Habari za Punde

Sekta ya Utalii Inaimarika na Kuendelea Kuleta TijaSambamba na Kuongeza Pato la Taifa.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesisitiza haja kwa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kuendelea kuviimarisha vivutio vya utalii kutokana na utajiri mkubwa uliopo wa vivutio hivyo hapa Zanzibar.

Dk. Shein aliyasema hayo katika ukumbi wa Ikulu ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale wakati ilipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar imebarikiwa kuwa na vivutio vingi vya kitalii ikifananishwa na nchi za ukanda wa Afrika Mashariki hivyo kuna kila sababu ya kuviimarisha vivutio hivyo ili vizidi kuwavutia watalii wa ndani na nje ya Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa upande wake itaendelea kutoa msukumo kupitia Wizara yake hiyo ili kuhakikisha sekta ya utalii inaimarika na kuendelea kuleta tija sambamba na kuongeza pato la taifa.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza haja kwa Wizara hiyo kuendeleza michezo ambayo itakuwa ndio kivutio cha watalii hasa ile ambayo ilikuwepo siku za nyuma na kuweza kuitangaza Zanzibar kwa kiasi kikubwa ukiwemo mchezo wa Gofu.  

Akieleza mafanikio yaliopatikana Zanzibar, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kutokana na kuimarisha kwa uchumi wake mafanikio makubwa yameweza kupatikana na kuipelekea Serikali kutekeleza miradi kadhaa ambayo haipo kwenye Bajeti wala kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM, ukiwemo ujenzi wa barabara na daraja la Kibondemzungu, Mwanakwerekwe na miradi mengineyo.


Mapema Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, alisisitiza haja kwa Wizara hiyo kufanya utaratibu na kuweka ratiba maalumu kwa viongozi ili kwenda kuangalia vivutio vya kitalii vikiwemo mapango na magofu.

Alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia na hasa kwa viongozi kuzidi kuendelea kuutangaza utalii wa Zanzibar kwa kutoa taarifa na maelezo pale wanapokuwa nje ya nchi ambapo huweza kuzungumza na viongozi pamoja na watu mbali mbali wakiwemo wawekezaji wa sekta ya utalii.

Nae Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo alieleza hatua za kuimarisha sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kuimarisha maeneo ya kihistoria ya Fukuchani kwa upande wa Unguja na Mkamandume kwa Pemba ambapo Wizara imefanikiwa kuyaimarisha maeneo hayo.

Alieleza kuwa utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa eneo la Mkamandume umeanza kwa kutengeneza njia maalum ya bahari ambayo ilikuwa ikitumika kwa njia ya kusafirishia jahazi njia ambayo ikitokea katika usawa wa bahari hadi kwenye jengo la Mkamandume pamoja na ujenzi wa kuta za ngome hiyo.

Aidha, Wizara imelifanyia matengenezo makubwa jengo la ngome ya kihistoria ya Wareno ya Fukuchani kwa kuzijenga upya kuta za jengo hilo, kuweka milango na madirisha mapya, kuliezeka paa la bati pamoja na kujenga kuta zinazozizunguka ngome hiyo.

Waziri Kombo alisisitiza kuwa maeneo hayo ya kihistoria yanachangia kwa kiasi kikubwa katika kukusanya mapato ya fedha za kigeni ambapo wageni kutoka mataifa mbali mbali hupata fursa ya kuyatembelea.

Sambamba na hayo, Waziri Kombo alieleza hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara hiyo katika kutekeleza Mradi wa kuimarisha Utalii kwa Wote ambao unahusu ujenzi wa kituo cha utalii katika eneo la Bi Khole huko Bungi Wilaya ya Kati Unguja.

Alieleza kuwa Mkandarasi wa ujenzi huo ameshapatikana ambaye ni Quality Building Contractor na tayari ameshaanza hatua za ujenzi ambapo katika awamu ya kwanza ya mradi huo unategemea kutekeleza shughuli za uwekaji sawa muonekano wa ardhi pamoja na kuweka njia katika eneo.

Aliongeza kuwa shughuli nyengine ni kutengeneza bustani, kujenga mikahawa 10 kwa ajili ya utoaji wa huduma za vyakula mbali mbali, ujenzi wa baraza za kukalia zenye uwezo wa kukalia watu 2000 kwa wakati mmoja pamoja na ujenzi wa vyoo na maegesho ya gari.

Waziri huyo anaehusika na sekta ya utalii alieleza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaongeza vivutio vya utalii, kuimarisha utalii wa ndani na kimataifa pamoja na kuongeza ajira kwa jamii hasa vijana.

Aidha, uongozi wa Wizara ulieleza juhudi zinazochukuliwa na Shirika la Magazeti ya Serikali katika kuhakikisha linatoa habari zake ndani na nje ya nchi kwa kutumia jumla ya mitandao sita ya kijamii ikiwemo Twitter, Istagram, Youtube, Facebook, Tovuti pamoja na gazeti mtandao (Online).

Pia, uongozi huo wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale ulieleza namna juhudi za makusudi zinavyochukuliwa katika kuuimarisha utalii hasa katika kisiwa cha Pemba ambapo ulieleza kuwa kwa kipindi hichi wageni wengi wamekuwa wakikitembelea.

Aidha, uongozi huo ulieleza ujio wa meli maalum ya kitalii kisiwani humo ambayo itakuwa na watalii kutoka maeneo mbali mbali duniani watakaofika kwa ajili ya kuangalia vivutio kadhaa vilivyopo kisiwani humo.

Uongozi wa Wizara hiyo pia, ulieleza kuwa miongoni mwa vivutio kadhaa vilivyopo kisiwani Pemba vikiwemo vile vya asili pia, watalii wengi wamekuwa wakivutiwa na chumba cha hoteli ya Mantarif ambacho kiko chini ya bahari.

Sambamba na hayo, uongozi huo pia ulitoa pongezi na shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa maelekezo,busara na hekima aliyonayo katika kuwaongoza hatua ambayo imekuwa chachu ya mafanikio katika Wizara hiyo.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.