Habari za Punde

Mbunge wa Jimbo la Mtama Mhe. Nape Afunguka Akimnadi Dkt. Ndumbaro Na Kusema Kamwe Hatahama CCM.

Nape akibadilishana mawazo na Dk. Ndumbaro
Na Gideon Mwakanosya-Songea


MBUNGE wa jimbo la Mtama mkoa wa Lindi Nape Nnauye amefunguka kwa kudai kuwa hawezi kukihama chama cha mapinduzi (CCM) kama baadhi ya watu wakiwemo wa vyama vya upinzani  kwa kile alichodai kuwa  magari ya upinzani yanaenda kuzama na hayajulikani yataibuka lini.
Uwazi huo ameuweka jana wakati akimnadi mgombea ubunge wa jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma kwa tiketi ya CCM Dk, Damas Ndumbaro kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika katika viwanja vya bombambili Manispaa ya Songea.
Nnauye ambaye aliwahi kuwa katibu wa hitikadi na uenezi CCM taifa na Waziri wa Habari, Michezo na Sanaa katika serikali ya awamu ya tano alisema kuwa kama kuna watu walidhani atakihama chama cha mapinduzi (CCM) na kwenda upinzani wasahau kabisa .
Akizungumza kwa kujiamini huku akishangiliwa na mamia ya wakazi wa bombambili alisema kuwa kama kuna kuwa na matatizo ndani ya CCM tunaonyana ndani ya chama na kuyamaliza na siyo kuhama chama.
“Naikubali serikali ya awamu ya tano inayongonzwa na jemedali Dk. John Magufuli pamoja na makamu wa Rais na waziri mkuu wake kuwa ipo imara na mimi naapa kufia CCM na siyo vinginevyo” alisema Nape Nnauye.
“Nasikia maneno maneno kutoka kwa baadhi ya watu wakisema Nape anataka kuhamia upinzani jambo ambalo siyo la kweli kuanzia leo watu hao waondokane na mawazo hayo” alisema mbunge wa Mtama Nape Nnauye.
Katika kampeni hizo ambazo uchaguzi wake utafanyika Januari 13 mwaka huu Nape Nnauye na Moses Machali aliyewahi kuwa mbunge wa jimbo la Kasulu mkoa wa Kigoma kwa tiketi ya NCCR Mageuzi wamekuwa kivutio kikubwa kwa wakazi wa jimbo la Songea hasa wanapokuwa majukwani.
  MWISHO.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.