Habari za Punde

Mikakati yaandaliwa kudhibiti Taka Mjini Zanzibar

 WAJUMBE wa Manispaa za Mjini, Magharibi A na B, watendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar, Wanasheria na watalamu elekezi kutoka nchini India, wakijadili kanuni mpya inayotarajiwa kutoa muongozo wa udhibiti wa taka katika manispaa tatu za mji wa Zanzibarhizo.

Na Salum Vuai, ZANZIBAR


MABARAZA ya Manispaa ya Mkoa wa Mjini Magharibi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mazingira Zanzibar, wanaandaa mkakati maalumu wa ukusanyaji taka ili kuuweka mji katika usafi wa kudumu.
Mabaraza hayo ni ya manispaa za Mjini pamoja na Magharibi ‘A’ na ‘B’.
Tayari mabaraza hayo yameandaa kanuni ndogondogo zinazolenga kuchukua nafasi ya zile za zamani, ambazo zinatoa miongozo juu ya namna ya kuimarisha usafi kwenye manispaa hizo.
Katika kikao cha kupitia kanuni hizo kilichofanyika mwishoni mwa wiki mjini Zanzibar, wajumbe walitoa maoni mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha kanuni hizo zinatekelezeka.
Awali, akifungua kikao hicho, Sheha Mjaja Juma ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA), alisema kumekuwa na tatizo kubwa la usimamizi wa taka ndani ya manispaa hizo.
Alifahamisha kuwa, tatizo hilo linasababishwa na mambo mbalimbali, ikiwemo kutokuwepo kwa kanuni au sheria ndogo ndogo zinazotoa usimamizi mzuri wa kupunguza tatizo la utupaji taka ovyo.
                                                     
“Baadhi ya watu wanapokwenda kutupa taka hawatumii makontena maalumu yaliyowekwa kwa ajili hiyo, na badala yake huzimwaga ovyo ardhini hata kama kontena halikujaa, na hata katika misingi ya maji ya mvua au machafu na kusababisha kuziba,” alifahamisha.

Mkurugenzi huyo pia alisema kanuni hizo pia zinalenga kuwadhibiti watu waache kutupa taka majiani, kama vile mabaki ya vyakula na matunda, chupa tupu hasa wanapokuwa ndani ya magari.

Kwa hivyo, alisema kuundwa kwa kanuni hizo kunajielekeza katika kutoa majibu ya matatizo hayo, ili manispaa hizo na Zanzibar kwa jumla ziwe mfano bora wa usafi Afrika Mashariki na duniani kote.

Alitoa mfano wa miji ya Moshi na Arusha ambayo alisema imefanikiwa katika jambo hilo kutokana na kuwa na kanuni bora.

“Tuipitie kwa kina na kuichangia  rasimu hii, ili baadae tuwe na kanuni itakayokuwa rahisi kwetu ili hapo baadae kusiwepo tena mtu anayetupa taka kwenye misingi, magofu au katika ukanda wa pwani na mito, wala mtu anayesubiri mvua inyeshe ili atupe taka zake,” alieleza Mjaja.   

Akizungumzia kanuni hiyo inayohusu uhifadhi wa taka, Mwanasheria wa Manispaa ya Magharibi ‘A’ Zainab Makame Mussa, alikiri kuwa ukusanyaji wa taka ni tatizo sugu linaloiumiza kichwa manispaa yake.

Alieleza matarajio yake, kuwa kupatikana kwa kanuni mpya ambayo itawahusisha wananchi na taasisi mbalimbali ambazo ndio wazalishaji wakubwa wa taka, kutaleta ufumbuzi wa kuzihifadhi taka ili zisisambae ovyo na kupoteza haiba ya miji.

Aidha alisema, ili kanuni hiyo iwe na nguvu na iweze kutekelezeka, ni lazima kutolewe elimu kwa wananchi, na kuwepo ushirikiano kati yao na manispaa, katika jitihada za kuimarisha huduma za miji na kuiondoshea Zanzibar aibu ya uchafu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Manispaa ya Mjini Aboud Hassan Serenge, alisema suala la kuuweka mji usafi na utunzaji mazingira kwa jumla, sio la manispaa au serikali pekee, bali ni la kila mwananchi. 
  
Alisema kanuni inayojadiliwa ili iweze kufanywa sheria ndogo, itakuwa tiba ya tatizo la uchafu, ambapo kutakuwa na uchambuzi wa taka za aina mbalimbali, utakaonzzia katika nyumba za wakaazi kabla hazijakusanywa na watu watakaopewa jukumu hilo.

Mpango huo unaendeshwa chini ya ushauri na usimamizi wa kituo cha sayansi na mazingira kutoka India, ambapo Naibu Meneja wake Dkt. Sonia Devi Henam alishiriki kikao hicho kuzipitia kanuni hizo na kutoa mapendekezo kadhaa. 

IMETOLEWA NA HABARI MAELEZO ZANZIBAR
25 AGOSTI, 2018



No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.