Habari za Punde

BOT yatoa waraka kwa wafanyabiashara wa maduka ya kuuza na kununua fedha za kigeni

Leseni mpya kutolewa

Mfanyabiashara kumiliki duka moja tu

BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imetoa waraka kwa wafanyabiashara wa maduka ya kuuza na kununua fedha za kigeni kuomba upya leseni kwa ajili ya kufanya biashara hiyo. Leseni zote za maduka ya kubadilisha fedha za kigeni zitafutwa ifikapo Septemba 2, mwaka huu ili wamiliki waombe upya.

Hayo yalisemwa jana na Ofisa Msimamizi Maduka ya Kuuza na Kununua Fedha za Kigeni wa Benki Kuu ya Tanzania, Kanuti Mosha kwenye Maonesho ya 41 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF) yanayoendelea kwenye Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Barabara ya Kilwa, Temeke jijini Dar es Salaam.

Mosha alisema kwa sheria ya sasa, mfanyabiashara atatakiwa kumiliki duka moja tu tofauti na ilivyokuwa awali mtu mmoja anaweza kumiliki maduka hata matano. Alisema sambamba na kutoa leseni upya, BoT imeweka viwango vipya vya mtaji ambavyo vinaanzia Sh milioni 100 hadi 300 kwa daraja A, na kuanzia Sh milioni 250 hadi Sh bilioni moja kwa daraja B na Amana ya Thamani kuanzia Dola za Marekani milioni 50 hadi milioni 100.

Aidha, alisema wafanyabiashara wa Daraja B watafanya miamala ya papo kwa hapo pamoja na miamala ya nje ya nchi. Hata hivyo, Mosha alisema mbali na masharti ya mtaji, watahitajika pia kufunga kamera tatu ‘CCTV‘ kwa ajili ya usalama.

Alieleza kuwa lengo ni kudhibiti ubadilishaji wa fedha na utoaji wa stakabadhi, kamera zinatakiwa kufungwa kaunta, kwenye kabati la kuhifadhia fedha na eneo la kuhudumia wateja.

Alisema watakaokamilisha masharti hayo ndio watakuwa wanaendesha biashara hiyo kuanzia Septemba mwaka huu Wafanyabiashara hao wa maduka ya kubadilisha fedha za kigeni wamepewa miezi mitatu kuanzia Juni 2, 2017 hadi Septemba mosi, mwaka huu wakamilishe usajili na kumiliki duka moja tu. Mosha alisema endapo mfanyabiashara atataka kufungua tawi, itamlazimu kutuma maombi BoT.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.