Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Balozi wa Brazil Nchini Tanzania.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Balozi wa Shirikisho la Jamuhuri ya Brazil Nchini Tanzania Mhe Antonio Augusto Cesar alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuna umuhimu mkubwa wa kuendeleza ushirikiano uliopo kati ya Zanzibar na Brazil kwa maslahi ya wananchi wa nchi mbili hizo.

Dk. Shein amesema hayo leo Ikulu mjini hapa, wakati alipokuwa na mazungumzo na Balozi wa Shirikisho la Jamhuri ya Brazil nchini Tanzania Antonio Augusto Cesar aliefika kwa ajili ya kujitambulisha.

Dk. Shein alisema Zanzibar na Brazil zina uhusiano wa muda mrefu na zimekuwa zikishirikiana katika masuala mbali mbali ya maendeleo, ikiwemo ya kiuchumi na kijamii

Alisema pamoja na nchi hizo kutofautiana kwa ukubwa wa eneo na kupatikana katika Mabara tofauti, zimekuwa zikishirikiana kwa karibu, huku Zanzibar ikiwa na mengi ya kujifunza kutoka nchi hiyo, ikiwemo suala la kuiendeleza sekta ya Utalii.

Alisema Zanzibar ambayo kabla ilikuwa ikilitegemea zao la Karafuu kuendesha uchumi wake, imebarikiwa kuwa na vivutio na rasilimali kadhaa za Utalii hususan kupitia uchumi wa bahari (Blue Economy), eneo ambalo kuna mambo mengi ya kufanya.

Dk. Shein alimweleza Balozi huyo dhamira  ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuvutia Wawekezaji kutoka Brazil katika nyanja mbali mbali, ikiwemo sekta ya Utalii, ili kuimarisha uchumi wake.

Alisema pamoja na kuwepo sheria na miundombinu iliyo bora kuelekea maeneo ya Uwekezaji, Zanzibar inajivunia  kwa kuwepo hali ya amani na usalama muda wote hivyo kutoa fursa adhimu ya kuwekeza.

Aidha, Dk. Shein alimhakikishia Balozi huyo kuwa Zanzibar na Tanzania ujumla zina matarajio ya kupata maendeleo makubwa kutokana na kuwa na viongozi imara, hatua aliyosema imeziwezesha nchi hizo kufikia miaka 55 ya Muungano wake ikiwa salama.

“Leo hii ni miaka 55 tangu nchi hizi kuungana, Muungano umebaki imara.  nchi nyingi zimejaribu kufanya hivyo, lakini zimeshindwa”, alisema Dk. Shein.

Katika hatua nyengine Dk. Shein alipongeza azma ya Brazil kuendelea kushirikana na Zanzibar katika suala zima la kuimarisha huduma za Afya, ili kuleta ustawi wa wananchi.

Nae, Balozi wa Shirikisho la Jamuhuri ya Brazil nchini Tanzania, Antonio Augusto Cesar alimweleza Dk. Shein hatua mbali mbali zinazochukuliwa na Uongozi wa nchi yake katika kuleta ustawi wa kiuchumi, kisiasa  na kijamii kwa wananchi wa Taifa hilo.

Alisema Brazil imeazimia kuendeleza ushirikano na Zanzibar katika nyanja mbali mbali ikiwemo sekta ya Afya ili kuimarisha afya za wananchi.

Aidha, alisema kuna umuhimu mkubwa wa kuendeleza mashirikiano na Zanzibar ili kuimarisha sekta ya Utalii, akisifia mandhari na vivutio mbali mbali vilivyopo hapa nchini, na hivyo akaahidi kutumia fursa iliyiopo kuvutia Wawekezaji kutoka nchini Brazil.

Wakati huo huo, Balozi wa Heshima wa Shirikisho la Jamuhuri ya Brazil hapa Zanzibar, Abdulsamad Abdurahman, amesema zaidi ya vijana 37 kutoka  Zanzibar na wachache kutoka Tanzania Bara, wanatarajiwa kushiriki katika mkutano maalum wa Kibiashara utakalofanyika nchini Brazil, baadae mwezi ujao.

Alisema vijana hao walioandaliwa watashiriki katika mkutano huo wa siku kumi utakaoanza Juni, 28, 2019 kwa ajili ya kuitangaza Zanzibar kupitia sekta za Utalii, Biashara, Kilimo, pamoja na viungo ikiwemo Karafuu.

Alisema kupitia mkutano huo  utakaowashirikisha wadau mbali mbali kutoka Chamber na Incubator za huko,  viijana hao wataangazia fursa za kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza Zanzibar katika sekta mbali mbali pamoja na kufanya ubia na wawekezaji wa huko.

“Hivi sasa tayari kuna wawekezaji wapatao sita kutoka Brazil waliowekeza hapa, tunafanya juhudi ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi”, alisema.

Aidha, Balozi huyo alisema wawapo nchini Brazil, ujumbe huo utatembelea miji ya Brasilia, Sao Paolo pamoja na Rio de Geneiro, ambako utapata fursa ya kujionea shughulli mbali mbali za viwanda vidogo vidogo, Mafuta na Gesi, mashamba ya ufugaji kuku, utengenezaji wa na uhifadhi ya nyama ya ngombe na sekta  yenginezo.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.