Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Ujumbe wa Taasisi ya Al-Hikma Ikulu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Ujumbe wa Taasisi ya Al-Hikma Foundation ya Jijini Dar es Salaam walipofika Ikulu Zanzibar kujitambulishwa, ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu Sheikh Nurdin Kishki kushoto na Sheikh Suleiman Khamis Habib.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein ameitaka taasisi ya Al – Hikma Foundation  kuzingatia kiwango chenye uwiano kwa washiriki wa Zanzibar, pale inapoandaa mashindano ya kuhifadhisha Qur-ani.

Alhaj Dk. Shein amesema hayo Ikulu mjini Zanzibar, alipokutana na Uongozi wa taasisi ya Al-Hikma Foundation kutoka Jijini Dar es Salaam, uliofika kujitambulisha pamoja na kumuombea dua ya kumtakia maisha mema na uongozi bora.

Alhaj Dk. Shein alisema kuna umuhimu mkubwa kwa taasisi hiyo pale inapofanya shughuli zake, hususan zinazoambatana na mashindano ya kuhifadhi Qur-ani pamoja na upatikanaji wa fursa mbali mbali zikiwemo za kijamii, kuzingatia umuhimu wa kuongeza kiwango cha kuishirikisha Zanzibar kwani kiwango cha sasa ni kidogo.

Alisema amevutiwa sana na juhudi zinazofanywa na Taasisi hiyo na kubainisha mafanikio yaliofikiwa kuwa ni matunda yanayotokana na kuwepo kwa viongozi bora, sambamba na kuitaka kuendelea kuitumia kikamilifu fursa ya kuwa na mlezi mahiri Alhadj Ali Hassan Mwinyi.

Aidha, Alhaj Dk. Shein alisema usimamizi wa mashindano ya kuhifadhisha Qur-an kunakofanywa na taasisi hiyo ni njia bora katika kuwajenga watoto kupenda kuhifadhi qur-an, akibainisha umuhimu wa jambo hilo kwa msingi kuwa ni lazima Qur-an ihifadhiwe na kuendelezwa.

Alisema Mwenyezi Mungu ameahidi kuihifadhi Qur-an, hivyo ni jukumu  la waumini wanaume na wanawake pamoja na watoto kuisoma kikamilifu.

Alisema Zanzibar ina historia ya kuwa chemchem ya dini ya kiislamu na kueleza kuwa kwa nyakati tofauti imefanikiwa kutowa  wanazuoni mashuhuri katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, hivyo akatowa wito kwa watu mbali mbali kuja kujifunza masuala ya dini ya kiislamu.

Alhaj Dk. Shein aliipongeza taasisi hiyo kwa kufikisha miaka 22 tangu kuanzishwa kwake, sambamba na kutekeleza jukumu lake la kusimamia mashindano ya Qur-an kwa kipindi chote hicho.

Aidha, akaipongeza taasisi hiyo kwa hatua mbali mbali inazozichukuwa katika uimarishaji wa huduma za kijamii, ikiwemo uchimbaji wa visima na ujenzi wa misikiti, hatua aliyosema ni amali nzuri na muhimu kwa jamii ya Watanzania.

Nae, Mwenyekiti wa Al-hikma Foundation, Sheikh Nurdin Muhammed Ahmeid Al-Ahdal ‘Kishki’ alisema Qur-an ni msingi wa dini na yule mwenye kuifahamu huwa mcha Mungu na raia mwema.

Alisema Kamati iliyoundwa kwa ajili ya kuhifadhisha Qur-an kutoka taasisi hiyo, pamoja na shughuli nyengine pia inajishughulisha na suala la kuhubiri amani nchini kwa kuzingatia umuhimu wake kama  ulivyobainishwa katika dini ya kiislamu.

Aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, inayoongozwa Rais Dk. Shein kwa kutoa fursa kwa wananchi wake katika kuendeleza dini, hatua inayoliwezesha Taifa kupata matokeo mazuri katika mashindano mbali mbali ya kitaifa na kimataifa.

Vile vile, Mwenyekiti wa Al-Hikma Foundation Zanzibar, Omar Hussein Mussa, alimhakikishia Alhaj Dk. Shein kuwa taasisi hiyo  inafanya kazi zake kwa kuzingatia pande mbili za Muungano, akibainisha hekma zake zimeiwezesha kufanikisha shughuli hizo kwa uwazi na mafanikio makubwa.

Alitoa rai kwa serikali kuipatia eneo la ujenzi taasisi hiyo, ili iweze kuanzisha rasmi Tawi lake hapa Zanzibar, hatua itakayofungua milango ya uendelezaji wa huduma mbali mbali za kijamii zinazofanywa na taasisi hiyo, kama vile uchimbaji wa visima, ujenzi wa misikiti nauanzishaji wa skuli za msingi na sekondari.

Aidha, Mwenyekiti huyo alimueleza Alhaj Dk. Shein kuwa kupitia Jumuiya ya Kuhifadhisha Quran Zanzibar , watoto kadhaa wamepata mafanikio ya kuwa washindi katika mashindano tofauti ya kuhifadhi Quran yaliofanyika katika nchi mbali mbali Barani Afrika.

Ujumbe huo wa watu 13 uliosimamia mashindano ya Kimataifa ya kuhifadhisha Qur-an yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, ulikuwa Zanzibar kwa takriban wiki moja kwa mapumziko baada ya kufanikisha vyema mashindano hayo, ambapo mtoto Shamsuddin Hussein Ali (21) kutoka Zanzibar alikuwa mshindi wa tatu.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.