Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk.Ali Mohamed Shein, akizungumza na Balozi wa Jamuhuri ya Watu wa Korea Nchini Tanzania Mhe. Balozi Song Geum -young, wakiwa katika mazungumzo yao yaliofanyika Ikulu Zanzibar leo.6/12/2018.kwa ajili ya kumuaga baada ya kumaliza mada wake wa kazi Nchini Tanzania.
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini juhudi za Jamhuri ya Korea za kuendelea
kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya
kilimo.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri
ya Korea nchini Tanzania Sog Geum-yong, ambaye amefika Ikulu kwa ajili ya
kumuaga Rais baada ya kumaliza muda wake wa kazi hapa nchini.
Katika maelezo yake
Rais Dk. Shein alimueleza Balozi Sog kuwa Zanzibar inajivunia uhusiano na
ushirikiano mwema uliopo kati yake na Jamhuri ya Korea ambao umeweza kusaidia
kuimarika kwa sekta za maendeleo ikiwemo sekta hiyo ya kilimo ambapo tayari
imejiandaa vizuri kwa kuweka mazingira
mazuri ya mradi huo kwa kuyatayarisha mashamba yapatayo 60.
Rais Dk. Shein alimueleza
Balozi huyo kuwa hatua za Jamhuri ya Korea kusaini mradi wa miundombinu ya kilimo
cha mpunga wa umwagiliaji maji hivi leo ni uthibitisho wa wazi kuwa nchi hiyo
imeamua kwa makusudi kushirikiania na Zanzibar kivitendo.
Alieleza kuwa tokea
nchi hiyo ianze ushirikiano na ushusiano wa kidiplomasia kati yake na Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar mnamo miaka ya tisini, imeweza kutoa
ushirikiano wake mkubwa kwa Zanzibar kwa
kuweza kusaidia miradi kadhaa ikiwemo kilimo, elimu, uvuvi na mengineyo ambayo
imeweza kuimarisha sekta za maendeleo nchini.
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Jamhuri ya Korea imeweza kusaidia katika ujenzi wa skuli ya
kisasa ya Sekondari ya Kwarara ambayo pia, ina studio ya matangazo pamoja na
vifaa mbali mbali vya habari kwa ajili ya mafunzo na kutoa elimu kwa wananchi.
Pia, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa juhudi za Jamhuri ya Korea imeweza kusaidia kuanzishwa kwa kituo
cha kutotolea vifaranga vya samaki (marine hatchery), kaa na majongoo ya
baharini huko Bait el Ras ikiwa ni jitihada za kuhakikisha sekta ya uvuvi,
ufugaji, ajira kwa vijana sambamba na ukuaji wa uchumi vinaimarika hapa Zanzibar.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza kuwa Jamhuri ya Korea imekuwa mshirika mzuri wa maendeleo ya
Zanzibar kwa kuweza kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
katika mikakati yake ya kupambana na umasikini pamoja na kutekeleza Dira ya
Maendeleo ya Zanzibar ya 2020.
Rais Dk. Shein pia,
alimtaka Balozi Sog kuitangaza Zanzibar kiutalii katika Jamhuri ya Korea
sambamba na kuwakaribisha wawekezaji kuja kuekeza Zanzibar.
Aliongeza kuwa
Zanzibar iko salama na ushahidi wa kuthibitisha hilo unaonekana pale Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar ilivyoamua kwa makusudi kuanzisha mradi wa mji salama
ambao una malengo mazuri na mafanikio makubwa kwa wageni na wenyeji wa Zanzibar
katika kuhakikisha amani na usalama wao unakuwepo muda wote.
Nae Balozi wa Jamhuri
ya Korea nchini Tanzania Sog Geum-yong alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Jamhuri
ya Korea itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake kati yake na Zanzibar ikiwa
ni pamoja na kuhakikisha mradi wa mpunga wa umwagiliaji maji unatekelezwa.
Alisisitiza kuwa
katika kuongeza juhudi hizo kwenye sekta ya kilimo kupitia mradi huo
uliosainiwa wa miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji maji ambao unatarajiwa
kuwa wa miaka mitatu utagharimu Dola za Kimarekani milioni 59.9.
Alieleza kuwa licha ya
mradi huo kuchelewa kidogo lakini Jamhuri ya Korea bado ina imani kubwa kuwa
utafanikiwa kutokana na azma iliyowekwa na nchi hiyo kwa Zanzibar hasa
ikitambua juhudi za Rais Dk. Shein katika kuhakikisha Mapinduzi makubwa ya
kilimo yanafanyika Zanzibar kupitia kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji.
Balozi Song alieleza
kuwa mbali ya mradi huo wa mpunga wa umwagiliaji maji tayari nchi yake kupitia
Mashirikika yake likiwemo Shirika la Maendeleo la Jamhuri ya Korea (KOICA) linaendelea
kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali hapa Zanzibar.
Aidha, Balozi huyo
alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa kutokana na mafanikio makubwa iliyofia
Zanzibar katika sekta ya utalii atahakikisha anaendelea kuitangaza kiutalii
kutokana na kuwepo vivutio kadhaa ambavyo ni adimu kuvipata katika maeneo
mengine duniani.
Pia, Balozi huyo
ameahidi kuimarisha mashirikiano na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA)
katika kuendeleza programu mbali mbali sambamba na kusaidia Dola za Kimarekani
milioni 10 kwa ajili ya Mradi wa kusaidia elimu ya Sekondari ambao utajumuisha
ujenzi wa vituo vya kufundishia Sayansi na Maktaba kwa ngazi ya elimu ya
Sekondari pamoja na mradi wa mafunzo kwa walimu kazini.
Balozi Sog alitumia
fursa hiyo kumpongeza na Rais Dk. Shein na Serikali anayoiongoza kwa kumpa
mashirikiano makubwa wakati wote alipofanya kazi katika Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment