Habari za Punde

ZFA yatoa onyo kali kwa timu itakayopanga matokeo


Msemaji wa kamati Teule ya chama cha soka Visiwani Zanzibar (ZFA) Abubakar Khatib Kisandu amezitahadharisha timu zote ambazo zinashiriki ligi kuu soka ya Zanzibar hatua ya nane bora pamoja na zile zinacheza ligi ya Mabingwa Wilaya kuwa makini na aina yoyote ya upangaji wa matokeo katika kipindi hichi cha mwisho kuelekea kumalizika michezo ya mwisho ya msimu wa mwaka 2017-2018 huku kukiwa na mvutano mkubwa wa kuzitafuta nafasi za ubingwa wa ligi hizo.
 Kisandu amesema kuna viashiria vya upangaji wa matokeo katika kipindi hichi lakini ZFA wamejipanga kuhakikisha kuwachukulia hatua timu au mtu yoyote atakaehusika katika kadhia hiyo.
Amesema kwa sasa ZFA wanashirikiana kwa ukaribu sana Mamlaka ya Kupambana na Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar (ZAECA) ili kuwakamata wale wote wanaohusika na makosa hayo.
 ‘’ Kuna viashiria vya Rushwa tumevibaini, tayari kuna baadhi ya timu tumeshaanza kuzigundua zinataka kucheza mchezo huu mchafu, lakini wajuwe kuwa tupo makini sana na tutachukua hatua kali dhidi yao, kama walizowea kufanya mchezo huo mchafu kwa miaka ya nyuma, kamati ipo makini kwa hilo na timu yoyote tukiigundua bila kuiangalia usoni kama ni ya kikosi au ya uraiani tutaichukulia hatua’’. Alisema Kisandu.
 Inasemekana ikifika kipindi hichi cha mwisho wa kumalizika kwa msimu kwaajili ya kumtafuta bingwa kuna baadhi ya timu hucheza mchezo huo mchafu hasa kwa timu za aina mbili zinazowania Ubingwa na Makamo Bingwa hupanga na zile ambazo hazina nafasi yoyote ya kutwaa Ubingwa au nafasi ya Pili.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.