Habari za Punde

Uzinduzi wa Klinik ya Meno Katika Hospitali ya Kivunge Mkoa wa Kaskazini Unguja.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akiondoa kipazia kuashiria kuizindua Klinik ya Mane katika Hospitali ya Kivunge Mkoa wa Kaskazini Unguja.kushoto Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Hamad Rashid Mohammed. 


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ametangaza rasmi kuwa Hospitali ya Kivunge na Hospitali ya Makunduchi ambazo zote ni Hospitali za Koteji zifutwe na ziwe Hospitali za Wilaya kuanzia leo kutokana na sifa, mwelekeo na vigezo ilivyovifikia.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika uzinduzi wa Kitengo cha Kinywa na Meno kiliyoko katika huko Hospital ya Kivunge Mkoa wa Kaskazini Unguja ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na serikali akiwemo Balozi wa Uturuki nchini Tanzania Ali Govutogh pamoja na wananchi wa Mkoa huo.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa kwa huduma zake tayari hospitali hizo ni za Wilaya ambapo tayari jengo jipya la mama wajawazito na watoto linajengwa jambo ambalo aliielekeza Wizara kuwa lengo lake ifikapo mwaka 2020 hospitali hizo ziwe za Mkoa kwani tayari kuna mambo yamekamilika.

Aliwataka Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja na Waziri wa Afya kuanza kufikiria nafasi  ya ili hospitali hiyo izidi kupanuka zaidi na kuwataka kuzungumza na Wizara nyengine ili watu wa Kaskazini Unguja wapate hospitali ya kisasa ambayo itakayokuwa inatoa huduma bora na kulaza wagonjwa pamoja na kutoa huduma bora za meno.

Aliwataka viongozi hao wakutane na Kamati zao na watendaji wao kutafuta nafasi ya kuipanua Hospitali ya Kivunge kwani Ilani ya Uchaguzi ya CCM imeweka lengo kuwa Hospitali hiyo iwe ya Wilaya ifikapo 2020 kwa kupanda daraja

“Naiagiza Wizara ya Afya kuwa jina la Hospitali hii ya Koteji ya Kivunge lifutwe na andikeni Hospitali ya Kivunge ya Wilaya na Hospitali na ile ya Makunduchi andikeni Hopatali ya Makunduchi ya Wilaya na mwaka 2020 zitakuwa hospitali za Mkoa”,alisisitiza Dk. Shein.

Alisema kuwa Marehemu Mzee Abeid Amani Karume yeye ndio msingi wa yote mazuri yanayofanyika na chanzo cha kutangazwa na huduma bure za afya ambayo yote hayo yalitokana na Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ambayo yalikuwa na lengo la kuondosha dhiki na dhulma kwa mwenye nacho na asiyekuwa nacho kwani yameleta usawa.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Mapinduzi Daima ina maana ya kuwa yale yote yaliyokuwa si mema na yanakwenda kinyume na matakwa ya Wazanzibari yataondoshwa, kwani huduma za afya zilikuwa zikipatikana kwa ubaguzi na hali kwa sekta hiyo na sekta ya elimu haikuwa nzuri.

Akitoa historia fupi ya sekta ya afya, Dk. Shein alisema kuwa tarehe 3 Julai mwaka 1964 ndio ulipowekwa utaratibu mpya wa misingi ya Afya ambapo Marehemu Mzee Aboud Jumbe Mwinyi alipeleka warka maalum namba 37 katika Baraza la Mapinduzi (BLM) pamoja na mambo mengine 17 ambapo mambo yote yanayofanyika hivi sasa msingi wake ni huo.

Aliongeza kuwa hatua hiyo ndiyo iliyompekekea Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kutangaza afya bure siku ya tarehe 3, Machi, 1965 ambapo kwa mujibu wa Rais Dk. Shein Sera hiyo bado inaendelezwa hadi hivi leo katika uongozi chini ya CCM.

Alisema kuwa kutokana na changamoto ya ongezeko la idadi ya watu hapa Zanzibar ndio ilipelekea mambo mengi kutotosha kutokana na kuongezeka mara kumi zaidi katika eneo la Kivunge jambo ambalo linahitaji kuwepo mpango madhubuti na sio kama Serikali inashindwa kutoa huduma hizo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza historia ya afya hapa Zanzibar na kusema kuwa wakati wa ukoloni ambapo Zanzibar ilikuwa na watu 320,000 na vituo vya afya vilikuwa 32 Unguja na Pemba ambapo hivi sasa vipo karibu vituo 150 pamoja na hospitali kuwa zenye mambo mengi na huduma za kisasa licha ya kuwepo kwa idadi kubwa ya watu.

Alisema kuwa Serikali imejidhatiti kuhakikisha haiba ya hospitali ya Kivunge inabadilika kwa kuongeza na kupanua huduma zote za afya na kuupongeza Mradi wa Kuimarisha Afya Zanzibar (HPZ) kwa kujenga kituo hicho“abebwae hujikaza hivyo na sisi tutajikaza ili kuhakikisha huduma za meno hapa Zanzibar zinaimarika” alisema Dk Shein.

Alisema kuwa kituo hicho ni mwanzo katika huduma za meno na kuahadi kuwa Serikali itapanua njia zaidi na kuunga mkono ambapo kwenye Bajeti ya Serikali hapo mwakani itaongeza vifaa na nafasi katika kitengo hicho cha meno pamoja na huduma nyengine katika hospitali hiyo.

Alisema kuwa kuna uhusiano mzuri baina ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Uturuki na Zanzibar na Uturuki na kutumia fursa hiyo kueleza kuwa mafanikio hayo yanatokana na ziara aliyoifanya mwezi Februari 2011 alipofanya mazungumzo na Rais wa nchi hiyo Abdullah Gul wakati huo ambapo katika maeneo waliyoahidi kushirikiana ni pamoja na sekta ya afya.

Dk. Shein pia, alieleza hatua alizozichukua akiwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kwa kuanzisha Kitivo cha Madaktari katika chuo hicho huku akieleza azma ya kuanzisha  kufundishwa kwa Madaktari wa meno hapa Zanzibar.

Rais Dk. Shein aliwahakikishia viongozi na Wanajumuiya wa mradi wa (HIPZ) kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana nao kwa kasi, ari na nia ile ile na kuendelea kushirikiana nao kwa yote wanayoyafanya kwa lengo la kuimarisha sekta ya afya  hapa nchini.

Alisema kuwa huduma hizo za afya za meno katika hospitali hiyo hazikuwepo hapo kabla ambapo hivi sasa mambo yameongezeka na vifaa vya kisasa vya Digital vipo vya kutosha na kuwataka wananchi wa eneo hilo kuitumia vyema bahati na neema hiyo.

Alisisitiza haja ya kwa wananchi kuvitunza vifaa hivyo vipya na vya kisasa katika Kitengo hicho cha Kinywa na Meno katika Hospitali ya Kivunge na kuwataka kuthamini jitihada za (HIPZ) za kuchangia na kusaidia huduma za afya hapa nchini. ”lazima tushirikiane nao ili ndugu zetu hawa waendeleee kutusaidia”,alisisitiza Dk. Shein.

Nae Waziri wa Afya  Hamad Rashid Mohammed alisisistiza haja ya wananchi kuthamini na kuzijali juhudi zinazochukuliwa na Mradi wa (HIPZ)  sambamba na kuiga mifano yao huku akiwapongeza wasimamizi wa mradi huo hapa nchini.

Aidha, Waziri Hamad alilaani kitendo kinachofanywa na wale wote wanaosomeshwa na Serikali ndani na nje ya nchi na hatimae wanaporudi hushindwa kuitumikia nchi yao na wananchi wenzao na badala yake wanakwenda kufanya kazi sehemu nyengine kwa kisingizo cha mshahara mdogo.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Asha Ali Abdalla alieleza kuwa kwa hatua iliyofikia Hospitali ya Kivunge tayari Hospitali hiyo imeshafikiwa daraja la kuwa Hospitali ya Wilaya na mwelekeo ni kuendelezwa ili iweze kufikia daraja la Hospitali ya Mkoa.

Alieleza kuwa katika kufanikisha hilo juhudi zinaendelea za kuimarisha utoaji wa huduma kwenye Hospitali hiyo ambapo jengo jipya la ghorofa mbili kwa ajili ya wodi ya wazazi na ya watoto linaendelea kujengwa na linategemewa kumaliza mwezi Julai 2019.   

Meneja Mkuu wa Mradi wa (HIPZ) kutoka Uingereza Ru MacDonald Alieleza juhudi za Mradi huo tokea kuanzishwa kwake na kuahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na kuziimarisha Hospitali ya Kivunge na Makunduchi.

Mapema Meneja wa (HIPZ) Zanzibar Pamella Allard alisema kuwa (HIPZ) imeanzisha huduma nyingi za msaada katika Hopsitali ya Kivunge na Makunduchi za kukabiliana na changamoto za kiafya kama vile utapia mlo, ajali za kuungua, huduma za afya ya watoto njiti ambapo mtazamo wao ni kutoa elimu kwa jamii hasa kwa maradi ya meno.

Aliongeza kuwa tangu kuanza mwaka 2007 (HIPZ) imetumia Bilioni 5.5 ambapo kwa kufanya kazi pamoja na Serikali sasa wana wafanyakazi wengi zaidi kuliko hapo mwanzo katika hospitazli za Makunduci na Kivunge.

Mapema Dk. Shein alitembelea jengo jipya lilojengwa la mama wajawazito na watoto na kupata maelezo juu ya ujenzi huo na kutembelea wodi ya wazazi, maabara, wodi ya watoto njiti na kuizindua Kitengo cha Kinywa na Meno kilichojengwa chini ya mradi wa (HIPZ).
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.