Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Habari Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar.




RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, aliipongeza Wizara hiyo kwa mafanikio yaliopatikana pamoja na kupongeza hatua zilizochukuliwa hadi kufikia Kampuni ya DSTV kurusha matangazo ya Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) moja kwa moja.  

Hayo aliyasema leo, katika ukumbi wa Ikulu ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale wakati ilipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Rais Dk. Shein aliwakumbusha viongozi na watendaji wa Wizara hiyo umuhimu wa kukumbuka historia ya kuwepo kwa Chanel ya ZBC2, hivyo akawataka kuitumia vyema fursa iliopo ili Televisheni hiyo iendelee kuonekana katika maeneo tofauti ndani na nje ya nchi.

Aidha, alielezea azma ya Serikali ya kujenga jengo kwa ajili ya kuhifadhia mitambo ya kuchapia madaftari, kwa kigezo kuwa kiwanda cha uchapaji ni muhimu katika kuliingizia Taifa mapato sambamba na kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza haja ya kuufufuwa mchezo wa Golf hapa nchini kwa lengo la kushajiisha uimarishaji wa sekta ya Utalii, sambamba na kushirikiana na taasisi binafsi ikiwemo Hoteli ya Sea Cliff katika kufanikisha dhamira hiyo.

Alieleza kuwa Serikali itaendelea kuzisaidia na kuziunga mkono na kuzisimamia taasisi zote zilizo chini ya Wizara hiyo bila ya upendeleleo huku akisisitiza haja ya uongozi wa Wizara hiyo kuendelea kuwahimiza watendaji wake kufanya kazi kwa ufanisi kwa lengo la kupata tija na mafanikio bora zaidi.

Mapema Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, alitumia fursa hiyo kuipongeza Wizara hiyo  na kuieleza jinsi alivyofanya ziara za kutembelea taasisi za Serikali za habari na kukutana na kufanya mazungumzo na watendaji wake.

Balozi Seif alisisitiza haja kwa taasisi za habari ambazo zinamadai kwa taasisi nyengine kuendeleza mikakati yao ya kufuatilia madai yao ili fedha zitakazopatikana ziendelee kusaidia na kuleta tija kwa Serikali na kufikia azma iliyokusudiwa.

Alieleza umhimu wa Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), kuifanya redio yake ya ZBC kuzidi kusikika ndani na nje ya Zanzibar.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alieleza haja kwa uongozi wa Wizara hiyo kujua azma ya Serikali ya kuiweka Wizara hiyo kuwa na sekta ya habari, utalii na mambo ya kale ambapo utegemezi wa sekta hizo ni muhimu katika mashirikiano ya pamoja hasa katika kujitangaza.

Alisisitiza haja ya kukaa na kufanya kazi kwa pamoja kwa lengo la kuendeleza na kuimarisha sekta  ya utalii.

Nae Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo alieleza kuwa Wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii imefanikiwa kuandaa tamasha la Urithi wa Utamaduni wa Mtanzania (Urithi Vestival).

Alieleza kuwa wizara imepokea vifaa vya kisasa vya kazi za Digitali na kuhuisha nyaraka zilizochakaa kutoka kwa Washirika wa Maendeleo wa Serikali ya Oman vyenye thamani ya zaidi ya TZS 89,204,100 ambavyo ni kwa ajili ya kuhuisha na kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka kwa matumizi ya sasa na baadae.

Aidha, Waziri Kombo alieleza kuwa Wizara hiyo imeandaa kwa mara ya kwanza kwa kushirikiana na sekta binafsi Tamasha la Utalii la Zanzibar ambalo lilifunguliwa rasmi na Rais Dk. Shein Novemba 17 mwaka jana 2018 katika hoteli ya Verde Mtoni Zanzibar.

Sambamba na hayo, Waziri huyo alieleza mafanikio ya Wizara kwa kuwasiliana na Kampuni ya DSTV ambayo inarusha matangazo yake karibu duniani kote, ambapo hatua za kufungua ofisi hapa Zanzibar zimekamilika ambapo hivi sasa wanafanya matengenezo ya jengo la ofisi lililopo Mlandege Unguja hatua ambayo pia itopanua soko la ajira katika tasnia ya utangazaji.
 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.