Habari za Punde

Rais Dk Shein akutana na Balozi wa Urusi nchini

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na Balozi wa Shirikisho la Urusi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe,Yuri Fedorovich Popov alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa mazungumzo na Rais leo asubuhi,[Picha na Ikulu.] 23 /02/2017.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na mgeni wake  Balozi wa Shirikisho la Urusi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe,Yuri  Fedorovich Popov  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo asubuhi,[Picha na Ikulu.] 23 /02/2017.

 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                  23.2.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  ameeleza kuwa kuimarika zaidi kwa uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Urusi na Zanzibar kutazidisha juhudi za kukuza uchumi hasa katika sekta ya utalii ambayo Zanzibar imepiga hatua.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa Urusi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Yuri Fedorovich Popov ambapo katika mazungumzo hayo balozi huyo alimuahidi Dk. Shein kuwa Urusi itazidisha uhusiano na ushirikiano kati yake na Zanzibar.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa ipo haja ya kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano huo uliopo kati ya nchi hizo kwa kutambua kuwa thamani yake ni kubwa katika maendeleo kwa pande zote mbili.

Dk. Shein alisema kuwa Urusi ni nchi moja wapo inayotoa watalii wengi duniani ambao sio wengi wanaozitembelea nchi za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania, hivyo alisisitiza haja ya mashirikiano ya pamoja kati ya pande mbili hizo katika kuifanyia kazi sekta hiyo ambayo nimuhimukatika kukuza uchumi na maendeleo hapa nchini.

Dk. Shein aliongeza kuwa kurejea huduma za usafiri wa ndege kati ya Tanzania na Urusi kama ilivyokuwa hapo siku za nyuma kupitia Shirika lake la ndege la “Aeroflot”,    kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuikamarisha sekta ya utalii hapa nchini kwani itasaidia kuleta watalii kutoka nchi hiyo moja kwa moja.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo haja ya kuendeleza na kuongeza nafasi za masomo kwa vijana wa Zanzibar wanaokwenda nchi hiyo kwa ajili ya kusoma katika kada mbali mbali za elimu ya juu.

Akizungumzia kuhusu sekta ya biashara, Dk. Shein alisema kuwa Tanzania ikiwemo Zanzibar ina historia kubwa katika sekta ya biashara kati yake na Urusi hivyo ipo haja kwa hatua hiyo kurejeshwa kama ilivyokuwa siku za nyuma.

Aidha, Dk. Shein aliipongeza Serikali ya Urusi kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa karibu kati yake na Zanzibar na kueleza kuwa nchi hiyo ni miongoni mwa nchi za mwanzo kufungua Ubalozi wake hapa Zanzibar mara tu baada ya Mapinduzi ya Januari 12, mwaka 1964.

Hivyo, Dk. Shein aliitilia mkazo rai ya Balozi Yuri Popov ya kuimarisha uhusiano kama ilivyokuwa katika miaka ya 1970 na 1980 ambapo Urusi iliimarisha zaidi uhusiano huo na Tanzania ikiwemo Zanzibar kwani pia, nchi hiyo ni miongoni mwa nchi za mwanzo kuyatambua Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Nae Balozi wa Urusi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Yuri Fedorovich Popov alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Urusi itaendelea kushirikiana na kuiunga mkono Zanzibar kwa kutambua uhusiano na ushirikiano mwema wa kihistoria uliopo.

Katika maelezo yake, Balozi Yuri alieleza kuwa Urusi inatambua umuhimu wa kuimarisha uhusiano na ushirikiano huo ambao utakuza maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa pande zote mbili.

Kwa upande wa sekta ya utalii, Balozi Popov alieleza kuwa juhudi za makusudi zitachukuliwa katika kuhakikisha usafiri wa ndege kati ya Urusi na Tanzania utarejeshwa ili kukuza sekta hiyo ya utalii pamoja na sekta ya biashara na shughuli za uwekezaji.

Alieleza kuwa kwa upande wa sekta nyengine za maendeleo nchi yake itaongeza nguvu zaidi katika kuhakikisha mafanikio zaidi yanapatikana katika sekta hizo ili kuimarisha uchumi na maendeleo kwa nchi mbili hizo.

Pamoja na hayo, Balozi Popov alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kipindi cha Pili pamoja na kuwapongeza wananchi wa Zanzibar huku akiahidi kuwa wananchi wa Urusi wataendeleza ushirikiano na ndugu zao wa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.