Habari za Punde

Rais Dk Shein afanya mazungumzo na Mratibu Mkuu wa Programu ya Kujitolea ya Umoja wa Mataifa (UNV) Oliver Adam, Ikulu



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Zanzibar                                                                 19.03.2019
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Mratibu Mkuu wa Program ya Kujitolea ya "United Nations Volunteers " (UNV) Bw,Oliver Adam kushoto,alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na Rais leo 19-3-2019.(Picha na Ikulu)


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza azma ya Umoja wa Mataifa (UN) kupitia programu yake ya  kujitolea ya Umoja huo (UNV) kwa kuendea kuiunga mkono Zanzibar katika shughuli za maendeleo.


Dk. Shein aliyasema hayo  leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Mratibu Mkuu wa Programu ya Kujitolea ya Umoja wa Mataifa (UNV) Oliver Adam, aliyefika Zanzibar kwa lengo la kuimarisha mashirikiano baina ya pande mbili hizo.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Mratibu huyo kuwa (UNV) ni programu muhimu iliyo chini ya Umoja wa Mataifa ambayo ina umuhimu mkubwa katika kuendeleza shughuli mbali mbali za maendeleo hapa Zanzibar.

Alieleza kuwa progmu hiyo ya Umoja wa Mataifa imeanza miaka mingi  na kuwez kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kuendeleza na kuunga mkono juhudi za serikali katika shughuli za maendeleo ikiwemo sekta ya afya, kilimo na sekta nyenginezo.

Aidha, Rais Dk. Shein alimueleza Mkuu huyo kuwa tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanzisha Kituo cha Ujasiriamali ambacho kinatoa mafunzo kwa vijana ya kazi za aina mbali mbali za ujasiriamali ambapo kuna haja ya kukiongezea uwezo pamoja na kuwapatia mtaji vijana hao ili wanaufaike na elimu wanayoipata.

Pia, alisisitiza kuwa kuna haja ya kuweka mikakati maalum ya kuwajengea uwezo vijana wote wa Unguja na Pemba ili waweze kujiajiri wenyewe kwa kuwapa mikopo midogo midogo itakayowasaidia kujiendeleza na hatimae kujiajiri.

Pia, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya Programu hiyo ya (UNV) kuunga mkono katika kuongeza nguvu kwa kupata walimu wa masomo ya Sayansi kwa skuli za Sekondari za Zanzibar ambao bado wanahitajika kwa kiasi kikubwa.


Alieleza kuwa licha ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuweka mikakati maalum na kuyapa kipaumbele masomo ya Sayansi kwa kuwashajiisha wanafunzi kuyasoma kwa bidii na hatimae kujiendeleza katika vyuo vyake vitatu vikuu vilivyopo hapa nchini.

Aliongeza kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuwapata walimu na wataalamu wa masomo ya Sayansi ili kuondokana na upungufu uliopo ambapo tayari hata hivyo zipo nchi zinazosaidia kwa kuleta walimu wa masomo ya Sayansi ikiwemo Nigeria.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza uhaba wa madaktari wa upasuaji ambao bado wanahitajika katika kuimarisha sekta ya afya hapa nchini licha ya juhudi zinazochukuliwa na Serikali za kuwasomesha wataalamu wa kada hiyo.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Umoja wa Mataifa (UN) kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kuitumia programu ya kujitolea ya UN kwa kuiunga mkono Zanzibar .

Nae Mratibu Mkuu wa Programu ya Kujitolea ya Umoja wa Mataifa (UNV) Oliver Adam alimueleza Rais Dk. Shein azma ya Progmau hiyo katika kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza shughuli mbali mbali za maendeleo.

Mratibu Mkuu huyo alimuhakikishia Dk. Shein pamoja na kuihakikishia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa (UNV) iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika kuhakikisha shughuli zote za kujitolea zinazosimamiwa na Umoja wa Mataifa (UN) na Zanzibar nayo itafaidika.

Aidha, Mratibu Mkuu huyo alieleza azma ya (UNV) ya kusaidia kuendeleza miradi kadhaa hapa Zanzibar sambamba na kuzifanyia kazi hoja za Rais Dk. Shein za kuwawezesha vijana, kuimarisha sekta ya afya kwa kuongeza uwezo kwa madaktari wapasuaji pamoja na walimu wa masomo ya sayansi na nyenginezo.

Mratibu Mkuu huyo, alimueleza Dk. Shein kuwa (UNV) ina uzoefu na umahiri mkubwa katika suala zima la shughuli za kujitolea zinazoendeshwa na Umoja wa Mataifa kupitia programu hiyo, hivyo itautumia kwa kuendelea kuisaidia Zanzibar.

Programu ya kujitolea ya Umoja wa Mataifa (UNV) imekusudia  kusadia kufanikisha mikakati mbali mbali inayoendeshwa na Serikali ili kuimarisha hali ya kujitolea nchini kwa manufaa ya taifa.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.