Habari za Punde

Balozi Seif Aendelea na Ziara Yake Nchini India



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiwasha mshumaha mara baada ya kuwasili Makao Makuu ya Kampuni ya Ujenzi wa Nyumba za Mkopo katika Jimbo la Chennai Nchini India. Kushoto ya Balozi Seif ni Rais wa Jumuiya ya Makampuni ya Nichan Nchini India Bwana Manohar Nichani, Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi Dr.
Sira Ubwa Mambora, Kayibu Mkuu Wizara ya Kilimo Nd. Juma Ali na Kaimu Balozi wa Tanzania Nchini India Balozi Mohamed Hija. Kulia ya Balozi Seif ni Afisa wa Ubalozi wa Tanzania Nchini India Bibi Haika Msuya na  Mwakilishi wa Taasisi ya Kitaifa ya mpango wa kilimo kinachotumia mbolea za Asili India Bwana Satyajit Kittur Mjini Chennai.
Balozi Seif Ali Iddi Kushoto akizungumza na Mwakilishi wa Taasisi ya Kitaifa ya mpango wa kilimo kinachotumiambolea za Asili India Bwana Satyajit Kittur Makao Makuu ya Kampuni ya Ujenzi ya Nchini India Mjini Chenna
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiagana na Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali ya Kimataifa ya Miot Dr. Malika Mohandazaz kwenye Hotelli ya Crowne Plaza Mjini Chennai kabla ya kurejea Mjini New Delhi.

Mke wa Makamu wa Pili wa Raios wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi akibadilishana mawazo nammoja wa Viongozi Wandamizi wa Hospitali ya Miot Mjini Chennai kabla ya Kuelekea Mjini New Delhi. Picha na – OMPR – ZNZ.



Na Othman Khamis OMPR.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Zanzibar inakusudia kubadilisha muundo wa ujenzi wa nyumba zake za makazi na Ofisi za Serikali ili kujaribu kukabiliana na uhaba wa maeneo ya ardhi unaovikabili Visiwa vya Zanzibar.

Balozi Seif  alitoa Kauli hiyo wakati wa mazungumzo yake na Uongozi wa Kampuni ya Ujenzi wa Nyumba za Mikopo ya Jimbo la Chennai ya TVH katika Jengo la Ofisi hizo liliopo Mjini Chennai Nchini India.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikizisisitiza Taasisi zake za Umma, zile Binafsi  pamoja na watu wenye uwezo kufikiria muelekeo wa Utamaduni wa kujenga majengo ya ghorofa ambayo mbali ya kubadilisha mandhari ya Miji mipya,  lakini pia yatakidhi mahitaji ya upatikanaji wa nyumba katika eneo dogo.

Balozi Seif  alisema Zanzibar bado inahitaji kuwa na majengo ya Kisasa yanayokwenda  na wakati. Hivyo aliushauri Uongozi wa Kampuni hiyo ya ujenzi ya TVH ya India kuangalia uwezekano wa kutumia fursa zilizopo Zanzibar  katika mpango wa uwekezaji katika Sekta ya Makaazi.

Hata hivyo Balozi Seif alisema endapo Kampuni hiyo itafikia maamuzi ya kuanzisha Miradi yao Zanzibar ni vyema wakaangalia njia ya Ujenzi wa Nyumba kwa kutumia Teknojia isiyohitaji Mchanga kwa vile Rasilmali hiyo hivi sasa imepungua kwa kiasi kikubwa.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikutana  kwa mazungumzo na Mwakilishi wa Taasisi ya Kitaifa ya mpango wa kilimo kinachotumia mbolea za Asili India Bwana Satyajit Kittur Mjini Chennai.

Katika Mazungumzo yao Bwana Satyajit Kittur alisema India imefanikiwa vyema katika kuimarisha Kilimo hicho na kupata heshima na tuzo mbali mbali za Kimataifa.

Alisema zipo jitihada zinazochukuliwa na Taasisi hiyo katika muelekeo wake wa kushirikiana na Mataifa mbali mbali zikiiwemo nchi za Bara la Afrika zenye kutegemea uchumi wake katika Sekta ya Kilimo.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo. Maliasili, Mifugo na Uvuvi Zanzibar Nd. Juma Ali Juma alisema Wananchi wengi wa Zanzibar  wamaekuwa wakitegemea Kilimo katika kuendesha maisha yao licha ya utaalamu mdogo wanaoutumia katika sekta hiyo.

Nd. Juma aliuomba Uongozi wa Taasisi hiyo ya Kitaifa ya mpango wa kilimo kinachotumia mbolea za Asili India kufanya ziara maalum Zanzibar ili kujionea hali halisi ya Wakulima hao na namna watakavyoweza kusaidia Taaluma ya kuendesha kilimo kinachozingatia tija.

Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar B alozi Seif Ali Iddi alisema Zanzibar iko tayari kushirikiana na Taasisi hiyo katika muelekeo wa kuwakomboa Wakulima wake  ambao  wengi kati yao bado wanaendesha kilimo kwa kutumia njia za asili.

Balozi Seif alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi iko tayari kutoa kila msaada kwa Wataalamu wa Taasisi hiyo watakaoshawishika kufika Zanzibar kuangalia mazingira halisi ya uendeshaji wa Sekta ya Kilimo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.