Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Awatembelea na Kuwafariji Wananchi Waliopata Janga la Upepo


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                16.05.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewafariji na kuwapa pole wananchi waliopata athari baada ya nyumba zao kuezuka mapaa kufuatia upepo mkali uliotokea hapo jana mnamo majira ya saa tatu asubuhi na kuathiri nyumba zipatazo 123.

Upepo huo, ulitokea katika maeneo ya Nyarugusu, Pangawe, Kinuni, Makondeko na  Shehia ya Mwanakwerekwe na kupelekea nyumba kadhaa kuezeka mapaa.

Akiwa katika eneo hilo mara baada ya kukagua baadhi ya nyumba zilizopata athari, Rais Dk. Shein aliwaeleza wananchi hao kuwa Serikali yao ipo na itachukua kila jitihada katika kuhakikisha inawapa msaada unaostahiki haraka iwezekanavyo.

Dk. Shein aliwapa pole wananchi hao na kuwapongeza kwa ushirikiano wao mkubwa waliouonesha katika kipindi hichi na kueleza kuvutiwa kwake na juhudi zao hizo.

Alisema kuwa yeye mwenyewe binafsi baada ya kupata taarifa hiyo akiwa huko kisiwani Pemba hapo jana ambako alikwenda kuwafariji wananchi waliopata athari za mvua za masika zinazoendelea kunyesha ambazo zimeharibu makaazi ya watu, miundombinu ya barabara, madaraja na mazao kiswani humo, alipatwa na simanzi na majonzi makubwa sana.

Alisisitiza kuwa hiyo yote ni shani yake Mwenyezi Mungu, na mtukuio kama hayo si mara ya kwanza kutokea na yanapotokea huwa hayana taarifa ambapo aliwahimiza wananchi kusaidiana, kustiriana na wale wote wenye uwezo wawasaidia wasio na uwezo huku akieleza kuwa Serikali kwa upande wake ina jukumu la msingi la kuwatendelea mema wananchi wake.

Dk. Shein aliwataka wananchi kutolaumiana kwani hakuna mtu aliyoyatenda na kuwataka wananchi kutowabeza waliopatwa na athari hiyo kwani janga hilo linaweza kumpata mtu yeyote na wakati wowote.

Aidha, Alieleza kuwa mipango ya Serikali ni mizuri lakini inazidiwa kimo na mipango ya Mwenyezi Mungu, hivyo aliwasisitiza wananchi kusaidiana na kuahudi kuwa Serikali kwa upande wake itaongeza nguvu kwani ipo na iko imara na haitochelea kutoa misaada na itawasaidia wale wote waliokuwa hawana uwezo.
Mapema wananchi walioathirika na upepo huo katika maeneo ya Pangawe na Makondeko walimueleza Dk. Shein jinsi upepo huo mkali ulivyoanza na hatimae kuleta athari kubwa katika eneo hilo na namna walivyokabiliana nao huku wakitoa pongeza kwa Dk. Shein kwa kuwajali na kuwathamini kutokana na kitendo chake hicho cha kwenda kuwafariji na kuwapa pole.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza viongozi wa Mkoa, Wilaya, Jimbo, Manispaa na wengineo kwa hatua madhubuti walizozichukua katika kukabiliana na tukio hilo ambalo limeathiri nyumba za wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaandaa utaratibu maalum wa kuhakikisha kila mwenye uwezo akiwa ndani ama nje ya nchi anaweza kuchangia katika maafa yaliyosababishwa na mvua hizi za masika zinazoendelea kwani Serikali haiwezi kufanya mambo yote peke yake.

Alieleza haja ya kuwepo maandalizi katika kukabiliana na matukio kama hayo na kuahidi kwa upande wa Serikali itajiandaa lakini pia aliwataka wananchi nao wajiande kwa kuepuka kufanya vitendo ambavyo vitapelekea kuzidisha athari za mvua zikiwemo ujenzi usio salama.

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohammed pamoja na Uongozi wa Manispaa  Wilaya ya Magharibi B, walimueleza Dk. Shein hatua za awali zilizochukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwapatia chakula wananchi hao walioathirika kwa kila nyumba kupewa kipolo cha mchele wa kilo 25 huku juhudi zikifanywa kufuatia Kamati maalum kuundwa ambayo inafanya kazi na kuahidi kutoa taarifa ndani ya masaa 24. 

Mkuu wa Mkoa huyo alieleza kuwa nyumba zilizoathirika idadi yake ni 123 ambapo 96 ni za Shehia ya Kinuni, 26 Shehia ya Mwanakwerekwe na nyumba moja ni ya Shehia ya Pangawe.

Nae Mbunge wa Jimbo la Pangawe Shamsi Vuai Nahodha kwa niaba ya wananchi wa Jimbo hilo na Majimbo ya jirani yaliyoathirika walieleza kufarajika kwao kwa ziara hiyo ya Dk. Shein ya kwenda kuwaona na kuwapa pole.

Alieleza kuwa kutokana na wananchi hao kupita katika kipindi kigumu sana katika msimu huu wa mvua za masika,  Mbunge huyo alisema kuwa Serikali imeonesha juhudi kubwa katika kuwasaidia wananchi ambapo viongozi wa siasa nao kwa upande wao wamekuwa wakiwaunga mkono na kuwafariji pamoja na kuwasaidia huku akisifu moyo waliouonesha wananchi hao katika kipindi hichi na kuwataka waendelee nao.

Akitoa neno la shukurani kwa Rais, Mwakilishi wa Jimbo la Pangawe ambaye pia, ni Naibu Waziri, Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Khamis Juma Maalim alisema kuwa ujio wa viongozi wa Serikali akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein umewapa faraja kubwa wananchi wa maeneo hayo ambao wameathirika na upepo huo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar


Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.