Habari za Punde

Hotuba ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, Aliyoisoma leo Wakati wa Kuahirisha Mkutano wa Kumi na Mbili wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi,akisoma Hutuba ya Kuahirisha Mkutano wa Kumi na Mbili wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar leo, Tarehe 06 Disemba, 2018

Mheshimiwa Spika, Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwingi wa Rehma kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kufanikisha Mkutano huu wa Kumi na Mbili wa Baraza la Tisa ulioanza tarehe 28 Novemba, 2018 hadi leo tarehe 6 Disemba, 2018 tunapouahirisha.

Mheshimiwa Spika, Napenda kutoa pongezi zangu za dhati kabisa kwa Rais wetu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kutekeleza matakwa ya Wazanzibari ya kutia saini mkataba wa mgawanyo wa uzalishaji wa mafuta na gesi asilia (Production Sharing Agreement) baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Kampuni ya RAKGAS tarehe 23 Oktoba, 2018. Mkataba huo ni halali kama ilivyokuwa halali boribo siagi kuliwa! Wale wanaodhani Rais wetu amevunja Katiba au sharia ya nchi ruhsa kwenda Mahakamani kwani nchi yetu inafuata misingi ya utawala bora.  

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza kwa dhati Mwakilishi wa Jimbo la Jang’ombe, Mheshimiwa Ramadhan Hamza Chande kwa kuapishwa kuwa Mjumbe wa Baraza lako Tukufu baada ya ushindi mkubwa wa kishindo alioupata wa uchaguzi mdogo uliofanyika tarehe 27 Oktoba, 2018.   Aidha, nawapongeza wananchi wa Jimbo la Jang’ombe kwa kuendelea kukiamini Chama cha Mapinduzi kuwa ndio Chama pekee kinachoweza kusimamia amani, utulivu na mshikamano wa nchi na kuwaletea maendeleo ndani ya nchi yao. 

Mheshimiwa Spika, mkutano huu tumejadili kwa kina Miswada mitatu ambayo ni:-
i.     Mswada wa Sheria ya Kuweka Masharti Yanayosimamia Utoaji wa Huduma za Msaada wa Kisheria, Kurahisisha Upatikanaji wa Haki na Kuweka Masharti Mengine Yanayohusiana na Hayo.
ii.      Mswada wa Sheria ya Kufuta Sheria ya Ukuzaji na Kulinda Uchumi Zanzibar Nam. 11 ya mwaka 2004 na Kutunga Sheria ya Mamlaka ya Ukuzaji na Kulinda Vitega uchumi Zanzibar na kuweka Masharti Mengine yanayohusiana na Hayo.
iii.   Mswada wa Sheria ya Kufuta Sheria ya Vyama vya Ushirika Nam. 4 ya Mwaka 1986 na Kutunga Sheria ya Vyama vya Ushirika Zanzibar ya Mwaka 2018 ambayo inaweka utaratibu wa Uundaji na Uendeshaji ya Vyama vya Ushirika na Mambo Mengine Yanayohusiana na Hayo.

Mheshimiwa Spika, ni imani yangu Miswada hiyo mitatu (3) tuliyoipitisha itakapokuwa Sheria itasaidia kuondoa changamoto mbali mbali tulizozijadili ambazo  zilipelekea haja ya kuwa na Miswada hii. Mbali na Miswada hii Baraza lako Tukufu pia lilipokea taarifa ya Serikali kuhusu hoja ya Mjumbe ya kuitaka Serikali kuja na mkakati unaotekelezeka kwa kutatua changamoto zinazowakabili wakulima wa zao la mwani. 

Mheshimiwa Spika, Halikadhalika, Baraza lilipokea hoja mbili kutoka kwa Waheshimiwa Wajumbe ikiwemo hoja inayotaka Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kutoka Viti Maalum vya Wanawake kufaidika na fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo, na Hoja ya kutaka kuliomba Baraza lako Tukufu kutoa maazimio ya kushughulikia tatizo la kuharibika kwa vifaa tiba   kwenye Hospitali ya Abdulla Mzee iliyoko Mkoani, Pemba.   Serikali imeichukua hoja hiyo na kwenda kuifanyia kazi na hatimae itakuja na majibu muafaka yatakayoweza kuondoa matatizo yaliyokuwepo katika eneo hilo.  Mbali na hayo Waheshimiwa Wajumbe walipata nafasi kuuliza maswali ya msingi 123 na maswali ya nyongeza ...... ambayo yote yalijibiwa kwa mfasaha na Waheshimiwa Mawaziri.
  
Mheshimiwa Spika, kama tujuavyo tarehe 3 Disemba ya kila mwaka ni Siku ya Watu Wenye Ulemavu Duniani. Zanzibar kama nchi nyengine tumeadhimisha siku hii na mimi nilibahatika kuwa Mgeni Rasmi. Miongoni mwa mambo yanayowakwamisha watu wenye ulemavu ambayo yanawapa usumbufu mkubwa na mara nyengine huwa wanadhalilika ni kutokana na miundombinu isiyokuwa rafiki kwao. Majengo yetu mengi yamejengwa bila kuzingatia mahitaji ya watu wenye ulemavu ambayo yanawapa usumbufu mkubwa na mara nyengine huwa wanadhalilika katika kuzifikia huduma muhimu za kijamii kutokana na miundombinu iliyopo. Kwa mara nyengine tena, napenda kutoa wito kwa vyombo vyote nchini vinavyohusiana na ujenzi wa miundombinu yote pamoja na majengo kuzingatia muongozo wa Serikali wa miundombinu rafiki ambao unaelezea upatikanaji wa haki na fursa za watu wenye ulemavu kuweza kuzifikia huduma zitolewazo bila ya vikwazo, kwani tuelewe sisi sote ni walemavu watarajiwa, hivyo tunahitaji kujitengenezea miundombinu ambayo isiyomkwaza au kumpa shida mwengine katika maisha yake.

Mheshimiwa Spika, mwezi huu wa Disemba tarehe 1 tuliadhimisha Siku ya Ukimwi Duniani.   Miongoni mwa malengo ya nchi yetu kama zilivyo nchi nyengine duniani katika kupambana na maradhi haya thakili ya ukimwi ni kuzifikia shabaha za 90 tatu (90-90-90) ifikapo mwaka 2020, ili kumaliza maradhi ya UKIMWI ifikapo mwaka 2030. Katika kuzifikia shabaha hizo tumefanikiwa kuzifikia 90 mbili za mwanzo. Kwa ufafanuzi Tisini ya mwanzo maana yake ni asilimia 90 ya watu wanaoishi na VVU wawe wanajitambua.  Hadi kufikia Septemba mwaka huu, asilimia 92 ya watu wanaokisiwa kuishi na VVU tayari wanajitambua (kwa lugha nyengine watu 5,861 kati ya watu 6,393 wanaoishi na VVU tayari wanajitambua). Tisini ya pili maana yake asilimia 90 ya wale wanaojitambua wawe wanatumia dawa za kupunguza makali ya VVU umaarufu kama ARVs. Shabaha hii nayo Zanzibar tayari tumeifikia. Hadi kufikia Septemba asilimia 98 ya wanaojitambua wanatumia dawa za ARVs (kwa lugha nyengine watu 5,725 kati ya watu 5,861 wanaojitambua kuambukizwa na virusi vya ukimwi wanatumia ARVs). Bado hatujaifikia shabaha ya 90 ya tatu inayotaka asilimia 90 ya wale wanaotumia dawa za ARVs wawe na kiwango cha chini cha virusi mwilini.  Hadi kufikia Septemba tulifikia asilimia 76, naamini kwa kushirikiana vizuri na wagonjwa, watoa huduma na jamii kwa ujumla 90 hiyo nayo ifikapo mwaka 2020 tutaweza kuifikia bila ya matatizo.

Mheshimiwa Spika, ukimwi bado upo unaathiri nguvu kazi ya Taifa na bado hauna dawa. Wito wangu kwa wananchi wenzangu kuchukua juhudi za makusudi kutumia ipasavyo huduma za upimaji ili kuitendea haki kauli mbiu ya mwaka huu “Pima Virusi vya Ukimwi ujue Afya Yako”.

Mheshimiwa Spika, maradhi yasiyoambukiza (Non-Communicable Diseases - NCD) hivi sasa yanaongezeka kwa kasi ya kutisha duniani kote kwa mujibu wa wataalamu wetu wa afya. Maradhi haya yakiwemo kisukari, shindikizo la damu (pressure), tezi dume na saratani ya shingo kizazi yapo pia hapa kwetu na ndio maana hata Jumuiya inayohusika na maradhi yasiyoambukiza imeundwa hapa Zanzibar. Miongoni mwa mambo ambayo yatasaidia kupambana na maradhi haya ni kupima afya zetu mara kwa mara, kufanya mazoezi pamoja na kupendelea kula vyakula vya asili badala ya vyakula vya makopo.

Mheshimiwa Spika, Nawaomba Waheshimiwa Wajumbe tujitokeze kwenda kupima ili tujue afya zetu mapema.  Tupime tezi dume japo mara moja kwa miezi sita, tusiogope upimaji wake pamoja na saratani ya shingo ya kizazi.  Sisi ni Viongozi na Viongozi huongoza kwa mifano bora.  Naamini tukiwa mstari wa mbele katika kupambana na maradhi haya yasiyoambukiza wananchi wetu watakuwa nyuma yetu.  Kinga ni bora kuliko tiba. Tuutumie usemi huu kumpambana na maradhi yasiyoambukiza kwa kwenda kupima afya zetu.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imejidhatiti kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto kwa nguvu zake zote. Takwimu za mwaka 2017/2018 zinaonyesha kuwa matukio 1,091 yameripotiwa kutoka Jeshi la Polisi ukilinganisha na matukio 2,449 yaliyoripotiwa mwaka 2016/2017. Takwimu hizi bado hazifurahishi ijapokuwa kutokana na jitihada mbali mbali matukio haya yamepunguwa kwa mwaka 2017/2018. Hivyo basi, inaonyesha wazi tukijipanga vizuri tunaweza kabisa kupunguza vitendo hivi na hatimaye kuvimaliza kabisa.
Uzoefu unaonyesha kuwa vitendo vya ukatili na udhalilishaji hufanywa na watu wa karibu na familia na jambo la kusikitisha zaidi pale watu tunaowaamini kama walimu wa Madrasa na Skuli kushiriki katika vitendo hivi. Matukio ya vitendo hivi zaidi hufanywa kwa watoto kuliko watu Wazima. Takwimu kutoka jeshi la Polisi zinaonyesha kwamba asilimia 88.8 ya matukio yaliyopokelewa kwa mwaka 2017/2018 yalikuwa ni ya watoto.

Mheshimiwa Spika, ukitaka kuiangamiza nchi kiurahisi basi chezea elimu yake.  Udanganyifu wa mitihani ni miongoni mwa vitendo vya uhalifu vyenye nia ya kuiangamiza nchi yetu kimaendeleo. Hakuna Serikali makini duniani itakayokubali kuchezewa elimu yake.  Kwa maana hiyo udanganyifu wa mitihani ya Taifa ya Darasa la 10 au Form II uliotokea na kulazimisha Serikali kufuta mitihani yote haukubaliki hata kidogo. Serikali itachukuwa hatua kali dhidi ya wale wote waliohusika na uhalifu huu. Tutang’oa miti hata kama ni mikubwa kama mbuyu, miche, mizizi na mbegu zinazosubiri kuchipua ili tukio hili lililotia aibu Serikali yetu lisitokee tena.   Napenda kumpongeza Mhe. Riziki Pembe Juma, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali kwa umakini wake mkubwa wa kufuta mara moja mtihani wote wa Darasa la 10 baada ya kugundua kuvuja kwa mtihani huo.

Nawaomba wananchi wote wa Zanzibar washirikiane na Serikali katika kupiga vita uhalifu huu ambao ukiachiwa utaliangamiza Taifa letu. Natoa agizo kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuchukua tahadhari zote ili udanganyifu wa mitihani Zanzibar usitokee tena.  Aidha, naviomba vyombo vya ulinzi na usalama kufanya upelelezi wa kina na kuwapeleka Mahakamani mara moja wale wote waliohusika na udanganyifu wa mitihani hiyo.

Mheshimiwa Spika, Zanzibar ni nchi inayoongozwa na kuendeshwa katika misingi ya utawala bora na kufuata sharia ilizojiwekea.  Hata hivyo, hivi karibuni kumekuwa na tabia ya baadhi ya watu kupuuza au kutofuata na kutoheshimu Sheria zilizowekwa kwa baadhi yao wasio waaminifu kwa sababu wanazozijua wao wenyewe katika Taasisi mbali mbali za umma na kusababisha madhara makubwa kwa jamii yetu.

Kwa mfano, tulitunga sheria ndani ya Baraza hili kuhusu uvaaji wa kofia ngumu (helmet) kwa vyombo vya maringi mawili, na ukipita njiani utakuta wasimamizi wa Sheria hiyo na watekelezaji wanapuuza kwa kiasi kikubwa.  Hivyo, natoa wito kwa Jeshi la Polisi kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo bila muhali wala upendeleo. Kwani kupuuza utekelezaji wa Sheria hiyo ni kuhatarisha maisha ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia hotuba yangu nakushukuru wewe Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, Katibu wa Baraza na timu yake yote kwa kuliendesha    Baraza hili Tukufu kwa ueledi wa hali ya juu. Aidha, nawashukuru Waheshimiwa Wajumbe kwa kutumia nafasi yenu ya kidemokrasia ya kuisimamia, kuishauri na kuihoji Serikali, jambo ambalo limeonesha nia thabiti mliyonayo ya kuitaka Serikali yenu kuwajibika ipasavyo kwa wananchi wake.  Kadhalika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kujibu maswali yote mliyoulizwa; mliweza kuyatolea ufafanuzi vizuri na kwa usahihi yote maswali yaliyoulizwa kwa lengo la kuwafahamisha wananchi wetu jinsi Serikali yao inavyowatumikia. Aidha, napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ufafanuzi alioutoa katika mambo mbali mbali yaliyohitaji ufafanuzi wa kisheria.

Kwa namna ya pekee navishukuru vyombo vya habari kwa kazi yao nzuri ya kuwawezesha wananchi walioko majumbani kufuatilia yaliyokuwa yanatokea ndani humu.  Nawaomba Waheshimiwa Wajumbe tuendelee kupendana, kuvumiliana na kushirikiana katika kuijenga nchi yetu kiuchumi na kijamii kwani mshikamano na umoja wetu ndio utakaoivusha nchi yetu kuelekea kwenye maendeleo endelevu.


Mheshimiwa Spika, nawashukuru wananchi wote wa Zanzibar kwa namna walivyoutumia vyema mwaka 2018 katika shughuli za uzalishaji na ninawatakia kheri ya mwaka mpya wa 2019 Mungu atujaalie kheri, salama na mapenzi baina yetu.  Uwe ni mwaka wa mavuno mengine, na ambao Mwenyezi Mungu atuondoshee maradhi kwa wagonjwa wetu na kuipa nguvu Serikali yetu ili itekeleze kwa ufanisi wa hali ya juu malengo iliyojiwekea kwa ajili ya watu wake.  Aidha, nawaomba wananchi wote wajitokeze kwa wingi kusherehekea miaka 55 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar siku itakapowadia katika kiwanja cha Gombani, Pemba kwenye upepo mwanana wa marashi ya karafuu.

Mwisho, napenda kuwapongeza Wakalimani wetu wa lugha za alama ambao wamefanya kazi nzuri ya kuwajulisha watazamaji wetu wenye ulemavu wa kusikia kilichokuwa kinaendelea ndani ya Baraza lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, Baada ya maelezo hayo, naomba sasa kwa heshima na taadhima kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu liakhirishwe hadi siku ya Jumatano tarehe 06 Februari, 2019, saa 3.00 barabara za asubuhi panapo majaaliwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.