Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Afanya Ziara Kukagua Vifaa UUB Kibele Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Wafanyakazi wa Idara ya Ujenzi na Utunzaji wa Barabara Zanzibar (UUB) alipofanya ziara kutembelea Vifaa Vipya vya Ujenzi wa Barabara Zanzibar katika Kituo cha UUB Kibele Wilaya ya Kati Unguja, kushoto Waziri wa Ujenzi Mawasiliani na Usafirishaji Zanzibar Mhe.Dr. Sira Ubwa  na Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe Mohammed Ahmed Salum. 

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewahakikishia wananchi kuwa ahadi zote zilizotolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kutengeneza barabara kubwa na ndogo zitatekelezwa baada ya vifaa vipya na vya kisasa kuwasili.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipofanya ziara fupi ya kukagua vifaa vipya na vya kisasa vya kutengenezea barabara ukiwemo mtambo wa lami wa digitali ambavyo vimenunuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoka nje ya nchi ambavyo kwa hivi sasa vimewekwa Kibele, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.

Katika maelezo yake mara baada ya kukagua vifaa hivyo na kupata maelezo kutoka uongozi wa wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Dk. Shein alieleza kuwa ni azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutekeleza ahadi zake za ujenzi wa barabara ambazo iliahidi kwa wananchi.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilitoa ahadi kwa wananchi za ujenzi wa barabara mbali mbali za Unguja na Pemba lakini nyengine zilijengwa na nyengine bado hazijafanyiwa ujenzi kutokana na uhaba na ukosefu wa viifaa vya kutosha vya ujenzi wa barabara.

Alieleza kuwa kutokana na maamuzi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kununua vifaa vyake wenyewe kutakuwa ndio mkombozi mkubwa wa kutekeleza ahadi hiyo kwa azma ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa ndani ya kipindi chake cha uongozi atahakikisha ahadi zilizotolewa za ujenzi wa barabara zinatekelezwa baada ya Serikali kununua vifaa hivyo vipya na vya kisasa vya digitali.

“ Furaha yangu ni kwamba kazi hii itakamilika na hatimae tutajenga wenyewe, kwa fedha zetu wenyewe na wataalamu wetu wenyewe kwa vifaa vyetu wenyewe na kwa nguvu zetu wenyewe kwani azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kufanya hivyo”,alisisitiza Rais Dk. Shein.

Aliwaeleza wafanyakazi wa Wizara hiyo kuwa vifaa hivyo ambavyo vimewasili kwa awamu ni vipya, na vimeagizwa kutoka Kampuni zenye sifa duniani kutoka nchi za Itali, Brazil, Ujerumani, Japan pamoja na  India hivyo ni vyema vikatunzwa na kuenziwa ili visijeonekana ni vya mtumba hasa ikizingatiwa kuwa gharama yake ni kubwa kwani vifaa hivyo vimegharimu TZS Bilioni 10.3.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa Wizara hiyo kuhakikisha barabara zilizoharibika zinatengenezwa ikiwa ni pamoja na kuwekwa viraka kwa baadhi ya barabara zilizofanya mashimo ambayo wakati mwengine husababisha foleni ya gari na hata kusababisha ajali.

Hata hivyo, Rais Dk. Shein amekubali rai ya uongozi wa Wizara hiyo ya kujengwa uzio katika eneo hilo ili kuhakikisha usalama wa vifaa hivyo sambamba na kukabidhiwa hati miliki ya eneo hilo hasa ikizingatiwa kuwa eneo lote katika sehemu hiyo ni la Serikali.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliuagiza uongozi wa Wizara hiyo kuhakikisha inawawekea mazingira mazuri wafanyakazi wake sambamba na kuwaandaa watalamu kwa lengo la kuendesha na kusimamia Idara hiyo ya Barabara ili kuepusha kukimbiwa na wataalamu ambao hufuata maslahi kwenye Kampuni binafsi.

Alieleza kuwa Serikali inahitaji wataalamu hivyo jitihada zifanyike za kuwaajiri vijana waliomaliza masomo ya kada zote kwani kwa wale waliofika kiwango cha Shahada hata za Sheria basi wanafundishika katika fani hiyo ya ujenzi kwani jambo la muhimu ni kuwapa mafunzo japo ya muda mfupi juu ya fani hiyo kwani wanafundishika.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuzishukuru na kuzipongeza Kampuni binafsi ambazo zilishirikiana na Serikali wakati palipokuwa na uhaba na ukosefu wa vifaa kwa kujenga na kukarabati barabara kadhaa hapa nchini na kuzitaka ziendelee licha ya kuwa hivi sasa Serikali tayari imeshapata vifaa vyake.

Alieleza kuwa kupata vifaa hivyo isiwe ndio mwisho wa mashirikiano kwani tayari kumeshajengwa mahusiano na udugu kati ya Serikali na Kampuni hizo zilizojenga barabara kwa upande wa Unguja na Pemba.

Aliongeza kuwa kwa vile ujenzi wa barabara unagharimu fedha nyingi hivyo, ujenzi wa barabara iwapo utaendeshwa na Idara husika ya Barabara gharama hizo zitapungua na kuleta afuweni kubwa kwani hilo ndio lengo la Serikali na ndio maana imeamua kununua vifaa hivyo kwa ajili ya kujenga barabara za Unguja na Pemba.

Nae Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Dk. Sira Ubwa Mwamboya alieleza furaha aliyonayo kwa ujio wa vifaa hivyo na kusema kuwa hatua hiyo itasaidia na kutoa nafasi kubwa kwa ujenzi wa barabara ambao ulizorota kutokana na uhaba na ukosefu wa vifaa.

Alisema kuwa  kununuliwa kwa vifaa hivyo, kutafikisha asilimia mia moja ya uwezekano wa  ujenzi wa barabara mbali mbali hapa nchini ambapo pia, zitajengwa kwa wakati sambamba na kufikia malengo ya utekelezaji wa ujenzi wa barabara kutokana na ahadi zake anazozitoa.


Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mustafa Aboud Jumbe aliemueleza Rais Dk. Shein aina za vifaa viliyonunuliwa na vile ambayo vimeshawasili ukiwemo mtambo wa kupikia lami kutoka nchini Brazil, makatapila,  paver, magrader,mabuldoza, excaveta,gari ya kuwekea lami ya maji, vijiko, na vifaa vyenginevyo huku akiahidi ujio wa gari 10 kutoka nchini India mnamo Julai mwaka huu.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa ununuzi wa vifaa hivyo vyenye thamani ya zaidi ya TZS Bilioni 10.3 unatokana na agizo alilolitoa Rais Dk. Shein mnamo Septemba 2016 wakati alipofanya ziara ya kutembelea sehemu hiyo na kuona mtambo wa kupikia lami pamoja na vifaa ambavyo vilikuwa vimechakaa.

Alieleza kuwa vifaa hivyo vitasaidia kwa kiasi kikubwa katika ujenzi wa barabara ya Charawe na Ukongoroni ambao tayari umeshaanza pamoja na ujenzi wa barabara ya Ole-Kengeja unaoendelea huku akieleza kuwa tayari lami tani 400 kati ya tani 1000 imeshawasili.

Pamoja na hayo, Katibu Jumbe alisema kuwa wataalamu wa kuja kutoa mafunzo juu ya uendeshaji wa vifaa hivyo wanatarajiwa kuwasili Julai 2 mwaka huu 2019 na kueleza kuwa vifaa hivyo nusu vitapelekwa Pemba na nusu vitabaki Unguja kwa kuendelea na shughuli za ujenzi wa barabara huku akiomba kupatiwa hati miliki sambamba na ujenzi wa uzio katika eneo hilo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.