Habari za Punde

Jumla ya Shehiya 388 Kuwekewa Alama Mpya za Mipaka Zanzibar.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Mhe. Haji Omar Kheir akiwa na uongozi mzima wa Wizara yake akitoa tamko la uwekaji wa alama za mipaka ya shehia zote za Unguja na Pemba kwa wandishi wa habari huko katika ukumbi wa Chuo cha Mafunzo Kilimani Mjini Unguja.

Baadhi ya viongozi wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ wakimsikiliza Waziri wa Wizara hiyo (hayupo pichani) alipokuwa akitoa tamko la uwekaji wa alama za mipaka ya shehia katika ukumbi wa Chuo cha Mafunzo Kilimani Mjini Unguja. Picha na Makame Mshenga.


Na.Khadija Khamis –Maelezo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ Haji Omar Kheir ametangaza uwekaji wa alama za mipaka ya shehia zote za Unguja na Pemba.
Akitoa taarifa ya uwekaji wa Mipaka mbele ya Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Chuo cha Mafunzo Kilimani, Waziri Haji Omar Kheir alisema zoezi hilo litaanza rasmi Disemba 18, 2018 katika Wilaya ya Mjini na baadae kuendelea katika Wilaya nyegine.
Alisema usimamizi wa kazi hiyo inafanywa kwa mashirikiano makubwa na Taasisi muhimu za Serikali zikiwemo Kamisheni ya Ardhi na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali.
Alisema kukamilika kwa kazi hiyo haitanufaisha Wizara hiyo peke yake bali   itawasaidai wahusika wengine kufanyakazi zao zikiwemo za utafiti, mipango miji na vijiji, utafutaji wa rasilimali, sense, uandikishaji wa raia, ulinzi na usalama, mipango ya kijamii na kiuchumi pamoja na ukusanyaji wa takwimu
Waziri Haji Omar Kheir aliweka wazi kuwa lengo la uwekaji wa mipaka hiyo ni kurahisisha shughuli za kiutawala na utowaji bora wa huduma kwa wananchi na halihusiani na masuala mengine yoyote na hakuna haja ya kuanzisha ajenda itakayoleta mifarakano ndani ya shehia.
Aliwataka viongozi wa shehia na wananchi kwa jumla kutowa ushirikiano kwa maafisa watakaoendesha zoezi hilo na kufuata maelekezo watakayopewa ili liweze kufanikiwa kama lilivyokusudiwa.
Waziri Haji Omar Kheir alisema Zaidi ya shiling milioni 37 zimetumika kwa kutengeneza alama (Bicon) ambazo zitawekwa katika shehia zote 388 Unguja na Pemba.
Katika mwezi wa Mei, 2015 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein alifanya maamuzi ya kuigawa Zanzibar katika maeneo ya  Shehia Wilaya na Mikoa na maeneo mengine ya kiutawala  kwa mujibu wa uwezo aliopewa na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 Sheria ya Tawala za Mikoa ya Mwaka 2014.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.