Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Mwakilishi wa INICEF Nchini Tanzania Bi. Maniza Zamani alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa Kazi Nchini Tanzania.
SHIRIKA la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Watoto Duniani
(UNICEF) limepongeza mikakati iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya
kuwahudumia watoto ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta
ya afya na elimu.
Mwakilishi wa UNICEF
katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anaemaliza muda wake wa kazi Bi Maniza
Zaman aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.
Mwakilishi huyo wa UNICEF ambaye alifika Ikulu kwa ajili ya
kumuaga Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweza
kupata mafanikio makubwa katika kuwahudumia watoto sambamba na kuhakikisha
wanapata haki zao za msingi ikiwemo kupata elimu na afya bora.
Alieleza kuwa Shirika hilo
linathamini juhudi hizo na limeweza kushuhudia mafanikio na mabadiliko makubwa katika
sekta za maendeleo hatua ambazo zimewawezesha watoto wa Zanzibar na wao kuweza
kupata haki zao za msingi pamoja na mahitaji yao muhimu ya kimaisha.
Bi Zaman alimuhakikishia
Rais Dk. Shein kuwa Shirika hilo litaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika
juhudi zake hizo na kueleza kuwa miongoni mwa mafanikio makubwa yaliopatikana
katika sekta ya afya ni pamoja na kupungua kwa vifo vya akina mama na watoto
kwa kiasi kikubwa hapa Zanzibar.
Aidha, Mwakilishi huyo
alimpongeza Dk. Shein kwa juhudi zake kubwa anazozichukua katika kupiga vita
vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto, maradhi mbali mbali
yakiwemo kipindupindu, Malaria na mengineyo huku akiahidi Shirika hilo
kuendelea kuisaidia sekta hiyo hapa nchini.
Mwakilishi huyo
alieleza kuwa UNICEF itaendelea na programu mbali mbali hapa Zanzibar ikiwa ni
pamoja na zile za kusaidia jamii hasa watoto mjini na vijijini sambamba na kuwawezesha
kiuchumi.
Nae Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wake
amelipongeza Shirika la UNICEF kwa juhudi zake za kuendelea kuiunga mkono
Zanzibar na kumpongeza Mwakilishi wa Shirika Bi Zamani kwa utendaji wake mzuri
wa kazi katika kipindi chake chote alichokuwepo Tanzania.
Katika maelezo yake
Dk. Shein alisema kuwa Shirika la UNICEF lina historia kubwa na mashirikiano
kati yake na Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo
sekta ya afya, elimu sambamba na kuimarisha ustawi wa akinamama na watoto hapa Zanzibar.
Aidha, Dk. Shein alisema
kuwa Shirika hilo limeendelea kutoa ushirikiano na msaada mkubwa kwa watoto wa
Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuanzisha programu kadhaa ambazo zimeweza kusaidia
katika kuleta maendeleo endelevu kwa watoto na jamii kwa ujumla.
Pamoja na hayo, Dk.
Shein alieleza juhudi zilizochukuliwa katika kupambana na vifo vya akinamama na
watoto, ambapo Zanzibar imepiga hatua kubwa hasa pale ilipoanzisha mapambano
dhidi ya Malaria jambo ambalo limefanikiwa.
Rais Dk. Shein
aliupongeza uongozi huo wa (UNICEF) nchini Tanzania na kueleza kuvutiwa kwake
na mikakati pamoja na programu mbali mbali zilizowekwa na Shirika hilo katika
kuhakikisha linaendelea kuwasaidia watoto katika nyanja mbali mbali.
Alieleza kufurahishwa
na mipango kabambe iliyowekwa na Shirika hilo katika kuendelea kuiunga mkono
Zanzibar katika nguzo zake nne ilizoziweka ikiwa ni pamoja na kuimarisha afya
kwa watoto, ukatili dhidi ya wanawake na watoto,kuwawezesha wanawake kiuchumi
pamoja na kuunga mkono Mpango wa Maendeleo endelevu (SDG).
Aidha, Dk. Shein
alimueleza kiongozi huyo wa (UNICEF) hapa nchini anaemaliza muda wake mikakati
madhubuti iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tokea Mapinduzi ya
Januari 12, 1964 katika kuhakikisha inaimarisha sekta zake za maendeleo ikiwemo
sekta ya elimu na sekta ya afya ambazo zote kwa pamoja zina dhima kubwa katika
kuwaendeleza na kuwahudumia watoto wa Zanzibar.
Alisema kuwa katika
sekta zote mbili za afya na elimu tayari Serikali imeshatangaza kuwa huduma za
afya kwa wananchi ziwe bure kama ilivyokusudiwa katika malengo ya Mapinduzi
sambamba na sekta ya elimu ambapo kwa elimu ya msingi na sekondari zote ni
bure.
Dk. Shein alieleza
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuzisimamia vyema, Sera,
Kanuni na Sheria zinazowahusu watoto katika kupata haki zao za msingi na huduma
za kijamii sambamba na kuahidi kuendelea kushirikiana na Mashirika ya Umaoja wa
Mataifa likiwemo Shirika la (UNICEF).
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment