Habari za Punde

Vijana jimbo la Uzini watakiwa kuimarisha michezo


   
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                   29.04.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka vijana wa Jimbo la Uzini kuimarisha michezo kwa lengo la kuwaunganisha na kujenga udugu na umoja miongoni mwao na viongozi wao wa chama na Serikali wataendelea kuwaunga mkono.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Skuli ya Dunga, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja,  katika hafla ya kukabidhi vifaa vya michezo kwa timu 46 za Jimbo la Uzini Mohammed Raza vilivyotolewa na Mwakilishi wa Jimbo hilo ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa chama na Serikali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa michezo ndio inayowanganisha vijana na hata wazee na kuwa kitu kimoja na kuwasisitiza waendelee kucheza michezo mbali mbali hasa ikizingatiwa kuwa michezo inahistoria kubwa katika kuwanganisha watu kwani ndio iliyowaunganisha Watanzania kupitia vyama vya siasa kikiwemo ASP, TANU na hatimae CCM.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza historia ya michezo  hapa  Zanzibar huku akiwataka  vijana  kuanza  michezo tokea wakiwa skuli kwani michezo ina nafasi kubwa katika elimu na elimu huenda sambamba na michezo.

Dk. Shein alieleza kuwa katika maisha ya mwanaadamu yoyote michezo ina umuhimu,  mkubwa kwani huleta mshikamano hujenga udugu na kujuana na pia, husaidia katika kujenga afya ya akili na kiwiliwili kwa vijana na wazee na watambue kuwa michezo si uhasama.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza umuhimu wa michezo kufuata kanuni na taratibu za kucheza na kuwataka vijana hao kushindana kimichezo na wasijenge uhasama na kupelekea kupambana kwani hilo sio lengo la michezo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwataka vijana hao wa Jimbo la Uzini kuwa wazalendo wa nchi yao, Jimbo lao, wazee wao, viongozi wao huku wakitambua kuwa Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar imefanya mambo mengi ya kimaendeleo ambayo wanapaswa kuyaunga mkono.

Akisisitiza haja ya vijana kuwa wazalendo, Dk. Shein alisema kuwa suala la uzalendo limepungua kwa kiasi kikubwa hapa nchini hivi sasa na kueleza haja ya kuitumia michezo kwani michezo ni uzalendo na kuwataka kuwa wazalendo wa timu zao za nyumbani huku akiwasisitiza kufuata msemo wa Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kuwa “Thamini chako na usahau cha mwenzako’.

Akiwaeleza juu ya ombi lao la kutengenezewa barabara zao za ndani katika Jimbo hilo, Dk. Shein alisema kuwa azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuzitengeneza barabara hizo iko pale pale na kuwaeleza jambo linalochelewesha azma hiyo ni uhaba wa vifaa ambapo tayari serikali ina mpango wa kununua vifaa zaidi vya kutengenezea barabara ukiwemo mtambo mpya wa kupikia lami.

Nae Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mohammed Raza alieleza kuwa mashirikiano ya pamoja kati yake na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na viongozi wa Serikali wa Wilaya na Mkoa ndio yaliopelekea kupata mafanikio hayo.

Aliongeza kuwa yote anayoyafanya kwa Jimbo hilo akiwa ni Mwakilishi wa wananchi wa Jimbo hilo la Uzini ni utekelezaji wa  Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010-2020 ambayo inasisitiza uimarishaji wa sekta ya michezo.

Alieleza kuwa kufanya hivyo ni njia moja wapo ya kuwapa wananchi haki yao ya kuwachagua viongozi ambao huwatumikia katika vyombo vya kutunga sheria sambamba na kuwa na majibu rahisi mbele ya wananchi wakati ukifika wa kuwaomba ridhaa yao ili wakuchague.

Pamoja na hayo, Raza aliwaahidi wanachi wa Jimbo la Uzini wakiwemo vijana kuwa ataendelea kuwatumikia na kusisitiza mashirikiano ya pamoja ambayo ndio ngao kubwa ya maendeleo Jimboni humo huku akiwataka kuendeleza michezo kwa amani na ushirikiano.

Mbali ya mafanikio makubwa yaliopatikana katika Jimbo hilo la Uzini Mwakilishi huyo alieleza changamoto ya miundombinu ya barabara za ndani zilizomo katika Jimbo hilo zikiwemo zile zenye kiwango cha kifusi

Nao wananchi wa Jimbo la Uzini katika risala yao iliyosomwa na Hamad Ali Haji, walimpongeza Dk. Shein kwa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa vitendo na kuahidi kuendelea kumuunga mkono.

Walimuhakikishia kuwa wataendelea kudumisha amani na utulivu na kuuunga mkono uongozi wake pamoja na chama chao cha CCM ambapo pia walitumia fursa hiyo kuyaeleza mambo mbali mbali ya maendeleo waliyofanyiwa na Mwakilishi wao huyo tokea walipompa ridhaa ya kuwaongoza  katika jimbo lao hilo la Uzini.

Miongoni mwa vifaa vilivyotolewa katika hafla hiyo ni pamoja jezi, mipira, viatu, soksi na shinguard ambavyo vyote vina thamani ya Tsh. Milioni 25.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.