Habari za Punde

Rais Dk Shein aendelea na ziara nchini Indonesia awakaribisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Indonesia kuja kuwekeza zanzibar




STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Jakarta, Indonesia                                                       02.08.2018
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewakaribisha wafanyabiashara na wawekezaji wa nchini Indonesia kuja kufanyabiashara na kuwekeza Zanzibar kutokana na fursa mbali mbali zilizopo.

Dk. Shein aliyasema hayo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenyeviwanda ya Indonesia (KADIN), huko katika ukumbi wa ofisi ya Jumuiya hiyo iliyopo mjini Jakarta Indonesia.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuna sababu mbali mbali ambazo wawekezaji wanaweza kuichagua Zanzibar kama ni sehemu pekee ya kuekeza ikiwa ni pamoja na kuwepo mazingira mazuri ya uwekezaji yaliowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kuwa na soko kubwa la kibiashara linalojumuisha nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).

Aidha, Rais Dk. Shein aliwaeleza wanajumuiya hiyo kuwa miongoni mwa sababu kubwa ambayo Zanzibar pamoja na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inajivunia ni kuwepo kwa amani, usalama na utulivu mkubwa nchini Tanzania na Zanzibar kwa ujumla.

Dk. Shein alieleza kuwa uchumi wa Zanzibar umekuwa ukiimarika ambapo mnamo mwaka 2017 ulifikia asilimia 7.5 ikilinganishwa na mwaka 2016 ambapo ulifikia asilimia 6.8 huku akieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2020.

“Tupo hapa kwa ajili ya kukukaribisheni mje Zanzibar kufanya biashara na kuwekeza katika sekta mbali mbali…..kihistoria Zanzibar ilikuwa ni kituo maalum cha biashara ndani na nje ya Bara la Afrika”,alisema Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa kunaweza kuimarishwa uhusiano madhubuti kati ya taasisi zinazomilikiwa na Serikali zote mbili katika maeneo ya biashara na uendelezaji wa miundombinu ambapo uhusiano kama huo pia, unaweza kuanzishwa kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kampuni mbali mbali za binafsi za nchini Indonesia.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kumekuwa na mahusiano ya karibu na ya muda mrefu kati ya Zanzibar na Indonesia na kusema kuwa tokea mwanzoni mwa miaka ya 50 Indonesia ilianza urafiki na nchi nyingi katika bara la Afrika ikiwemo Tanzania.

Aliongeza kuwa uhusiano huo, uliimarika zaidi mara baada ya Mkutano wa Bandung uliofanyika mwaka 1955 mjini Jakarta Indonesia ambao ulikuwa muhimu na kuweza kuongeza chachu katika nchi zisizofungamana na upande wowote na hatimae mnamo mwaka 1964 muungano wa nchi hizo uliimarishwa katika kkutano uliofanyika huko Bilgrade, mjini Yugoslavia.

Akitangaza fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar katika sekta mbali mbali za uchumi, katika mkutano huo Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) Salum Khamis Nassor alieleza kuwa Zanzibar ni eneo la pekee lenye matumaini katika kuekeza sekta kadhaa za uchumi.

Akizitaja sekta hizo alisema ni sekta ya utalii, kilimo, uvuvi, biashara, nishati, usafiri na usafirishaji pamoja na sekta ya uendeshaji wa miji mipya.

Mkurugenzi huyo wa (ZIPA), akizielezea fursa hizo alisema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua juhudi kubwa katika kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji pamoja na biashara ili kuwawezesha  wawekezaji na wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi kufanya biashara kwa faida kwa manufaa yao na ya nchi kwa jumla.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejidhatiti kusimamia mazingira ya uwekezaji kwa kuona kwamba wawekezaji wanashirikiana vyema na Serikali katika kuimarisha uchumi ikiwa ni pamoja na kuanzisha ajira kwa vijana.

Nao viongozi na Wanajumuiya ya Wafanyabiashara na Wenyeviwanda ya Indonesia (KADIN), walileza mafanikio waliyoyapata katika Jumuiya yao hiyo na kuahidi kuitumia vyema fursa ya kuja kuekeza na kufanya biashara Zanzibar ikiwa ni kuitikia wito wa Rais Dk. Shein wa kuwataka kuekeza Zanzibar.

Mara baada ya mkutano huo, Rais Dk. Shein alikutana na uongozi wa Kampuni ya mafuta na gesi ya Pertamina ya nchini humo ambao ulimueleza mafanikio iliyoyapata katika shughuli zake kwenye sekta hizo na kueleza kuwa tayari imeshaanza kufanya shughuli zake  huko Tanzania Bara katika maeneo ya Lindi na Mafia.

Hivyo, kutokana na mkutano huo Kampuni hiyo ilivutika na kuahidi kuitumia fursa hiyo ili kuangalia uwezekano wa kuanzisha mashirikiano na kuja kuekeza Zanzibar hasa ikizingatia uzoefu na mafanikio iliyoyapata katika sekta hizo.

Mapema katika ukumbi wa Hoteli ya Borobudur, Rais Dk. Shein alikuna na kufanya mazungumzo na Meya wa Jimbo la Gorontalo, Profesa Nelson Pomalingo ambapo Rais Dk. Shein na kiongozi huyo walieleza haja ya kuimaisha ushirikiano kati ya Zanzibar na Indonesia katika sekta ya kilimo hasa kilimo cha minazi.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo historia ya mafanukio iliyokuwa nayo Zanzibar katika kilimo cha zao hilo ambalo hivi sasa limekuwa adimu kutokana na sababu mbali mbali zikiwemo athari za kimaumbile na zile zinazofanywa na binaadamu ikiwemo kuikata kwa makusudi licha ya kuwepo kwa maradhi yanayoiathiri minazi kwa hivi sasa.

Nae kiongozi huyo wa Jimbo la Gorontala alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Indonesia na Zanzibar ni maeneo yaliyofanana kijiografia hivyo kushirikiana katika sekta ya kilimo kuna weza kuongeza tija na hatimae kuleta mafanikio kwa pande zote mbili.

Hata hivyo, kiongozi huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa katika kilimo cha minazi licha ya kuwa changamoto zilizopo katika kilimo hicho kwa upande wa Indonesia zinafanana na zile za Zanzibar lakini hata hivyo nchi hiyo imeweza kupata mafanikio makubwa katika kilimo cha minazi.

Katika mazungumzo hayo, kiongozi huyo wa Gorontalo aliahidi kuanzisha na kuendeleza uhusiano na ushirikiano uliopo na kusisitiza kuwa atahakikisha mashirikiano yanafanyika katika kuhakikisha kilimo hicho kinaimarika katika visiwa vya Zanzibar.

Wakati huo huo, viongozi na watendaji wakuu wa Serikali walioambatana na Rais Dk. Shein katika ziara yake hiyo walipata fursa ya kukutana na kufanya mazungumzo na watendaji wenzao wa nchini Indonesia katika ukumbi wa hoteli ya Borobudur.

Katika mikutano hiyo iliyofanyika kwa nyakati tofauti, viongozi na watendaji hao walieleza haja ya kuwepo kwa mashirikiano ya pamoja sambamba na kubadilishana uzoefu na utaalamu katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiweko sekta ya utalii, uvuvi na kilimo.

Pamoja na hayo, mazungumzo hayo yalionesha pande zote mbili kukubaliana na hoja ya kuimarisha ushirikiano katika sekta hizo ambazo zimekuwa ni sekta muhimu kwa nchi zote mbili na zimekuwa zikichangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi na kuchangia pato la Taifa.

 Rajab Mkasaba, Jakarta, Indonesia
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.