia madaktari wageni wanaokuja kufanya kazi Zanzibar kupitia katika Mradi huo wa HIPZ.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi kuendelea kuzitumia huduma zinazotolewa na wataalamu wa HIPZ kupitia Hospitali  ya Kivunge na Makunduchi  badala ya kukimbilia Hospitali Kuu ya MnaziMmoja.

Dk. Shein katika alieleza juhudi za Serikali katika kuimarisha sekta ya afya nchini ikiwa ni pamoja na kuimarisha huduma za afya, ujenzi wa Hospitali ya Abdalla Mzee, Hospitali ya Mnazi Mmoja, kuimarisha miundombinu ya hospitali, vifaa na mafunzo huku akieleza kuwa Serikali imeongeza Bajeti ya Wizara ya Afya kutoka Tsh. Bilioni 4.3 mwaka 2015/2016 hadi kufikia Bilioni 4.9 katika mwaka wa fedha wa 2016/2017.

Katika maelezo yake kwenye hotuba hiyo Dk. Shein alisema kuwa Mradi huo wa HIPZ umeimarishwa kwa mashirikiana kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzbar pamoja na madaktari kutoka nchini Uingereza, Canada na sehemu nyengine duniani.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwaahidi viongozi wa Mradi huo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Znzibar itaendea kuwaunga mkono ili Mradi huo uwe endelevu na uweze kufanya kazi vizuri.

Alitumia fursa hiyo pia, kuwashukuru Washirika wa maendeleo kwa kuendeleza aushirikiano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha huduma za afya.

Katika hafla hiyo jumla ya Tsh. Milioni 67 zilichangwa katika harambee ilioendeshwa ukumbini hapo ambapo Dk. Shein alichangia milioni kumi pamoja na Mama Mwanamwema Shein nae alichangia milioni tano.

Nae Waziri wa Afya, Mahamoud Thabit Kombo kwa upande wake alieleza mashirikiano mazuri yaliopo kati ya HIPZ na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake ya Afya na kumpongeza Rais  Dk. Shein  kwa kuwa kiungo kati Wizara hiyo na Mradi huo wa HIPZ.

Nao viongozi wa HIPZ kwa nyakati tofauti walieleza mafanikio na changamoto walizokabiliana nazo ndani ya miaka kumi ya Mradi huo na kuahidi kuendelea kuiunga mkono Serikali katika kuimaruisha sekta ya afya hapa nchini.

Sambamba na hayo walieleza mashirikiano mazuri waliyoyapata kutoka Serikalini pamoja na kutoka kwa washirika mbali mbali wa maendeleo.

Mradi wa HIPZ ulianzishwa mwaka 2006 ambao unafanyakazi chini ya Wizara ya Afya ili kuimarisha huduma zote za afya za Hospitali ya Makunduchi na Kivunge.

Viongozi mbali mbali walihudhuria katika hafla hiyo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Idd, Mama Asha Balozi, Mawaziri, viongozi Serikali na viongozi wa  HIPZ wakiongozwa na  Dk. Ruaraidh Mac Donagh pamoja na wageni wengine.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.