Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Akizungumza na Mtukufu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, Mrithi wa Mtawala wa Abu Dhabi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi wa Nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE)

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Mtukufu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, Mrithi wa Mtawala wa Abu Dhabi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi vya (UAE)wakiwa katika ukumbi wa makadhi ya Kiongozi huyo Nchini Abu Dhabi

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amefanya mazungumzo na Mtukufu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, Mrithi wa Mtawala wa Abu Dhabi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi wa Nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) ambapo viongozi hao wamekubaliana kuendeleza uhusiano na ushirikiano kati ya pande mbili hizo hasa katika sekta za maendeleo zikiwemo za kijamii na kiuchumi.

Viongozi hao walifanya mazungumzo hayo katika ukumbi wa Makaazi ya Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, mjini Abu Dhabi, mazungumzo yaliyohudhuriwa na viongozi mbali mbali wa ngazi za juu wa Abu Dhabi wakiwemo Mawaziri, Spika wa Abudhabi pamoja na viongozi wengine wa ukoo wa Sheikh ZaUAE pamoja na wageni waalikwa.

Katika mazungumzo hayo viongozi hao walikubaliana kwa pamoja kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kidugu na kihistoria uliopo kwa muda wa miaka 44 hivi sasa hatua ambayo imeleta manufaa makubwa kwa pande zote mbili.

Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, kwa upande wake alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Abu Dhabi itaendelea kuiunga mkono Zanzibar na iko tayari kutoa ushirikiano wake katika kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo za kiuchumi na kijamii.

Aidha, Sheikh Mohammed, alieleza kuwa Abu Dhabi inathamini sana uhusiano na ushirikiano huo na iko tayari kuunga mkono vipaumbele vyote vilivyowekwa na Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo.

Pamoja na hayo, Kiongozi huyo alimpongeza Dk. Shein kutokana na juhudi zake za kuendelea kuiongoza vyema Zanzibar na kusisitiza kuwa kutokana na juhudi hizo kuna kila sababu za yeye kumuunga mkono ili wananchi wa Zanzibar wazidi kupata maendeleo endelevu.

Aidha, Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan alimuhakikishia Dk. Shein kuwa uongozi wa Taifa hiyo unaona fahari kuwa na mashirikiano na uhusiano na ndugu zao Zanzibar na kueleza kuwa Abu Dhabi itahakikisha inaukuza na kuuendeleza uhusiano na ushirikiano huo ambao anaamini utakuwa na tija kubwa kwa pande zote mbili.

Kwa upande wake Dk. Shein, alitumia fursa hiyo kumpongeza na kumshukurani  Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, kwa mualiko wake aliompa nchini humo pamoja na mapokezi makubwa aliyoyapata yeye na ujumbe wake na kueleza kuwa ziara hiyo ni kichocheo kikubwa cha mashirikiano kati ya Zanzibar na Abu Dhabi.

Dk. Shein, alimuhakikishia Sheikh Mohammed kuwa Zanzibar imepata matumaini makubwa kutokana na hatua za kiongozi huyo za kuahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar ili izidi kupata manufaa katika sekta zake za maendeleo zikiwemo za kiuchumi na kijamii.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa ziara hiyo ni kielelezo cha urafiki, heshima na udugu baina ya Tanzania ikiwemo Zanzibar na Abu Dhabi pamoja na wananchi wake wote ambapo pia, itasaidia sana kukuza uhusiano na kuibua maeneo mapya ya ushirikiano.

Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka kwa ndugu zao wa Abu 
Dhabi hasa ikizingatiwa kuwa nchi hiyo imepiga hatua kubwa katika sekta zote za kiuchumi, kijamii na nyenginezo.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein alifanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Abu Dhabi katika ukumbi wa Hoteli ya Kimataifa ya “Jumeirah Etihad Towers” mjini Abu Dhabi ambapo katika mazungumzo hayo Mkurugenzi huyo alimueleza Dk. Shein azma ya Mfuko huo katika kuiunga mkono Zanzibar.

Katika maelezo yake, Mkurugenzi huyo alieleza kuwa Mfuko huo uko tayari kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo ikiwemo miundombinu pamoja na miradi mengine ya kijamii na kiuchumi.

Nae Dk. Shein kwa upande wake aliupongeza Mfuko huo kwa kuonesha kuwa tayari kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi yake ya maendeleo huku akieleza historia ya Mfuko huo katika kuiunga mkono Zanzibar.

Mapema Dk. Shein akiwa na ujumbe wake akiwemo Mama Mwanamwema Shein, alitembelea Mji mpya wa kisasa wa Masdar unaoendelea kujengwa kwa dhamira ya kuufanya kuwa ni mji wa kipekee duniani unaotumia nishati mbadala hasa umeme wa jua katika shuhuli zake zote zinazohitaji nishati.

Akiwa katika mji huo ulioko umbali wa kilomita 17 kutoka mjini Abu Dhabi, Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa uongozi wa Mradi huo Mkurugenzi Mkuu Yousef Baselaib na Meneja Msaidizi wa Mradi huo Fatma Al Shaigy walimueleza dhamira ya ujenzi huo ikiwa ni pamoja na kuendeleza miji inayoweka uhifadhi wa mazingira kwa kutumia nishati mbadala duniani na kumtajia nchi ambazo tayari zimeanza kufaidika na teknolojia hiyo kupitia taasisi yao.

Pia, alitembelea Msikiti Mkuu wa Abudhabi ambao unajulikana kwa jina maarufu la “Sheikh Zayed Grand Mosque” na kusali sala ya Adhuhuri, ambapo Dk. Shein akiwa katika msikiti huo alidhuru kaburi la Baba wa Taifa hilo na muwasisi wa Muungano wa nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) Marehemu Sheikh Zayed bin Sultan Al Nahyan, na kumuombea dua.

Kwa mujibu wa maelezo ya uongozi wa msikiti huo, ulieleza kuwa msikiti huo uloianza kujengwa mnamo mwaka 1996 hadi 2007 msingi wake uliwekwa na Marehemu Sheikh Zayed akiwa na lengo la kuanzisha sehemu maalum ambayo itakuwa kiungo cha kuwaunganisha Waislamu wa Madhehebu mbali mbali duniani, ambapo msikiti huo una uwezo wa kusali watu 40,000 kwa wakati mmoja.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.