Habari za Punde

‘Siti And The Band’ wakogeshwa manoti

WAZIRI wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo na Katibu Mkuu wa wake Khadija Bakari Juma (Kulia), kwa pamoja wakiwakabidhi wasanii wa kikundi cha taarab asilia ‘Siti And The Band’ shilingi 5,000,000 pamoja na Dola 300 za Kimarekani, walizotunukiwa na wafadhili wawili tafauti kukiunga mkono kikundi hicho baada ya kufanya  vizuri kwenye maonesho ya utalii 2018 yaliyoandaliwa hapa Zanzibar. Hafla hiyo ilifanyika leo Oktoba 25, 2018 katika ofisi za wizara Kikwajuni Unguja.

 MWIMBAJI na kiongozi wa kikundi cha ‘Siti And The Band’ Amina Omar Juma, akimzawadia fulana maalumu Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar, Mahmoud Thabit Kombo, kuthamini mchango wake na wizara katika kukisaidia kikundi chao kinachoundwa na wasanii wachache vijana.

                                     Picha zote na Salum Vuai, WHUMK.


Na Salum Vuai, WHUMK
BAADA ya kunogesha maonesho ya utalii Zanzibar yaliyofanyika wiki iliyopita, wasanii wa kikundi cha muziki ‘Siti And The Band’, leo Oktoba 25, 2018, wamekabidhiwa kitita cha shilingi 5,000,000 sambamba na dola 300 kutoka kwa wafadhili mbalimbali.
Fedha hizo walizoahidiwa siku ya kufungwa kwa maonesho hayo kwenye hoteli ya Verde iliyoko Mtoni mjini Zanzibar, zilikabidhiwa kwao na Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale, Mahmoud Thabit Kombo katika ukumbi wa wizira hiyo Kikwajuni.
Tunzo ya shilingi 5,000,000 imetolewa na mfadhili kutoka nchi ya Oman, Ahmed Suleiman, wakati mfadhili mwengine ambaye hakutaka kutajwa jina, amewatunuku vijana hao mahiri dola 300 za Kimarekani kwa lengo la kukiendeleza kikundi chao.
Akizungumza katika hafla hiyo fupoi iliyohudhuriwa pia na watendaji wakuu kadhaa wa wizara yake, Waziri Kombo amewaomba Wazanzibari na wageni wengineo wanaofika nchini, kuwaunga mkono vijana hao na wasanii wengine, kama anavyofanya Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein katika kukuza kazi za sanaa.
"Jambo walilolifanya katika tamasha la utalii ni kubwa na lilileta msisimko kwa wageni wote waliohudhuria, akiwemo Rais wa Zanzibar, ambaye daima amekuwa mstari wa mbele kuwawekea wasanii mazingira mazuri ili waweze kujiajiri kupitia Sanaa zao," alisema Waziri huyo.
Alisema kikundi hicho kimekuwa kikifanya vizuri katika muziki wa taarab kwa kutumia ala za asili kikiendeleza pia kazi za wasanii wakongwe wa zamani marehemu Sitti Bint Saad na Fatma Baraka ‘Bi. Kidude’ ambao wakati wa uhai wao, walifanya kazi kubwa kuitangaza Zanzibar kupitia taarab asilia.
Aliwatakia kila la kheri katika jitihada zao za kuendeleza muziki, akiahidi kuwasaidia kuwasafishia njia ya kupanda juu zaidi ya walipo sasa.
“Nakupongezeni sana na ninakuombeni mkatumie fedha mnazopewa ili zisaidie kukuleteeni maendeleo zaidi na zisigeuke kuwa fitna zikaleta mfarakano,” alisisitiza Waziri Kombo.
Kiongozi na mwimbaji wa kikundi hicho Amina Omar Juma, kwa niaba ya wenzake, alitumia nafasi hiyo kumshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Waziri wa Habari na uongozi wote wa wizara kwa namna walivyojitoa kuwaunga mkono, na wameahidi kutowaangusha.

Amina, maarufu ‘Sitti Amina’, amewataka wasanii wenzake kushikamana na kufanya kazi kwa bidii, kwa kubuni njia za kujipaisha badala ya kujikita kwenye kupikiana majungu, chuki na uhasama miongoni mwao.
Aidha, aliwasihi wajiepushe kuiga wasanii wa nje hasa katika mavazi na mitindo ya nywele inayokwenda kinyume na maadili ya nchi yao.
Aliwasisitiza watumie akili na maarifa yao kubuni vya kwao, huku wakiendeleza sanaa za asili za Zanzibar na Tanzania kwa jumla.
Ikumbukwe kuwa, katika hafla ya kufunga pazia la maonesho ya utalii usiku wa Oktoba 20, 2018, Rais Dk. Shein alikizawadia kikundi hicho shilingi 6,000,000 na mke wake Mama Mwamwema, akiitononosha zawadi hiyo kwa shilingi 4,000,000 na kufanya jumla kuwa shilingi 10,000,000.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.