Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar(SUZA) Dk. Ali Mohamed Shein, akiwahutubia na kutowa nasaha zake kwa Wahitimu wa SUZA wakati wa hafla hiyo ya Mahafali ya 13, yaliofanyika katika Ukumbi Mpya wa Chuo hicho uliofunguliwa leo na kuita Dk. Ali Mohamed Shein Hall Tunguu.(SUZA)
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa
Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Amali pamoja na Tume ya Mipango kufahamu mahitaji ya Serikali kwa
kila fani kwa kila mwaka.
Kwa kufanya hivyo,
Serikali itafahamu idadi halisi ya wanafunzi wanaohitajika na kuweza kujua
namna ya kuwaajiri vijana, vyenginevyo wakifundishwa vijana bila ya mpango
Serikali itajikuta ina idadi kubwa ya wahitimu bila ya ajira.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika Mahafali ya Kumi na Tatu ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar
(SUZA), huko katika ukumbi wa Chuo hicho Tunguu, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini
Unguja.
Katika hotuba hiyo,
Dk. Shein alitoa indhari hiyo ili kuepuka kupata matatizo ya kuwa na wasomi
wengi ambao hatimae watakuwa hawana kazi za kufanya, “lazima tuwe na malengo na
mipango madhubuti...tusifanye kwa pupa, kasi wala papara”,alisisitiza.
Aidha, Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kukiagiza Chuo hicho kushirikiana na BAKIZA pamoja na Taasisi mbali
mbali zinazoshughulikia maendeleo ya Kiswahili katika kuimarisha ufundishaji wa
Kiswahili kwa wageni hapa Zanzibar na kukitaka Chuo hicho kujiandaa,
kujitangaza na kujitahidi ili maendeleo yanayotarajiwa yapatikane.
Agizo hilo limekuja
baada ya kuwepo idadi ndogo ya wanafunzi wa kigeni chuoni hapo ambapo idadi
hiyo haitoi picha nzuri kwani inaonesha idadi ya wanafunzi wa kigeni
wanaojiunga inashuka mwaka hadi mwaka badala ya kupanda hasa ikitiliwa maanani
kuwa Zanzibar inategemewa kushika usukani wa kukuza lugha ya Kiswahili.
Hivyo, Dk. Shein
alieeleza kuwa SUZA kupitia Skuli ya Kiswahili na Lugha za Kigeni lazima ifanye
utafiti na kuandaa mikakati itakayosaidia kukiimarisha Kiswahili na kuongeza
idadi iliyopo hivi sasa ya wanafunzi wa nje wanaojiunga na masomo ya Lugha ya
Kiswahili.
Dk. Shein aliwatoa
wasi wasi wanafunzi wote waliofaulu na wanaoendelea kusoma Shahada ya
“Environment Health” kwamba Serikali inashughulikia suala la mafunzo ya mazoezi
yaani “intership” na kuiagiza Kamati ya Wataalamu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Chuo Kikuu cha
Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Wizara ya Afya, ili mazoezi hayo yaanze hivi
karibuni hapa hapa Zanzibar.
Alisisitiza kwamba
hapana hata mwanafunzi mmoja atakaekoseshwa nafasi hio na hapatakuwa na haja ya
wanafunzi kusafiri kwenda sehemu nyengine kwani wamefundishwa Zanzibar na mipango
yao itaandaliwa Zanzibar na yale yanayohitajika katika mazoezi hayo,
yatatekelezwa hapa hapa Zanzibar na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Alieleza kufarajika
kwa kuazishwa fani tatu mwaka huu baada ya kupata vigezo vya Tume ya Vyuo Vikuu
vya Tanzania (TCU), ambazo ni Shahada ya Uzamili ya Sayansi na Tabianchi na
Usimamizi wa Rasilimali, Shahada ya
Uzamili ya Elimu ya Vijana, Jisnia na Maendeleo na Shahada ya kufundisha Lugha
ya Kiswahili kwa Wageni.
Dk. Shein alieleza
kuwa fani zote zinazosomeshwa Chuoni hapo ni muhimu na zimeanzishwa kwa wakati
mzuri hasa katika kuipatia nchi wataalamu wa kuisaidia kukabiliana vyema na
athari za mabadiliko ya tabianchi na kupata wataalamu watakaochochea maendeleo
ya vijana na masuala ya jinsia katika kukabiliana na changamoto zilizopo.
Pamoja na hayo, Dk.
Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza wana “Diaspora” ambao ni wataalamu wa
lugha kwa mapenzi na uzalendo wao kwa nchi yao kwa kumkubalia kuja nchini
kuendesha mafunzo ya Shahada za Juu za Lugha ya Kiswahili katika chuo hicho.
Alieleza kuwa Serikali tayari inakamilisha Sera ya
“Diaspora” na itaanza kutumika, ili iweze kutoa mwongozo ili wana “Diaspora”
washiriki katika maendeleo hapa Zanzibar.
Dk. Shein alisema kuwa
mwaka huu wahitimu wa Shahada ya Usimamizi wa Utalii na Masoko wameanza
kupatikana hatua ambayo ni muhimu katika
kuendeleza dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta
ya utalii.
Hivyo, hali hiyo
itapunguza na hatimae kuondoa tatizo linalolalamikiwa kwa muda mrefu kwamba
vijana wa Zanzibar wanakosa fursa bora za ajira katika mahoteli mbali mbali ya
Kitalii yanayoanzishwa hapa Zanzibar kwa kigezo cha kukosa sifa zinazohitajika.
“Wizara ya Habari,
Utalii, Utamaduni na Michezo italazimika iandae utaratibu, ili wahitimu hawa
waweze kutumika katika kuimarisha sekta ya utalii hapa nchini”,alisisitiza Rais
Dk. Shein.
Rais Dk. Shein,
alikipongeza Chuo cha SUZA, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na
Wizara ya Fedha kwa kutekeleza agizo lake la kujengwa kwa ukumbi huo mpya ambao
kwa mara ya kwanza hivi leo umeanza kazi na kuahidi kuwa utaendelezwa ili uzidi
kukidhi haja. Pia, aliwapongewa wahitimu wote waliomaliza masomo yao leo.
Mapema Rais Dk. Shein
aliuzindua ukumbi mpya wa Chuo hicho ulioitwa jina la Ukumbi wa Dk. Ali Mohamed
Shein na kupata maelezo juu ya hatua za ujenzi wa ukumbi huo.
Pamoja na hilo, Dk.
Shein aliwatunuku wahitimu watano Shahada za Uzamivu za Kiswahili, 21 Shahada
za Uzamili za Kiswahili, Sayansi za Mazingira na Kemia, asilimia 37.6 ya wahitimu
aliwatunuku Shahada za Kwanza, asilimia 46.3 ni wahitimu ngazi za Stashahada na
asilimia 14.2 ni ngazi ya Cheti.
Pia, Rais Dk. Shein
aliwatunuku zawadi wanafunzi bora wa Chuo hicho kwa mwaka huu ambapo mwanafunzi
bora zaidi alikuwa ni Aisha Ali Abdallah ambae ni Mhitimu wa Shahada ya Tehama
na Uhasibu.
Nae Makamu Mkuu wa
Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Profesa Idris Rai alieleza kuwa
ukumbi huo umegharimiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambapo mpaka
uliofikia umeshagharimu shilingi za kitanzania bilioni moja ambao unachukua
watu zaidi ya 300.
Aidha, Profesa Rai,
alieleza kuwa jitihada za kukikuza Chuo zinaonekanwa kupitia ongezeko la
wahitimu wa SUZA ambapo katika Mahafali ya tisa yaliofanyika mwaka 2010, idadi
ya wahitimu wa ilikuwa 320 na mwaka huu imefikia 2099.
Makamu Mkuu huyo
aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa michango yake katika
kukiendeleza Chuo hicho pamoja na Rais Dk. Shein mwenyewe binafsi kwa kuipa
elimu ya Juu kipaumbele inachostahiki.
Kaimu Waziri wa Elimu
na Mafunzo ya Amali ambaye pia, ni Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo alimpongeza
Dk. Shein kwa kuziunganisha Taasisi za Elimu ya Juu za Serikali kuwa sehemu ya
Vitengo vya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar SUZA.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment