Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe
Magufuli akihutubia katika hafla ya Utiaji saini wa Mkataba wa Ujenzi wa Mradi wa kuzalisha Umeme
katika mto Rufuji, Mkataba ambao umesainiwa leo 12 Disemba ,2018 Ikulu Jijini
Dar es Salaam, kati ya Serikali ya Tanzania na kampuni ya ujenzi ya Arab Constructor kutoka nchini Misri.
Na
Mwandishi Wetu,MAELEZO.12.12.2018
RAIS
Dkt. John Magufuli ameihakikishia Serikali ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri na
wadau wa maendeleo kuwa Serikali yake
itasimamia utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme katika Mto Rufiji
(Stiegler’s Gorge) kwa kuwa ndiyo njia sahihi ya kufikia Uchumi wa Viwanda
ifikapo mwaka 2025.
Akizungumza katika Hafla ya Utiaji saini ya Mkataba
wa Ujenzi wa Mradi huo leo Jumatano (Desemba 12,2018) Jijini Dar es Salaam na
kushuhudiwa na Waziri Mkuu wa Misri, Dkt. Mostafa Madbouly,
Rais Magufuli alisema Serikali ya Awamu ya Tano ipo imara na itahakikisha kuwa
mradi huo utakaozalisha Megawati 2100 unakamilika kwa wakati ili kuiwezesha
Tanzania kuweza kupiga hatua kubwa zaidi katika maendeleo.
Rais Magufuli alisema Serikali ya Awamu ya Tano
imekusudia kuharakisha utekelezaji wa mradi wa umeme wa Mto Rufiji Stiegler’s
Gorge huo kutokana na ukweli kuwa uzalishaji wa umeme kwa chanzo cha maji ni
rahisi katika uzalishaji wake ukilinganisha na vyanzo vingine vya uzalishaji wa
nishati ya umeme ikiwemo upepo, makaa ya mawe, nyuklia, jua na joto ardhi.
“Ukiutazama mradi huu wa Stiegler’s Gorge unatoka
katika mikoa na maeneo ambayo yana kiasi kikubwa cha mvua, lakini pia umeme wa
maji ni rahisi sana ni Tsh 36 kwa uniti moja ukilinganisha na Nyuklia (Tsh 65),
Jua (Tsh 103.5), joto ardhi (Tsh 114.5), upepo (Tsh 103.5), Makaa ya Mawe (Tsh
118), na mradi huu ukikamilika bei ya umeme itashuka kwa kiasi kikubwa sana”
alisema Rais Magufuli.
Aidha Rais Magufuli alisema kukamilika kwa
utekelezaji wa mradi wa ujenzi huo, kutaiwezesha Tanzania kuzalisha kiasi
kikubwa cha umeme kitachokasaidia kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati
ikiwemo ujenzi wa uchumi wa viwanda na mradi wa reli ya kisasa, hatua
itakayoiwezesha kupiga hatua kubwa za maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wake.
Akifafanua zaidi Rais Magufuli alisema kabla ya
kufikiwa kwa uamuzi wa utekelezaji wa mradi huo, kulitokea baadhi ya makundi ya watu waliokuwa wakipinga kujengwa
kwa mradi huo huo kwa kigezo kuwa mradi huo utaleta tishio la uharibifu wa
mazingira katika hifadhi ya selous jambo ambalo halina ukweli wowote.
“Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Timu ya
Watalaamu wa Serikali, hakutokuwa na athari yoyote ya mazingira na kwa kuwa
mradi wote unachukua aslimia 1.8 ya eneo la hifadhi, lakini eneo lile litakuwa eneo mahsusi kwa wanyama,
ndege na viumbe wote wa majini ikiwemo kuongezeka kwa mazalia ya samaki”
alisema Rais Magufuli.
Rais Magufuli alisema mradi huo unajengwa na mkandarasi
wa kampuni ya Arab Contractor utagharimu kiasi cha Trilioni 6.5 unatarajiwa
kujengwa kwa kipindi cha miezi 42 ambapo
Serikali imetoa sita kati ya miezi 36 ya ukamilishaji wa mradi huo, kwa
mkandarasi kuweza kukusanya vifaa vyake na kuvipeleka katika eneo la mradi.
Kwa upande wake, Waziri Mkuu wa Misri Dkt. Mostafa Madbouly alisema Serikali yake
itaendelea kuimarisha ushirikiano wa kiufundi, kitaalamu na kidiplomasia na
Tanzania ili kuhakikisha kuwa ndoto za waasisi wa urafiki wa mataifa hayo zinaweza
kutimizwa ikiwemo utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Aliongeza kuwa Serikali ya
Jamhuri ya Kiarabu ya Misri imeridhishwa na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano
kupitia kwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya
maendeleo iliyofikiwa na Tanzania katika kipindi kifupi cha utawala tangu
kuingia kwake madarakani mwaka 2015.
Kwa mujibu wa Madbouly alisema katika kipindi cha miaka michache ijayo,
Serikali ya Misri kupitia kwa taasisi zake za kiuchumi zitaendelea kuwekeza kwa
kasi zaidi nchini Tanzania ili kuhakikisha kuwa miradi yote ya maendeleo
inayotekelezwa na Tanzania inaweza kuleta tija kwa wananchi wake.
Awali akitoa taarifa ya mradi huo, Waziri wa Nishati wa Tanzania, Dkt.
Medard Kalemani alisema Mradi wa Stiegler’s Gorge ni moja ya miradi mikubwa ya
kufua umeme katika dunia na Afrika kwa ujumla na hivyo utekelezaji wake utaiweka
Tanzania katika ramani ya juu zaidi ulimwenguni.
Dkt. Kalemani alisema kupitia katika vyanzo mbalimbali vya nishati ya umeme
vilivyopo nchini, Serikali ya Awamu ya Tano imekusudia kuhakikisha Tanzania
inaweza kuzalisha Megawati 5000 za umeme ifikapo mwaka 2020 na Megawati 10,000
ifikapo mwaka 2025 na hivyo kuiwezesha Nchi kuwa muuzaji wa umeme katika nchi
jirani.
“Tumepanga kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2025, tunakuwa na umeme katika
kila kijiji na hili litawezekana kwa kupitia utekelezaji wa miradi ya umeme
iliyopo nchini, na mradi wa Mto Rufiji ni mojawapo ya vipaumbele vya kimkakati”
alisema Dkt. Kalemani.
No comments:
Post a Comment