Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Shein, Azungumza na Ujumbe wa Kampuni ya "ENGINEERING CUNSULTANTS GROUPS"-ECG

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akisalimiana na mgeni wake  Mwenyekiti wa Kampuni ya "Engineering Consultants Groups"-ECG  Bw.Amr Hassan Allouba  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo na ujumbe wake. 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akizungumza na mgeni wake  Mwenyekiti wa Kampuni ya "Engineering Consultants Groups"-ECG  Bw.Amr Hassan Allouba  yaliyofanyika Ikulu Mjini Zanzibar leo
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akifuatana na Mwenyekiti wa Kampuni ya "Engineering Consultants Groups"-ECG  Bw.Amr Hassan Allouba (katikati) baada ya mazungumzo yao yaliyofanyika Ikulu Mjini Zanzibar leo,(kushoto) Balozi wa Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania Nchini Misri Balozi Mohamed Haji Hamza.
 [Picha na Ikulu.]24/04/2017. 


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                               24.04.2017
---
AZMA ya Kampuni ya ‘Engineering Consultants Group’ kutoka Misri ya kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sekta ya ujenzi wa miji mipya ya kisasa inayotumia teknolojia mpya katika kurahisisha maisha ya wakaazi wake ‘Smart City’ itasaidia kufikia lengo la ujenzi wa miji hiyo inayokusudiwa kujengwa hapa Zanzibar sambamba na kuimarisha sekta ya uwekezaji.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Mwenyekiti wa Kampuni ya ‘Engineering Consultants Group’ Mhandisi Amr Hassan Allouba, Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake, Dk. Shein aliyasema  kuwa katika kuimarisha utekelezaji wa Mipango miji,  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika jitihada za makusudi za kuhakikisha inashirikiana na Kampuni mbali mbali za ndani na nje ya nchi katika ujenzi wa miji ya kisasa hapa Zanzibar.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa azma ya Serikali ni kuufanya Mji wa Zanzibar kupiga hatua kubwa zaidi za kimaendeleo  katika maamuzi ya ziada ya kufanya kitovu cha Mji (Ngambo) kuwa ni ‘Smart City’ ambayo ni nadharia mpya yenye lengo la kufanya miji iwe sio tu mizuri ya kileo na endelevu bali hutumia utaalamu na teknolojia mpya.

Dk. Shein alisema kuwa kujitokeza kwa Kampuni hiyo na kuonesha azma ya kutaka kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sekta hiyo ni jambo la faraja hali ambayo inatoa nafasi kwa Zanzibar kuzidi kujiwekea mazingira mazuri katika utekelezaji wa azma hiyo sambamba na kujipanga vyema kiuwekezaji.

Rais Dk. Shein alimueleza Mwenyekiti huyo wa Kampuni ya ECG yenye Makao Makuu yake mjini Cairo, Misri kuwa tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshatenga maeneo huru ya uwekezaji Fumba kwa upande wa Unguja na Micheweni kwa upande wa Pemba na katika maeneo yote hayo Serikali inaendelea kutoa fursa kwa wawekezaji kuekeza katika sekta mbali mbali za maendeleo.

Aliongeza kuwa Zanzibar iko tayari kushirikiana na Kampuni hiyo kwani itapata mengi ya kujifunza kutokana na uzoefu mkubwa ulionao na kusisitiza kuwa  ujenzi wa miji mipya ya kisasa inahitajika hasa ikizingatiwa kuwa maendeleo na teknolojia yamezidi kuimarika duniani kote ambapo kampuni hiyo nayo iko katika hatua hiyo.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Mwenyekiti huyo alieongozana na  kiongozi wa Kampuni hiyo kwa upande wa nchi za Bara la Afrika Sherif Mourad wakiwa na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Misri, Balozi Mohammed Hamza kuwa Zanzibar ina uhusiano na ushirikiano mwema na wakihistoria kati yake na Misri.

Aliongeza kuwa Misri ni miongoni mwa nchi za mwanzo zilizoanzisha uhusiano wa kidiplomasia kati yake na Zanzibar mara tu baada ya Mapinduzi Matkukufu ya Januari 12, 1964 hatua ambayo ilipelekea mashirikiano mazuri yaliopelekea kukuza uhusiano na ushirikiana katika sekta ya elimu, afya na nyenginezo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa wanafunzi walio wengi wa Zanzibar walipata fursa ya kusoma nchini Misri hasa katika Chuo Kikuu cha Al-Azhar na vyuo vyenginevyo na wengine kupata fursa ya kusomea udaktari na fani nyengine zikiwemo za elimu ya dini ya Kiislamu, habari na nyenginezo.

Nae Mwenyekiti wa Kampuni ya ‘Engineering Consultants Group’ Mhandisi Amr Hassan Allouba alimueleza Dk. Shein azma ya Kampuni hiyo kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha miji mipya ya kisasa ambayo inaendana na teknolojia ya kisasa  ambayo itaiwezesha Zanzibar kuimarika kiuchumi, kibiashara na  utoaji huduma kwa jamii.

Mhandisi Allouba alimuelezea Dk. Shein uzoefu wa kazi za Kampuni hiyo ndani na nje ya Misri pamoja na mafanikio iliyoyapata na kueleza kuwa Kamupuni yake iko tayari kuleta neema hiyo kwa Zanzibar ili kuwasaidia wananchi pamoja na Serikali yao katika kukuza uchumi wake na kuimarisha maendeleo.

Alieleza kuwa miradi hiyo kwa uzoefu wake imekuwa ni kichocheo kikubwa cha ajira hali ambayo imepelekea kuimarika kwa soko la ajira katika maeneo yote ambayo tayari wameshaitekeleza.

Alisema kuwa mbali ya kuimarika kwa ajira pia, hatua hiyo itasaidia katika kuifanya Zanzibar iimarike na iwe mbele katika sekta ya teknolojia ya kisasa kutokana na uzoefu walionao katika miradi hiyo.

Hivyo, Mwenyekiti huyo amemuhakikishia Dk. Shein kuwa Kampuni yake iko tayari kuimarisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Misri na Zanzibar kwa kuja kuekeza Zanzibar kwani ni pande mbili zenye uhusiano na udugu wa kihistoria, hivyo hatua hiyo itapanua wigo wa maendeleo kwa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.