Habari za Punde

TADMAC Wakutana Kujadili na Kuweka Mikakati ya Kuzuia na Kukabiliana na Majanga

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu) Prof. Faustine Kamuzora akizungumza wakati akifungua kikao cha Baraza la Usimamizi wa Maafa Tanzania (TADMAC)  leo Jijini Dodoma  ikiwa ni kikao cha pili cha Baraza hilo.
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Usimamizi wa Maafa Tanzania (TADMAC) wakifuatilia hafla ya ufunguzi wa kikao cha Baraza hilo leo Jijini Dodoma.
Sehemu ya watendaji na Idara ya maafa kutoka  Ofisi ya Waziri Mkuu na Wajumbe wa Baraza la Usimamizi wa Maafa Tanzania (TADMAC)  wakifuatilia kikao cha Baraza hilo leo Jijini Dodoma. 

(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Na; Mwandishi wetu;                                                                                                                                
Baraza la Usimamizi wa Maafa Tanzania (TADMAC) limekutana leo Jijini Dodoma na kuweka mikakati ya pamoja yakukabiliana na kuzuia  majanga .

Hayo yamesemwa na Katibu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera na Uratibu Prof. Faustine Kamuzora wakati akifungua kikao cha Baraza hilo leo Jijini Dodoma  ikiwa ni kikao cha pili .

“ Baraza hili limepewa jukumu kubwa na muhimu la kusimamia masuala yote yanayohusu maafa yanayotokana na majanga ya aina zote hapa nchini”. Alisisitiza Prof. Kamuzora

Akifafanua amesema kuwa, Serikali inaendelea kusisitiza kuimarisha hatua za kuzuia na kupunguza madhara ya majanga mbalimbali kwa kuhakikisha kuwa mipango ya maendeleo inazingatia viashiria vilivyopo katika sekta  mbalimbali.

Kila Taasisi katika ngazi zote zinatakiwa kujiandaa katika maeneo yao kwa kusaidia upatikanaji wa rasilimali za usimamizi wa maafa, Pia kutoa elimu kwa umma namna ya kuzuia majanga yanayoweza kuathiri shughuli za uzalishaji mali katika maeneo mbalimbali.

Alitaja baadhi ya matukio ya majanga yaliyojitokeza katika kipindi cha Januari hadi Disemba 2018 na kusababisha maafa kuwa ni pamoja na mafuriko katika Wilaya 50, upepo mkali ulioambatana na mvua kubwa katika  Wilaya saba, radi katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita na ajali iliyohusisha kivuko cha Mv Nyerere.

Kutokana na maafa hayo Serikali ilichukua hatua mbalimbali kwa kushirikiana na wadau kuokoa maisha, kutoa huduma kwa wananchi ikiwemo makazi ya muda, maji na chakula.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuzijengea uwezo kamati za maafa katika ngazi zote kuanzia Mikoa, Wilaya na Vijiji ili zitekeleze majukumu yao kwa weledi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Dkt Agness Kijazi amesema kuwa wamejipanga kuhakikisha kuwa wanaendelea kutoa taarifa za hali ya hewa kwa wakati ili zisaidie wadau na wananchi kuchukua tahadhari.

Aliongeza kuwa wataendelea kutoa taarifa za utabiri wa hali ya hewa kwa wakati na kutoa elimu kwa umma juu ya matumizi ya taarifa hizo.

Naye Msimamizi wa Mfumo wa Kitaifa wa Huduma za Hali ya Hewa Bi Mecklina Merchades amesema kuwa mfumo huo unasaidia kuwawezesha wananchi kutumia taarifa hizo kufanya maamuzi sahihi na wakati.


Kikao cha pili cha Baraza la Usimamizi wa Maafa Tanzania kimefanyika kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 7 ya mwaka 2015 ambayo pamoja na mambo mengine inaunda Baraza hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.