Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Akizungumza na Mwakilishi wa UNICEF Nchini Tanzania leo Ikulu Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Mfuko wa Umoja wa Mataifa Unaoshughulikia Maendeleo ya Watoto (UNICEF) Nchini Tanzania Bi.Maniza Zaman, alipofika Ikulu Zanzibar,kumtambulisha Mkuu wa UNICEF Ofisi ya Zanzibar Bi. Maha Damaj, na kufanya mazungumzo leo.4/12/2018.  

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza mikakati inayochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kupambana na maradhi mbali mbali yakiwemo ya miripuko ambapo yanapozuka huathiri watu wa rika zote wakiwemo watoto.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na  Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Watoto (UNICEF) nchini Tanzania Maniza Zaman aliyefuatana na Mkuu mpya wa Shirika hilo hapa Zanzibar Maha Damaj ambaye alifika kujitambulisha kwa Rais.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa miongoni mwa juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hivi sasa ni pamoja na kujenga mitaro mikubwa katika eneo la mji wa Zanzibar ambayo matokeo yake itaisadia kuondosha matuamo ya maji ambayo hatimae huleta maradhi ya miripuko na kulata athari kubwa kwa jamii.

Aliongeza kuwa katika kipindi kifupi ambacho bado mradi huo ujenzi wake unaendelea tayari mradi umeanza kuleta matumaini makubwa ambapo athari mbali mbali ambazo hapo siku za nyuma zilikuwa zikitokea zimepungua ikiwemo kutuama kwa maji pamoja na kuleta mafuriko.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya jitihada hizo suala zima la elimu pamoja na kuendeleza Sera na mikakati ya Serikali katika kupambana na maradhi mbali mbali pamoja na kuimarisha ustawi wa akina mama na watoto zimekua zikichukuliwa.

Hata hivyo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kulipongeza Shirika la UNICEF kwa jitihada zake za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuhakikisha watoto wa Zanzibar wanapata haki zao za msingi ikiwa ni pamoja na elimu, afya pamoja na huduma nyengine za kijamii.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuwepo kwa Programu ya Pamoja ya Zanzibar” (ZIP), inayohusisha Mashirika tisa ya UN iliyozinduliwa hivi karibuni kutasaida katika kuleta mafanikio yaliokusudiwa kwa wananchi wa Zanzibar.
Nae Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Watoto Duniani (UNICEF) nchini Tanzania Bi Maniza Zamani alipongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika suala zima la kuwahudumia watoto pamoja na akina mama.

Bi Zamani alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweza kupata mafanikio makubwa katika kuwahudumia watoto sambamba na kuhakikisha wanapata haki zao za msingi ikiwemo kupata elimu na afya bora huku akizipongeza juhudi za Serikali.

Alieleza kuwa Shirika hilo linathamini juhudi hizo na limeweza kushuhudia mafanikio na mabadiliko makubwa katika sekta za maendeleo hatua ambazo zimewawezesha watoto wa Zanzibar  kuweza kupata haki zao za msingi pamoja na mahitaji yao muhimu ya kimaisha.
Mwakilishi huyo alieleza azma ya programu ya pamoja ya UN hapa Zanzibar kuwa mbali na mambo mengine pia, itasaidia kupunguza vifo vya uzazi, ukatili dhidi ya wanawake na watoto.
Aliongeza kuwa Shirika la (UNICEF) limekwua likichukua juhudi zake katika kuhakikisha wananchi wa ngazi ya chini katika jamii wanashirikishwa kwa kuweka Kamati ndogondogo katika jamii katika kuhakikisha inakwenda sambamba na mikakati iliyowekwa na Shirika hilo. 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.