STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 10.2.2017

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ameeleza haja kwa Mabalozi wanaokwenda kuiwakilisha Tanzania
nchi za nje kutekeleza Sera ya Diplomasia ya Uchumi kwa kuhamasisha uwekezaji hasa
katika sekta ya viwanda ambayo ndio kiu ya uchumi wa Tanzania hivi sasa.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipofanya mazungumzo na Mabalozi Wateule
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, waliofika Ikulu kumuaga Rais pamoja na
kufanya nae mazungumzo ambapo alisisitiza kuwa sekta ya viwanda imepewa kipaumbele na kutiliwa mkazo mkubwa
na Serikali zote mbili.
Miongoni mwa Mabalozi
hao ni Balozi Emmanuel John Nchimbi ambaye anakwenda kuiwakilisha Tanzania
nchini Brazil, Balozi Mbelwa Brighton Kairuki anaekwenda nchini China, Balozi
Geogre Kahema Madafa anaekwenda Italy, Balozi Profesa Elizabeth Kiondo
anakwenda nchini Turkey.
Wengine ni Balozi Dk.
James Alex Msekela UN nchini Geneva, Balozi Samwel William Shelukindo
anaekwenda Paris, France na Balozi mteule Lt. Jeneral (Mstaafu) Paul Ignance
Mella anaekwenda D.R. Congo.
Katika maelezo yake Dk.
Shein alisema kuwa shabaha kuu ya Serikali zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuimarisha sekta ya viwanda
vikiwemo viwanda vikubwa, vidogo na vya kati hivyo ni vyema wakatumua fursa
hiyo kuwakaribisha wawekezaji wa nchi hizo wanazokwenda kufanyia kazi.
Akizungumzia kwa
upande wa Zanzibar, Dk. Shein alisema kuwa licha ya Zanzibar kuwa ni visiwa
ambavyo vimezungukwa na bahari sambamba na kuwepo ukanda wa bahari kutoka Tanga
hadi Mtwara lakini maeneo hayo hakuna viwanda vya samaki ambayo ni bidhaa
inayotokana na bahari.
Alieleza kuwa eneo la
bahari la Zanzibar ni maarufu sana kwa samaki aina ya jodari ambaye ni samaki anaependwa
duniani lakini wamekuwa hawavuliwi ipasavyo na badala yake hutokea meli kubwa za
kigeni za uvuvi ambazo huja kuwavua kwa njia za wizi.
Dk. Shein alieleza
kuwa hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha sekta ya ajira na
kupunguza changamoto iliyopo katika sekta hiyo hapa nchini hasa kwa vijana.
Aidha, Dk. Shein
alieleza haja ya Mabalozi hao kuitangaza Zanzibar na Tanzania nzima kiutalii
ambapo kwa upande wa Zanzibar sekta hiyo imekuwa ni muhimu kutokana na
kuchangia asilimia 80 ya pato la Taifa.
Dk. Shein alieleza
kuwa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ifikapo mwaka 2020 ni kupokea
watalii zaidi ya laki tano kutokana na mikakati iliyopo hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar
inavivutio vingi vya kitalii.
Pia, Dk. Shein alisisitiza
haja ya kuvitangaza vivutio vya kitalii vilivyopo nchini vikiwemo Mbuga za wanyama,
sehemu za kihistoria, fukwe na vyenginevyo.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein aliwatakia heri na fanaka Mabalozi hao katika utendaji wao wa kazi kwenye Balozi hizo na kueleza kuwa kwa
vile anatambua utendaji wao wa kazi ana matumaini makubwa kuwa watatekeleza
vyema dhamana zao hizo.
Nao Mabalozi hao
walimthibitishia Dk. Shein kuwa
wamepokea maelekezo yote aliyowapa na kuahidi kuyafanyia kazi hasa kwa maeneo
maaluma ya Zanzibar na Tanzania Bara.
Akitoa maelezo kwa
niaba ya Mabalozi wenziwe, Balozi wa Tanzania nchini Brazil Balozi Emmanuel
John Nchimbi, alimuhakikishia Dk. Shein kuwa watafanya kazi kwa juhudi kubwa na
maarifa kwa maslahi ya nchi yao na wananchi wake.
Balozi Nchimbi kwa
niaba ya wenziwe walitoa pongezi na shukurani kwa kwa Rais Dk. Shein pamoja na
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli kwa kuteuliwa
kwenda kuiwakilisha Tanzania katika nchi hizo.
Mabalozi hao walimuhakikishia
Dk. Shein kuwa katika wadhifa wao huo juhudi za makusudi watazichukua kwa
mashirikiano ya pamoja katika kuhakikisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati
ya nchi hizo na Tanzania unaimarishwa zaidi sambamba na kuimarisha maslahi kwa
pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment