Habari za Punde

Maadili ya Kazi na Uwajibikaji ni Muarobaini wa Utendajikazi Uliotukuka - Kamishna Sururu



Kamishna wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar , Johari Masoud Sururu alipokuwa akizungumza na  watumishi wa Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja  alipofanya ziara ya kikazi Mkoani humo tarehe 21 – 22 Novemba, 2017.


Kamishna wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar, Johari Masoud Sururu, amewataka watumishi wa Uhamiaji Zanzibar kufanyakazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu sambamba na Maadili ya Kazi. Aliyasema hayo wakati akizungumza na watumishi wa Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja  alipofanya ziara ya kikazi Mkoani humo tarehe 21 – 22 Novemba, 2017.

Aidha, katika kuhakikisha kuwa Wananchi wanapata huduma bora na stahiki toka Idara yake, aliwaasa Watumishi kuacha tabia ya kufanyakazi kwa mazowea na kuhakikisha kwamba kila siku wanafanyakazi kwa juhudi, maarifa na uweledi wa hali ya juu.

Kamishna Sururu, alitumia fursa hiyo kuwasisitiza watumishi wa Uhamiaji Mkoani humo,  kusimamia vyema majukumu yao kwa mujibu ya Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo. “Nawasihi na kuwataka muelewe kuwa sisi tumepewa dhamana na Serikali kuwatumikia wananchi, hivyo nidhamu na heshima ya kazi ndio msingi wa mafanikio katika utekelezaji wa majukumu yetu”. Ni vyema kila mtumishi kwa nafasi yake atambue wajibu wake na muda wote tuzingatie maadili ya kazi, nidhamu na uwajibikaji”. “Tuache kufanya kazi kwa mazowea na tutoe huduma bila ya upendeleo wa aina yoyote” “Narudia hizi ni nasaha zangu kwenu, kila mmoja ajitambue na kujua wajibu wake, toeni huduma bila ya upendeleo, tutumie lugha nzuri na za heshima muda wote” alisema Kamishna Sururu.

Kwa upande wa watumishi hao, waliahidi kutekeleza maagizo na maelekezo yaliyotolewa na Kamishna Sururu kwa vitendo. Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Mkemimi Mohamed Mhina wakati akitoa taarifa ya utendaji kazi wa Mkoa huo, alisema “Kipaumbele cha Mkoa wetu ni kuondoa malalamiko kutoka kwa Wateja na wananchi kwa ujumla, Mkoa wangu umedhamiria na unatekeleza kwa vitendo dhamira hiyo”

Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja imeboresha Utoaji wa Huduma mbali mbali sambamba na kusimamia vyema udhibiti wa wageni, kwani Mkoa wa Kusini Unguja ni Mkoa wenye miradi takriban 162 ya uwekezaji zikiwemo takriban  Hoteli  na nyumba za kulala wageni. “Pamoja na changamoto ya uwepo wa Bandari Bubu zipatazo ishirini na nne (24) na madiko ishirini (20), Udhibiti tunaofanya, Misako na Doria vimesaidia katika kuongeza ukusanyaji wa maduhuli ya serikali, kwa kipindi cha mwezi Mei – Oktoba, 2017 tumefanikiwa kukusanya Dola za Kimarekani 17,500 USD na  Shilingi 13,710,000/=” alisema “Naibu Kamishna Mkemimi.

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, akihitimisha ziara yake Ofisini hapo, alisema “Nimefarijika sana kuona kwamba suala la ukusanyaji wa mapato linapewa uzito unaostahiki. Tunaelewa Serikali zote mbili zinahimiza ukusanyaji wa maduhuli ili Serikali ziweze kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi wake na kuwaletea maendeleo wanayotarajia. Dhamira hiyo haitofikiwa ikiwa sisi watumishi tutafanya uzembe unaosababisha uvujaji wa maduhuli ya serikali na ubadhirifu wa fedha kwa kufanya matumizi yasiyo ya lazima”.

Aidha, Kamishna Sururu, katika ziara hiyo alipata nafasi ya kutembelea maeneo kadhaa yaliyopo Wilaya ya Kusini na Wilaya ya Kati na kushuhudia Viwanja vilivyotengwa kwa ajili ya miradi ya uendelezaji Majengo ya Ofisi na Makaazi ya Askari wa Uhamiaji Mkoani humo.
Idara ya Uhamiaji pamoja na juhudi hizo zinazolenga kuboresha utoaji wa Huduma zake kwa Jamii na Wageni kutoka Mataifa mbali mbali duniani, imelipa kipaumbele suala la kuboresha Makaazi ya Askari wake, Vitendea kazi sambmba na kuweka mifumo ya kisasa ya kielektroniki ambayo imekuwa nyenzo kubwa katika utoaji wa huduma unaozingatia viwango vya Kimataifa.

 “Idara yetu imekuwa na hadhi kubwa katika medani za Kimataifa, kwa kutumia mifumo ya teknolojia ya kisasa, tumeweza kusimamia na kudhibiti Uingiaji, Ukaaji na Utokaji holela wa watu katika mipaka yetu. Hii ni hatua ya kujivunia sana kwetu na kwa serikali zetu zote mbili” alisema Kamishna Sururu.


Imetolewa na: KITENGO CHA UHUSIANO, AFISI KUU YA UHAMIAJI ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.