Habari za Punde

Karafuu za magendo zakamatwa Micheweni


 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskzini Pemba, Haji Khamis Haji, akitowa maelezo ya kukamatwa kwa karafuu hizo ambazo zilikuwa zinataka kusafirishwa kwa magendo.

 Gari za aina ya Noha na gari la Ng'ombe ambazo zilikamatwa  zikiwa zimepakia Karafuu  za magendo mkoa Kaskazini Pemba.


Picha na Hanifa Salim-Pemba.


NA/ HANIFA SALIM—PEMBA.

JUMLA ya magunia matano ya Karafuu kavu yenye uzito wa kilo 300, yamekamatwa na vikosi vya Ulinzi na usalama katika maeneo ya Chanjaani na kiperani Konde Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Magunia mawili yalikamatwa Januari 4 yakiwa katika gari aina ya Noah yenye namba Z529GH na matatu Febuari 8 mwaka huu yakiwa katika gari ya Ng’ombe ambayo yalikamatwa na askari wa Vikosi vya ulinzi na usalama wakiwa katika doria majira ya saa 7:00 usiku.

Akizungumza na mwandishi wa habari Mkurugenzi mwendeshaji wa Shirika la ZSTC Zanzibar, Said Seif Mzee, aliwataka wananchi kuuza Karafuu ZSTC, alisema  karafuu ni zao la nchi ambalo linamgusa kila Mzanzibar hivyo wananchi wanapouza karafuu ZSTC inasaidia Serikali kuongeza mapato.

Alisema  Serikali imefanya juhudi ya kuwalipa wananchi bei nzuri kwa mauzo ya zao la Karafuu ambayo bei hiyo haipatikani katika nchi yoyote, hivyo ni vyema jamii iache kusafirisha karafuu kwa njia ya magendo.

“Katika kuziangalia karafuu hizi ambazo zimekamatwa zimeonekana kuwa vimechanganywa na makonyo ambapo hii ni kutokana na kutaka waziongeze uzito njambo ambalo ni kosa kisheria” alisema.

Hata hivyo thamani ya Karafuu hizo , haikuweza kupatikana kwa vile hazijafanyiwa upasishaji, na kutiwa bei yake halisi kulingana na ubora ilizonazo.

Alieleza  kwa mujibu wa sheria ya maendeleo ya Karafuu ya mwaka 2014, Sheria namba mbili sehemu ya 19 kifungu cha kwanza hadi cha sita, kimelezea usafirishaji wa karafuu kavu kutoka sehemu moja kwenda nyengine ni lazima kupata kibali.

Alisema  Shirika linaendelea kushawishi wananchi katika kuuza karafuu zao ZSTC na kuacha kusafirisha kimagendo jambo ambalo ni makosa na linasababisha kupunguza pato la nchi.

Kamanda msaidizi Kamishna wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba, Haji Khamis Haji, akithibitisha kukamatwa kwa magendo ya karafuu hizo alisema, ni kweli askari walifanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao kwa siku tafauti wakiwa katika shughuli zao za doria.

“Kuna karafuu zilikamatwa na wenzetu wa KMKM Konde katika gari aina ya Noha ambapo mtuhumiwa alikimbia, lakini asubuhi walikamatwa na Febuari 8 tulimkamata mtuhumiwa mwenginea kutoka konde kwenda bandari ya Kichungwani Msuka na wote tutafikishwa mahakamani Jumatatu” alisema.


Hivyo aliwataka wananchi na wakulima wote wa zao la Karafuu watumie fursa ya kuuza Karafuu zao ZSTC, ili kulipatia Shirika mapato halali ya nchi na kuacha kusafirisha Karafuu kimagendo pia wananchi kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ili wananchi waache tabia hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.