Katibu Mkuu Wizara ya Vijana Michezo Utamaduni na Sanaa Zanzibar Ndg. Omar Hassan King, akisoma Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara yao, wakati wa mkutanio huo,ukiongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, katika Ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa ni jambo baya
sana na halikubaliki katika jamii kwa wasanii kuibiwa kazi zao na wajanja
wachache ambao hujinufaisha wao.
Dk. Shein aliyasema leo, katika ukumbi wa Ikulu
ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Vijana,
Utamaduni, Sanaa na Michezo wakati ilipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango
Kazi wa Wizara hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.
Rais Dk. Shein alisema kuwa ni vyema sheria
ikatazamwa na kama kuna haja ya kuangaliwa kwa kufanywa marekebisho basi ni vyema
jambo hilo likafanyika kazi ipasavyo ili kuondosha kabisa dhulma hiyo
wanayofanyiwa wasanii wakiwemow asanii wakongwe.
Alisema kuwa imekuwa ni utamaduni hivi sasa kwa
baadhi ya watu kuzitumia kazi za wasanii kwa kujinufaisha wao huku wakiwaacha
wasanii husika kutopata kipato ama faida zozote za kazi zao na badala yake
wajanja hao wakajinufaisha wao.
Hivyo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuwekwa
mikakati maalum katika kutafuta taratibu na ufumbuzi wa suala hilo kisheria na
kusisitiza haja ya kutizamwa sheria iliopo hivi sasa kama inakidhi haja juu ya
suala hilo ama inahitaji marekebisho.
Aidha, Rais Dk. Shein alieleza haja kwa uongozi wa
Wizara hiyo kwa kupitia Idara yake ya Utamaduni na Sanaa ikalifanyia kazi suala
zima la kivazi cha Mzanzibari mwanamke na mwanamme na jinsi kinavyovaliwa.
Rais Dk. Shein pia, alisisitiza haja kwa Wizara
kutizama jinsi ya matumizi na kazi za studio mpya ya kisasa iliyojengwa na Serikali
kwa fedha nyingi hapo Rahaleo ambapo iwapo ingelitumika vyema ingekuwa mkombozi
mkubwa kwa wasanii wa Zanzibar.
Alieleza kuwa wasanii wa Zanzibar wana uwezo
mkubwa wa kutengeneza filamu mbalimbali kwa kutumia studio hiyo mpya zikiwemo
za maigizo na maonesho na kuipa sifa kubwa Zanzibar kama ilivyo kwa nchi
nyengine duniani.
Rais Dk. Shein pia, alieleza haja kwa Wizara hiyo
kubuni shughuli mbali mbali za kuwaendeleza vijana kwa kuwapatia miradi mbali
mbali sambamba na kutoa taaluma kwa kuwafanya wawe wazalendo ili waweze
kuilinda nchi yao.
Alisisitiza haja kwa Wizara kuwadhibiti vyema
vijana kwa kuwasaidia kwa nyenzo mbali mbali za kujiimarisha miradi ya kielimu
baada ya kujiunga katika vikundi.
Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza Wizara hiyo kwa kuwasilisha
vyema Mpango Kazi wake na kutoa nasaha zake kwa Wizara katika kuwasimamia
vijana ambao ndio kundi kubwa katika jamii.
Dk. Mzee alieleza kuwa Rais ameiunda Wizara hiyo
kutokana na kushabihiana sekta zake ikiwemo Sanaa, utamaduni na michezo ambazo
nazo iwapo zitafanyiwa kazi vizuri zinaweza kuzalisha ajira.
Mapema Naibu Waziri wa Wizara ya hiyo Lulu Msham
Abdalla alieleza kuwa Wizara kwa kushirikiana na Wizara nyengine imekamilisha
zoezi la utambuzi wa mahitaji ya vijana kwenye maeneo ya kilimo, ufugaji,
mafunzo ya kazi na ushonaji ambapo jumla ya vijana 4029 watanufaika.
Alieleza kuwa Wizara imefanikiwa kuhakikisha kuwa
utamaduni, mila, silka za Wazanzibari zinaenziwa, zinaendelezwa kwa manufaa ya
Taifa kwa kumia matamasha mbali mbali, vikundi vya Sanaa ikiwemo Kikundi cha
Taifa cha Taarab na kikundi cha ngoma asilia.
Aidha, alieleza kuwa Wuzara hiyo imefanikiwa
kulinda haki za wasanii na Sanaa zao
kupitia BASSFU na Ofisi ya Hakimiliki ambapo pia jumla ya matamasha
manane yamefanyika, kazi za Sanaa 379 zimekaguliwa, jumla ya watumiaji 305 wa
kazi za Hakimiliki kibiashara wamekaguliwa na mirahaba yenye thamani ya TZS
105,128,266 itagaiwa kwa wasanii na wabunifu 1,277.
Pia, Naibu Waziri huyo alieleza kuwa Wizara
imefanikiwa kukamilisha Kongamano la Pili la Kitaifa la Kiswahili na maonyesho
ya vitabu vya lugha na elimu, lililoshirikishs wataalamu 237 kutoka nchi mbali
mbali zikiwemo Marekani, Pakistani,Misri, Rwanda, Sweeden, Japan, Kenya,
Uganda, Austria, Tanzania Bara na Zanzibar.
Pamoja na hayo, alisema kuwa Wizara imefanikiwa
kukamilisha Sera ya Michezo na imeanza kutumika huku akieleza jinsi Wizara
ilivyofanikiwa kukamilisha matengenezo makubwa ya kiwanja cha Mao-Zedong na
matengenezo madogo kwa kiwanja cha Gombani na Amaan Stadium.
Sambamba na hayo alieleza kuwa kwa upande wa mradi
wa ujenzi wa viwanja vya Wilaya eneo la Mkokotoni Wilaya ya Kaskazini “A”
limeshapatikana na hatua ya kukamilisha michoro zinaendelea pamoja na
kupatikana kwa eneo la Kama JKU Wilaya ya Magharibi “A”, limeshapatikana na
taratibu za awali zinaendelea.
Pia, alieleza kuwa viwanja vya Wilaya ya Kusini
(Kangani) na Kaskazini (Kishindeni) Pemba vimo katika hatua za kukamilika.
Akisoma Utekelezaji wa Mpango Kazi Katibu Mkuu wa
wizara hiyo Omar Hassan (King) alieleza mikakati iliyowekwa na Serikali katika
kuiendeleza Wizara hiyo.
Wakati huo
huo, Rais
Dk. Shein alikutana na uongozi wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais na kutoa
pongezi kwa mashirikiano na juhudi kubwa zinazochukuliwa na uongozi wa Ofisi
hiyo kwa kumsaidia Makamo wa Pili wa Rais katika shughuli zake za kazi.
Dk. Shein alieleza kuridhika kwake na uwasilishaji
na utayarishaji wa Mpango Kazi wa Ofisi hiyo ambao umewasilishwa vizuri huku
akiusisitiza uongozi wa Ofisi hiyo kuendelea kushauriana kwani ndio msingi wa
kazi.
Nae Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd
alieleza mashirikiano na umoja wa viongozi pamoja na wafanyakazi wa Ofisi hiyo
ambayo yamekuwa chachu ya mafanikio yaliopatiana huku akimpongeza Dk. Shein kwa
kuendelea kumuongoza vyema.
Mapema akitoa muhtasi wa taarifa ya Utekelezaaji
wa Mpango Kazi wa mwaka 2018/2019 kwa kipindi cha robo tatu kuanzia Julai 2018
hadi Machi 2019 Waziri wa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais
Mohamed Aboud Mohamed alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa uongozi wake wenye
ufanisi mkubwa.
Waziri Aboud alisema kuwa Zanzibar imepata
mafanikio makubwa ambayo yameimarisha ustawi bora wa maisha ya wananchi, misingi
ya usawa, demokrasia na utawala bora inayopelekea kuimarika kwa uwajibikaji wa
viongozi na watendaji wa Serikali.
Alieleza kuwa Ofisi imeendelea kupambana na
uharibifu na uchafuzi wa mazingira kwa kutoa elimu kwa jamii juu ya uhifadhi wa
mazingira ikiwa ni pamoja na upigaji marufuku mifuko ya plastiki pamoja na
kufanya operesheni ya kusimamia maliasili zisizorejesheka.
Pia, aleleza jinsi Ofisi hiyo ilivyoendelea
kufuatilia na kuipatia ufumbuzi migogoro inayojitokeza katika maeneo mbali mbali
hapa nchini pamoja na kutoa elimu kwa jamii juu ya masuala ya kukabiliana na
maafa.
Aidha, alieleza kuwa Ofisi imechukua jitihada za
kulihami eneo la fukwe la Msuka ili lisiendelee kumungonyoka kutokana na maji
ya bahari kwa kuandaa utaratibu wa kujenga ukuta maalim utakaogharamiwa na
serikali.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment